October 8, 2014


WIKI ILIYOPITA, mashabiki kadhaa wa Coastal Union walishikiliwa katika kituo kimoja cha polisi mjini kwa madai walikuwa wanauza jezi za Coastal Union za msimu uliopita ambazo zilikuwa zina nembo ya mdhamini ajulikanaye kama Sound.


Sound ni nembo iliyokuwa inatumika wakati kampuni ya Bin Slum Tyres Ltd ikiidhamini Costal Union msimu uliopita. Msimu huu Wagosi wa Kaya wanadhaminiwa na bidhaa ya Pembe.

Pamoja na kukamatwa, ikaelezwa uongozi wa Coastal Union ndiyo ulishitaki, mashabiki hao walikana kuuza jezi hizo. Lakini kukazuka hali ya kutoelewana kati ya mashabiki hao na uongozi baada ya viongozi kuwataka kutoingia uwanjani kuishangilia Coastal Union wakiwa wamevaa jezi hizo.


Vijana hao wakaweka msisitizo kwamba hawakuona kama kuna tatizo lolote kuhusiana na wao kuvaa jezi za Coastal Union bila ya kujali zina nembo ya mdhamini yupi.

Walisema zina nembo ya Coastal Union, hivyo wakakataa kutekeleza agizo hilo na kuingia uwanjani wakiwa wamezivaa, wakaishangilia Coastal Union kwa nguvu na mwisho ikashinda kwa mabao 2-1 dhidi ya Ndanda FC.
Uongozi wa Coastal Union haukutoa ushirikiano mzuri kwa gazeti hili, lakini baadaye lilifanikiwa kumpata Nassor Bin Slum, mmiliki wa Kampuni ya Bin Slum Tyres Ltd ambaye alikiri kuzisikia taarifa hizo za mashabiki wa Coastal Union kupelekwa kituoni, kisa walivaa jezi hizo na kusema anaamini haikuwa sahihi na si haki kuwafanyia hivyo mashabiki hao.

“Mimi nahoji kuna tatizo gani mashabiki wa Coastal Union kuvaa jezi za mdhamini wao wa zamani, tena wanaingia uwanjani kwenda kuishangilia timu yao, kuipa nguvu ishinde?” alihoji Bin Slum.

“Nauliza mfano, mwakani kama Coastal Union itapata mdhamini mwingine, halafu mashabiki wakavaa jezi zenye nembo ya Pembe ambaye ni mdhamini wa msimu huu, watakamatwa?”

“Kuna kitu cha kulifanyia kazi suala hili ili liende kiungwana, pia kuangalia umuhimu wa kuwa na Coastal Union moja badala ya kugombana na kutengana kwa sababu ya matakwa ya mtu au watu wachache.

“Coastal Union ni timu ya watu, tena watu wengi. Hivyo ni vizuri watu kuangalia nini watu wanataka na si mtu mmoja au wawili wanataka nini,” alisisitiza Bin Slum.



“Viongozi si weledi pia, ndiyo maana mimi niliwakimbia, utaona hapa kuna tatizo. Nilifikiri ilikuwa ni vizuri kupambana na wale wanaouza jezi feki mitaani.

“Vipi unampangia shabiki avae nini, angalia hata wale wa Manchester United wanavaa jezi za wadhamini waliopita kama AIG au za wadhamini wa zamani zaidi.

“Kama kweli wanataka watu wavae jezi nyingi za mdhamini wa sasa kumfurahisha kuna vitu vya kufanya.

“Waandae utaratibu mzuri wa kupatikana jezi hizo, zipatikane kwa wingi na ikiwezekana kwa bei rahisi watu wengi wavae wakiingia uwanjani.

“Mimi nasikia jezi mia mbili tu ndiyo zimeletwa, sasa uwanjani pale wanaingia mashabiki wangapi? Halafu unakasirika watu wasivae jezi za Sound!

“Hii inashangaza kidogo, kingine lazima wajue jezi wanazovaa ni za Coastal, si Sound au Bin Slum. Jezi wanazovaa ni za Coastal Union, ndiyo maana zina nembo ya klabu.

“Ingekuwa ni jezi ya Bin Slum pekee, isingekuwa na nembo ya Coastal Union, ungeweza kusema jambo, lakini bado utamzuia vipi mtu kuingia uwanjani na nguo au jezi anayoitaka? Vipi hawazuii jezi za Arsenal, Manchester United na nyingine kuvaliwa uwanjani, halafu wanazuia jezi yenye nembo ya klabu yao? Hakika wanapaswa kuipa heshima nembo ya klabu yao.

“Wakati wa jezi zenye nembo ya Sound, kulikuwa na utaratibu mzuri wa upatikanaji, bei ilikuwa chini. Sasa wanaweza kuiga utaratibu huo mzuri na wakati mwingine wakiweza wagawe bure angalau jezi kadhaa,” alisema.

Pamoja na Bin Slum, shabiki mwingine wa Coastal Union aliyejitambulisha kwa jina la Abdulatif Famau, alipiga simu kwenye ofisi za gazeti hili na kueleza kuwa analaani kitendo hicho cha uongozi.

“Mwisho polisi walilazimika kuwaachia wenzetu waliowashikilia na kusema hakuna kesi. Jiulize nani anaweza kushitakiwa kwa kuchagua avae jezi ipi?

“Halafu ile si jezi ya Sound au Bin Slum, ni jezi ya Coastal Union, ina nembo na inatambulika kabisa kwa kuwa imetumika msimu uliopita tu.

“Ajabu hata tukitaka jezi ya msimu huu, leo hii hazitapatikana. Sasa tatizo ni lipi? waulize viongozi wadhamini wameingia mkataba na klabu au sisi mashabiki. Nafikiri vizuri tufanye mambo ya kuisaidia klabu na timu yetu na si kuangalia maslahi binafsi,” anasema Famau, akionyesha kujiamini.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic