February 9, 2015


NIANZE kwa kukiri kwamba wanachama na mashabiki wa Simba wana haki ya kumzomea kiongozi, kocha au mchezaji wanayekuwa hawakubaliani na utendaji wake.


Mashabiki wanachotaka ni kuona kikosi chao kinafanya vizuri. Kweli kuna matokeo ya mchezo wa soka ambayo hata hivyo mashabiki wachache wa soka wamekuwa wakikubaliana nayo.

Wako ambao wamekuwa wakikubaliana nayo lakini wako ambao wamekuwa wakishindwa kuvumilia kabisa kutokana na mateso makubwa kwa klabu yao.

Mashabiki hawataji hata kuona mchezaji anakosea, hii ni kawaida ndiyo maana ya kupeleka mambo kitaalamu na kishabiki. Hivyo uache kila upande ufanya kazi kivyake.

Pamoja na kukubali hayo, kuna jambo moja liliniumiza sana, nikataka kujua kwa undani kuhusiana na Kocha Msaidizi wa Simba, Selemani Matola ambaye aliamua kuuambia uongozi angependa kupumzika.

Wakati Matola anasema vile, uongozi ukamkubalia, lakini Kocha Mkuu, Goran Kopunovic akauomba uongozi wampe nafasi ya kuzungumza na Matola, kweli akapewa nafasi hiyo, mwisho wakakubaliana na kocha huyo msaidizi akakubali kubali.

Ajabu siku chache baadaye mashabiki wa Simba wakamzomea Matola pale Uwanja wa Taifa jijini Dar. Wengine nikawasikia wakihojiwa kwenye rekodi kuhusiana na kocha huyo.

Kilichonishangaza ni kusikia karibu kila aliyehojiwa anasema kwamba Matola anawahujumu. Alipoulizwa anawahujumu vipi? Jibu lilikuwa anampangia Kopunovic timu au anamshawishi wachezaji fulani wasicheze!

Majungu ya kijinga kabisa! Sikuamini kinachoelezwa, nilijaribu kufuatilia kwa karibu, mwisho nikagundua tatizo hili kuwa kuna kiongozi mmoja aliye ndani ya kamati ya utendaji haelewani na Matola.

Kiongozi huyo ambaye kwa uzoefu wangu wa kuripoti habari za michezo, naanza kumuona akiwa na Simba au akiisaidia ndani ya kipindi cha mwaka mmoja tu uliopita, si vibaya nikimuita mgeni.

Lakini anasifika kuwa na ukaribu na wanachama wengi kwenye matawi. Hivyo ukimuudhi au kupingana naye, basi anakupangia ‘mashambulizi’ ili uonekane mbaya mbele za watu. Mfano sasa usishangae kuona Saleh Ally anazomewa sana na mashabiki wa Simba (he..he..he).

Najiuliza kiongozi huyo mgeni, au mashabiki hao wa zamani na siku hizi, wanafikiri ni sawa kumzomea Matola kisa habari za uzushi zisizokuwa na uhakika?


Kama ni kweli, Kopunovic angesema. Kama kweli anampangia timu basi Simba imuondoea kocha mkuu maana hana msimamo. Lakini kama angekuwa si sahihi, Mserbia huyo asingekubali Matola aendelee kubaki naye.

Kama hayo yote si sawa, vipi Kopunovic aliuomba uongozi wa Simba umpe nafasi ya kuzungumza na Matola licha ya yeye kuomba aondoke?

Wanasimba wenye mapenzi na timu na klabu yao hawawezi kumlipa Matola kwa njia hiyo. Aliichezea Simba iliyojaa shida, wachezaji walikula kwa mama ntilie.

Aliendelea kubaki huku wengine wakikimbia hadi ilipoimarika na kuwa timu bora iliyobeba makombe kibao mwisho ikaweka rekodi ya kuing’oa Zamalek kwenye michuano mikubwa ya Afrika wakati huo ikiwa bingwa na timu bora Afrika.

Yule kiongozi mgeni, wewe shabiki mna chochote cha kujilinganisha naye? Je, mna uhakika kuhusiana na yanayozungumzwa au mmebebeshwa tu kama ilivyo bendera na sasa mnafuata upepo?

Unajua kwamba takribani wachezaji 12 wa Simba, ni vijana waliotoka katika kikosi cha vijana kilichosukwa na Matola hadi kutwaa Kombe la Banc ABC kukiwa na timu kongwe kama Mtibwa Sugar na Azam FC?

Leo wachezaji hao makinda ndiyo tegemeo la Simba tena wanafanya kazi nzuri hata kuliko wale wageni walionunuliwa mamilioni.

Vipi mnakubali kuvaa ngozi ya chui kwa lengo la kumfurahisha kiongozi mmoja tu na kusahau yote ya Matola ambaye ameifanyia Simba lukuki mkifananisha na huyo kiongozi mgeni?


Mkubali mkatae, Matola atabaki kuwa shujaa wa Simba milele na kiongozi huyo ataondoka. Hivyo kama uongozi umekubali aondoke, mpeni heshima yake aende kwa amani kwa kuwa ameifanyia Simba makubwa kuliko viongozi karibu wote wa Simba walio madarakani.

1 COMMENTS:

  1. Tatizo mnaandika makala bila kufanya utafiti. Kubali ama ukatae, Matola bado ni tatizo Simba. Katika kufuatilia kwangu mpira, na pia niliwahi kuwaambia watu mwanzoni tu Sele alipoteuliwa kufundisha timu ya wakubwa. Nikasema aidha Simba wampe ukocha mkuu ama timu haiwezi kuwa consistent na matokeo mazuri. Sele alifanya vizuri na timu ya vijana akiwa kocha mkuu na si msaidizi, hilo unalisahau. Fanya utafiti wako kwa kuwaangalia Matora japo hana muda mrefu kweye ualimu wa soka, Marehemu Mziray na Julio, utangundua hawajawahi kufanya vizuri na timu yoyote wakiwa makocha wasaidizi. Wanaopiga kelele leo wanajua walimtumia vipi kipindi cha Rage na ndio maana wanahisi sasa amewageuka

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic