September 22, 2014


KAMA kungekuwa na tuzo ya mdhamini bora wa Ligi Kuu Bara, basi moja kwa moja ingekwenda kwa kampuni ya kuuza matairi na betri za magari ya Bin Slum Tyres Limited ya jijini Dar es Salaam.

Sina uhakika kama Bin Slum ana matawi nje ya Jiji la Dar es Salaam, lakini kampuni hiyo imefanya mambo ambayo sasa ndiyo inapaswa kuwa njia sahihi kwa kampuni nyingine.
Nazungumzia kwenye soka, nasema Bin Slum ingeweza kupewa tuzo kutokana na uamuzi wake wa kishujaa, uamuzi wa kijasiri ambao unaonyesha ulilenga kusaidia hata kuliko faida.

Kampuni ipi ya kibiashara ambayo itafanya mchezo na suala linaloitwa faida? Lakini Bin Slum Ltd ni kampuni ambayo imejaribu baada ya kuamua kutoa udhamini kwa timu tatu za Ligi Kuu Bara.
Kwanza ni Mbeya City ambayo wameidhamini kupitia bidhaa za betri zake bora za RB na kumwaga zaidi ya Sh milioni 300 katika kipindi cha miaka mitatu, utakubaliana nami kwamba si jambo dogo.
Baada ya hapo, kampuni hiyo ikaamua kutoa udhamini mwingine kwa kampuni ya Stand United ya Shinyanga. Hapa ndiyo ujasiri unapoianzia, kwamba imekubali kuidhamini timu ambayo ndiyo imepanda tu daraja.
Kampuni ya Bin Slum haitokei Shinyanga, lakini imekubali kutoa udhamini wa vifaa pamoja na Sh milioni 50, lakini imechangia kwenye manunuzi ya basi la timu hiyo pia.
Kupitia matairi yake ya Double Star, Bin Slum imekuwa mdhamini wa Stand United ambayo ndiyo imepanda tu daraja. Hili ni jambo jema kwenye soka nchini.
Kama hiyo haitoshi, Bin Slum imeendelea kusambaa kwa kufunga safari hadi mkoani Mtwara na kuidhamini Ndanda FC kupitia matairi yake ya Vee Rubber. Hii ni timu pia iliyopanda daraja.
Utakumbuka timu chache za Ligi Kuu Bara zina wadhamini, lakini utaona timu zenye udhamini ni kubwa zenye majina kama Yanga au Simba. Kidogo Azam FC kwa kuwa msimu uliopita wamekuwa mabingwa.
Timu nyingine zimekuwa na mdhamini mmoja au hakuna kabisa. Jambo ambalo linatokana na kampuni nyingi kuingia woga kutokana na mambo mawili makubwa yanayojitokeza sana kwenye mchezo wa soka.
Kwanza, hofu ya kufanya kazi ya watu wasiokuwa na mpangilio wa mambo. Pili, kuamini kwa timu za ligi kuu ukiacha Yanga, Simba na Azam FC, nyingine ni vigumu sana kujitangaza.
Bin Slum hawakujali hilo, wameonyesha ujasiri na ndiyo maana kampuni nyingine zimeanza kujitokeza kuzidhamini Ndanda na Stand United kwa kuwa zinaona kumbe inawezekana kama ilivyofanya kampuni hiyo ya kuuza matairi.
Wapo wanaoweza kuona vibaya au haya kuipongeza kampuni hiyo ya Bin Slum. Lakini ukweli ni kwamba wanastahili pongezi ya kuwa chachu ya wengine kuona kuwa soka inaweza kuzitangaza bidhaa nyingi. Tumeona Benki ya Exim imeanza kuiunga mkono Bin Slum kwa kuidhamini Stand, wengine wajitokeze pia.
Lakini bado, wakati Bin Slum inakuwa mfano, inaweza kuzishawishi kampuni nyingine kuachana na kuamini Yanga na Simba tu, basi wanaodhaminiwa nao wafanye mambo yao kwa mpangilio.
Mfano kuvaa nguo za wadhamini kwa wakati unaotakiwa na kutekeleza mambo yaliyo kwenye mkataba ili kuondoa usumbufu kwa wadhamini ambao unaweza kuwakatisha tamaa na mwisho kuamini soka si sehemu sahihi kuingiza fedha zao.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic