December 1, 2014


Na Saleh Ally
MIAKA 15 iliyopita, Ambwene Allen Yessayah aliamua kutoka chumbani alipokuwa baada ya kukata shauri kwamba anafanya muziki na kumfuata mama yake alipokuwa.


Yessayah sasa maarufu kama AY, alimfuata mama yake mzazi ambaye alikuwa mmoja wa walimu maarufu mkoani Morogoro na kumueleza nia yake ya kutaka kufanya muziki.

Safari hii alikuwa ‘siriaz’, alichoka mambo ya kuimba chumbani na alitaka kurekodi wimbo utakaosikika redioni, lakini fedha ndiyo lilikuwa tatizo kubwa.


“Niliamua kuwa wazi, nilimuomba mama shilingi elfu ishirini kwa ajili ya kurekodi wimbo. Mwisho alikubali kwa kuwa niliamini nikirekodi lazima utafanya vizuri, tutasikika na baada ya hapo tutaanza kupata fedha,” anasema AY katika mahojiano na gazeti hili.

“Hatukuwa na uwezo nyumbani, elfu ishirini ilikuwa nyingi lakini mama ni mama. Ingawa baba hakupenda mambo ya muziki. Kwa fedha hizo nikafunga safari hadi Dar es Salaam kwenye studio za Master J, kwa kushirikiana na wenzangu wa Kundi la OSG, tukarekodi wimbo wetu wa kwanza kwa shilingi elfu kumi.”

Wimbo wa kwanza wa kundi hilo lililokuwa linaundwa na marafiki watatu, AY, Buff G na Snare unajulikana kama ‘Kipi Kikusikitishacho’.

“Siku chache baada ya kuanza kupigwa redioni, ulifika Top Ten. Nakumbuka nikiwa Morogoro niliambiwa natafutwa na watangazaji wa East Africa kutaka kufanyiwa mahojiano, nikapanda basi kutoka Morogoro hadi Dar kumfuata Steve B.”

Hiyo ndiyo safari ya msanii maarufu wa muziki wa kizazi kipya, AY ambaye amekuwa akifanya vizuri kila kukicha.

Msanii ambaye Nasibu Abdul maarufu kama Diamond’ aliandika kwenye Mtandao wa Kijamii wa Instagram kuwa ndiye amewapa moyo wasanii kupambana hadi nje ya Tanzania.

Siku moja baadaye, akatupia ujumbe kwenye Instagram akisema anaamini Diamond atashinda tuzo mbili Channel O.

Siku chache, Diamond amefanikiwa kuchota tuzo tatu za Channel O, vipi AY alijua mapema?
“Niliamka asubuhi, moyo ukaniambia Diamond atashinda zaidi ya tuzo moja. Niliangalia vipengele anavyogombea, nikaona itakuwa ni zaidi ya tuzo moja atakayoshinda, ndiyo nikaandika.

“Najivunia Diamond, tumeshauriana mara kadhaa. Ukiona umemhamasisha mtu, halafu anafanikiwa, unasikia raha sana.

“Najua wapo waliochukia, lakini sasa ni wakati wa kumuunga mkono. Mwakani Tanzania ipeleke hata wanamuziki kumi kwenye Channel O. Nakumbuka nimekuwa nikienda peke yangu kutoka Tanzania, Kenya wanaleta wanamuziki kumi, kwa nini?

“Tena kabla tulikuwa tunashinda tuzo ya Afrika Mashariki tu, sasa Diamond ameshinda hadi msanii anayechipukia waliyokuwa wakishinda Wanigeria na Wasauz. Huu ndiyo wakati mwafaka, mwakani tuzo hiyo ije nyumbani tena.

“Tusione ni rahisi kwa Diamond au nilipofikia mimi ilikuwa rahisi tu. Lazima tujiamini, tujitume, tujikubali na kushirikiana maana hauwezi kuinuka peke yako.”

Team Diamond Vs Team Kiba:
“Nimekuwa nikisikia, kwamba wanashindana kupitia hizo timu. Sidhani kama huu ni wakati mwafaka, naona kama kuna watu wanataka kuwatumia kusingizia wanashindana.

“Waamke, waone mbele. Kiba na Diamond washikane mikono, wasonge mbele na kazi zao ni nzuri, hakuna haja ya hizo timu, mimi sioni kama ni sahihi.

“Nataka kuwaunga mkono Diamond na Kiba wakati wowote kwa kuwa mimi ni kati ya waliopigania muziki huu kufika hapa. Roho inauma nikiona mtu anafanya utani, nimesumbuka sana.
“Mfano wakati huo nilisafiri hadi Uganda kwa saa 24, lengo ni kwenda kufanya shoo ya bure tu. Kisa, nilitaka kufahamika! Imenisaidia kujitangaza, kuitangaza nchi yangu ndiyo maana leo kwa wengine inakuwa rahisi.
“Nakumbuka nilitembea kwa miguu usiku saa tisa kutoka Masaki hadi Morocco, lengo ni kupunguza nauli. Sikuwa nayo, nilishinda njaa mara kibao. Siwezi kufurahi nikiona msanii anatokea anaharibu tu, kama anaona hawezi kuwa msanii, aachane na kuimba, afanye kitu kingine.

“Hata ukisema watoto, enzi zetu tulikuwa tunapambana kuwaonyesha wazazi na jamii muziki ni sanaa na itakuwa ajira. Leo wazazi wako tayari kuwasapoti watoto wao, utaona ni mabadiliko makubwa sana, ndiyo maana nasisitiza umoja.”

Songi jipya:
“Kwa kweli niwashukuru sana Watanzania, Wimbo wa Touch Me niliowashikirisha Shawn Kingston na Ms Triniti umepokelewa vizuri na unapendwa. Una kiwango cha juu, achana tu na niliowashirikisha, lakini hata maprodyuza (Reily Urick na Zaire Koalo wa Studio za Network Showbizz), wako vizuri. Hawa jamaa wako California, Marekani na wana uzoefu.

“Watanzania wanielewe, lengo si kujulikana Marekani au kufanya vizuri huko. Nataka kufanya vizuri hapa nyumbani kwa kushirikiana na watu wa ‘levo’ za juu.

“Hata soka ina ‘levo’ zake, mfano ligi kuu, ligi ya mabingwa. Mchezaji anajipima kutokana na kucheza mashindano makubwa, ndiyo ninachofanya.

“Sasa niko katika hatua za mwisho, inafuatia video ambayo pia imetengenezwa kwa kiwango cha juu kabisa,” anasema AY.


SOURCE: CHAMPIONI 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic