August 20, 2014





Na Saleh Ally
SASA ni uhakika kwamba Barcelona itamtumia Luis Suarez katika safu yake ya mashambulizi kuhakikisha inarejesha makombe yaliyopukutika.


Mataji ya Copa del Rey, La Liga na Ligi ya Mabingwa Ulaya yalikuwa ni mambo ya kawaida kabisa katika kikosi hicho ambacho msimu uliopita kilitoka kapa.

Kutoka katika chuo chake cha soka cha La Masia, aina ya uchezaji wa Barcelona umekuwa kivutio kikubwa, lakini ndani ya misimu miwili mambo yameonekana kwenda sivyo.

Baada ya kuondoka Pep Guardiola na nafasi yake kupewa Tito Vilanova ambaye sasa ni marehemu, taratibu kasi ya kikosi hicho cha Balaugrana ilianza kuporomoka.

Hata baada ya kupewa Kocha Tata Martino, bado mambo hayakuwa na mabadiliko makubwa, naye baada ya msimu mmoja, akaondoka kurejea kwao Argentina.

Kikosi kimerudishwa kwa mmoja wa magwiji wa Barcelona, Luis Enrique aliyekuwa mmoja wa viungo wa pembeni wenye kasi kubwa.

Kurudi kwa Enrique ni jambo bora, lakini usisahau kuongezeka kwa fowadi mpya Luis Suarez sasa kumekamilika.

Kukamilika kwake ni baada ya juhudi za kumtetea apunguziwe adhabu baada ya kufungiwa miezi minne kutokana na kumng’ata beki wa Italia, Giorgio Chiellini, wakati wa Kombe la Dunia nchini Brazil. Sasa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), limemruhusu afanye mazoezi na Barcelona na kucheza mechi za kirafiki.

Ujio wa Suarez unaifanya fowadi ya Barcelona kuundwa na watu watatu hatari zaidi lakini wote wanatokea Amerika ya Kusini.

Unaonekana umekuwa ni utamaduni, kwamba Barcelona inaamini zaidi washambuliaji nyota kutoka Amerika Kusini kama ilivyokuwa kwa Ronaldo Lima, Romario, Ronaldinho na baadaye Lionel Messi.

Sasa ina Neymar na Suarez na usisahau msimu uliopita, mmoja wa tegemeo alikuwa ni Alexis Sanchez aliyetua Arsenal.

Barcelona wanategemea zaidi fowadi kutoka kusini mwa Amerika na swali linaweza kupata majibu pale Suarez atakapoanza kuichezea mwishoni mwa Oktoba katika mechi ya El Classico dhidi ya Real Madrid.

Suarez alifunga mabao 31 na kuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu England ambayo ina mikiki na ngumu kwelikweli. Neymar akiwa mgeni alipiga mashuti 68 katika La Liga na kufunga mabao 11.

Messi akiwa amepiga mashuti 160 na pasi 11 za mabao, hiyo ni msimu uliopita. Amekuwa mfungaji bora zaidi ya mara mbili, msimu uliopita pamoja na kuwa majeruhi, alifunga mabao 28.

Wote watatu, jumla walifunga mabao 70, wana nafasi ya kufunga zaidi ya hayo na kama kweli wakiwa na Barcelona halafu wakafunga kwa idadi hiyo, hakuna shaka kikosi hicho 
kitakuwa na nafasi ya kutwaa kombe au makombe.
SOURCE: CHAMPIONI JUMATANO 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic