August 18, 2014




Na Mwandishi Wetu
MECHI ya Agosti 23, yaani Jumamosi ijayo imekuwa ikizidi kupata umaarufu zaidi hasa baada ya waratibu wa ziara hiyo kuamua kuteua kikosi cha wachezaji nyota wakongwe wa Tanzania.


Kikosi cha nyota wakongwe wa Tanzania kitakuwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, kuwavaa nyota wakongwe wa Real Madrid.

Awali kulikuwa na taarifa kwamba waliamua kutumia kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars kuwavaa wakongwe hao wa Real Madrid, lakini taarifa zilibadilika na sasa ni zamu ya wakongwe wa Tanzania.


Kampuni ya Tanzania Sisi ni Nyumbani (TSN), ambao ni waratibu, imepongezwa zaidi kwa wazo hilo la pili la kuwatumia wakongwe wa Tanzania.

Baadhi ya wakongwe waliotajwa kuunda kikosi hicho ni Mohammed Mwameja, Manyika Peter, Salum Sued, Shadrack Nsajigwa, Boniface Pawasa, George Masatu, Shabani Ramadhani, John Mwansasu, Salvatory Edward, Sabri Ramadhani ‘China’, Mao Mkami na Abubakar Kombo.

Wengine ni Malota Soma, Abubakari Kombo, Clement Kahabuka, Habib Kondo, Mtwa Kihwelo, Steven Nyenge, Dua Said na Edibily Jonas Lunyamila.




Wazo la kuteua wakongwe wenzao limekuwa kivutio zaidi na huenda ikawa ni kipimo cha wachezaji wetu, soka yetu na soka lao ambao wamecheza katika kiwango cha juu.

Katika listi iliyotolewa inaonyesha kuwa kuna wachezaji wenye rekodi za juu kabisa ikiwa ni pamoja na kubeba mataji ya Ulaya kwa ngazi za klabu na taifa lakini wako waliocheza kwenye Kombe la Dunia na wengine kulitwaa kama ilivyo kwa Zinedine Zidane.


Waliotajwa kuwa watakuja nchini ni Ruben de Lared, Michael Salgado, Luis Figo, Cristian Karembeu, Michael Owen, Steve McManamann, Zinedine Zidane na wengine ambao Watanzania wangependa kuwaona wakionyeshana kazi na nyota wa Tanzania.

Kwa kikosi hicho cha wakongwe dhidi ya wakongwe wa Madrid, kutakuwa na mambo mengi ya kuvutia, mfano Luis Figo, mmoja wa mawinga wenye kasi raia wa Ureno atakapokuwa akionyeshana kazi na Shadrack Nsajigwa au Abubakari Kombo.

Au winga mwenye kasi wa Tanzania, Akida Makunda ambaye pamoja na kuwa na umri mkubwa lakini bado ameendelea kuwa na kasi ya juu, atakuwa akipambana na Michel Salgado.

Burudani zitakuwa nyingi na kama Zidane atakuwa miongoni mwao, katikati pale upande wa nyota wa Tanzania kuna watu kama Sabri Ramadhani ‘China’, Mao Mkami ‘Ball Dancer’.

Katikati mtu kama Mwansasu na Pawasa wanaweza kazi, ingawa mashabiki wamekuwa wakiomba kuongezwa kwa beki ngangari, Bakari Malima ‘Jembe Ulaya’.

Mbele Tanzania itakuwa inasukuma mashambulizi na watu kama Malota Soma ‘Ball Juggler’, Dua Said na Clement Kahabuka ambaye uwezo wake wa kufunga bado uko juu sana.

Kikubwa ambacho kinatakiwa kwa waandaaji ni kuwaandaa wakongwe hao wa Tanzania kwa kuwapa maandalizi mazuri na ya kiwango cha juu.

Lakini wakongwe hao pia wanapaswa kujituma na kujiweka sawa kwa ajili ya mechi hiyo kwa kuwa hawapaswi kuamini mechi itakuwa rahisi hata kidogo.

Mechi itakuwa ngumu kwa kuwa kwa utaratibu, timu hiyo ya wakongwe wa Real Madrid inatambulika na uongozi wa klabu hiyo.

Inatunzwa na iko kwenye hesabu za klabu, wamekuwa wakifanya mazoezi mara mbili kwa wiki, tena kwenye vifaa vinavyotumiwa na ile timu kubwa iliyo na akina Cristiano Ronaldo, Gareth Bale na wengine.

Kama unakumbuka, Championi ndiyo lilikuwa gazeti la kwanza kuandika kuhusiana na ujio wa Real Madrid, huenda watu wakadhani ni utani au ‘changa’ kama ambavyo wamekuwa wakiona kwingine.

Lakini sasa yanatimia na aliyelihakikishia Championi mapema kwamba kweli timu hiyo inakuja alikuwa ni Rayco Garcia, mchezaji wa zamani wa timu ya vijana ya Barcelona na baadaye Real Madrid.

Garcia alilihakikishia Championi kuwa wakongwe hao wa Madrid wako fiti na wanacheza soka katika kiwango cha uhakika kwa kuwa wana programu ya uhakika kabisa ya mazoezi.

Alionya soka la vurugu, kwamba kama ni soka sawa, lakini si ‘kurukiana’. Lakini akasisitiza kwamba soka watakaloonyesha litakuwa funzo kwa timu yoyote, ndiyo maana walikuwa tayari hata kucheza na Taifa Stars.

Hivyo wakongwe wa Tanzania wajiandae kweli, la sivyo wataangukia kwenye aibu ya kufungwa mabao matano, sita au saba, kitu ambacho kitaharibu burudani wanayotaka kuiona Watanzania.


1 COMMENTS:

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic