February 13, 2015



Na Saleh Ally
MRISHO Ngassa huenda amekuwa kati ya wachezaji wachache sana wanaoweza kuweka hadharani kitu ambacho walifanya na wanaamini hakikuwa sawa kwa ajili ya maendeleo yao kimaisha.


Ngassa amesema anajutia uamuzi wake wa kukubali ushawishi wa kubaki Tanzania na kuacha kwenda kujiunga na El Merreikh ya Sudan, moja ya timu tajiri barani Afrika.

Naijua ishu ya El Merreikh, walikubali kutoa dola 50,000 (Sh Sh milioni 87.5) kwa Azam FC, halafu kiwango kama hicho kwa Simba ambayo Ngassa alikuwa anaichezea kwa mkopo wakati huo na dola 50,000 kwa Ngassa mwenyewe.

Ushawishi wa Yanga uliwashinda El Merreikh, Simba na Azam FC. Ngassa akakubali kubaki Tanzania kuichezea Yanga kwa dau la Sh milioni 60 kwa mkataba wa miaka miwili.

Inawezekana kabisa kilichosababisha Ngassa abaki nchini ni mambo mawili tu na hakuna ubishi. Kwanza mapenzi yake kwa Yanga, pili ni mazoezi, kukubali kuondoka nyumbani lazima uwe jasiri, si rahisi.
 
TEGETE (KULIA) AKIPAMBANA UWANJANI...
Wakati anaingia mkataba wa miaka miwili na Yanga, usisahau alikuwa na kesi na Simba iliyokuwa inamdai Sh milioni 30. Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) likaendesha kesi, ikafikia Sh milioni 45 baada ya kupigwa penalti ya Sh milioni 15.

Wakati Yanga inamsajili, ilishamlipa fedha yake Sh milioni 30 ya mwaka wa kwanza. Maana yake likaingia suala la deni na ndiyo chanzo cha kuzaliwa kwa ule mkopo wa Benki ya CRDB, hilo tuachane nalo.

Ishu ninayotaka kuizungumzia ni uamuzi wa Ngassa kuamua kubaki nyumbani wakati akijua kwenda El Merreikh kulikuwa na faida kubwa zaidi kwa maana ya maslahi, pia kuweza kujitangaza zaidi kwa kuwa timu ile ni kubwa, ina mafanikio makubwa zaidi na tajiri zaidi ya Yanga, wote tunalijua hilo.

Akabaki nyumbani, Ngassa hakuweza hata kuinua mguu. Nimesema mapenzi na mazoea, ndiyo maana leo nimemuita muungwana kuwa mkweli kwa alichokosea, huenda litakuwa funzo kwa wengi sana.

Unakumbuka wachezaji wangapi wao waliinua kabisa miguu yao, wakapata timu barani Ulaya, halafu mapenzi yakawarudisha nyumbani na mwisho wake wao ndiyo wakapoteza.
 
LUNYAMILA.
Mfano wa zamani kidogo ni ule wa Edibily Lunyamila aliyekuwa Ujerumani. Viongozi wa Yanga wakafanya kila juhudi kumshawishi arejee nyumbani ili kuisaidia Yanga kuimaliza Simba na ahadi kibao, baada ya kufanikiwa walichotaka wakamsahau.

Haruna Moshi ‘Boban’ alipata nafasi katika timu ya Gefle IF iliyokuwa Ligi Daraja la Kwanza Sweden. Wakati anafanya vizuri, kuna kiongozi mmoja wa Simba akawa anafanya kila juhudi kuhakikisha anarejea nchini.

Kiongozi huyo alimsisitizia Boban kuwa maslahi ya nyumbani yangekuwa bora. Ikaelezwa alimshawishi hadi kuanza vituko, ilimradi tu arudi nchini.

Jerry Tegete pia alipata timu ya daraja la kwanza nchini Sweden. Akapewa mshahara wa dola 2,500 (Sh milioni 4.4) na nyumba nzuri ya kuishi. Lengo walitaka wamuone, kipindi hicho Ligi Kuu Bara ilikuwa imebakiza mechi tatu, Simba walishakuwa mabingwa.

Mechi ya mwisho ilikuwa kati ya Simba dhidi ya Yanga. Tegete akaondoka Sweden baada ya kushawishiwa na viongozi, akarudi kuichezea Yanga iliyofungwa mabao 4-3, Hilary Echesa akihitimisha ushindi wa Simba.

Tegete alikubali kuacha bahati ya kuonekana zaidi, kuwashawishi Waswidi wamlipe mshahara mzuri zaidi na kumpa mkataba akarudi nchini kuichezea mechi iliyokuwa sawa na ya kirafiki tu!

Wengi wamepita kwenye njia hiyo ya kushawishiwa na viongozi kwa kisingizio cha mapenzi. Kwa kuwa nao wanayaamini mapenzi, basi wanajikuta wanapoteza vitu vikubwa na kujuta baadaye kabisa.

Hakuna ubishi Boban aliwahi kusikia ishu ya Lunyamila, hali kadhalika Ngassa alisikia ishu ya Tegete. Vipi sasa hakuna kati yao hakuna aliyejifunza? Au inawezekana wahusika wamekuwa wakiihadithia kwa kuficha mambo kwa ajili ya kutetea upande wao ili waonekane hawakukosea!

Lengo si kumlaumu mtu, lakini kueleza namna ambavyo ukweli wa Ngassa unavyoweza kuwa funzo pia kwa kukumbuka mifano hiyo iliyopita ya kina Lunyamila, Boban na wengine basi wachezaji wajifunze kuliko kusubiri nao waharibu halafu wajute!

Mapenzi ni jambo jema, kuitumikia kampuni au kitu unachokipenda ni bora lakini mara nyingi mtu hutakiwa kutafakari ushawishi ili kuepuka kuingia kwenye majuto kama ambayo aliyoyaanika Ngassa leo.

Inawezekana wengi wameshindwa kwenda nje ya Tanzania kutokana na ushawishi huo wa viongozi ambao wanakuwa wanaangalia zaidi maslahi yao kwa wakati huo maana ndiyo wanakuwa viongozi.

Kwa kuwa viongozi wanakuwa wanaangalia maslahi yao. Basi wachezaji amkeni, wakati mwingine wekeni mapenzi kando na muangalie maslahi yenu ili kuepuka kukumbuka shuka kukiwa kumekucha.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic