March 19, 2015


Na Saleh Ally
MSHAMBULIAJI wa Simba, Emmanuel Okwi amekuwa gumzo baada ya kufunga mabao mawili ‘matamu’ katika mechi mbili za Ligi Kuu Bara.


Okwi amefunga mabao hayo katika mechi dhidi ya Yanga, Jumapili iliyopita. Akaonyesha hakubahatisha tena kwa kufunga bao linalofanana na hilo Simba ilipoivaa Mtibwa Sugar, Jumatano.

Aina ya mabao hayo ambayo amefunga kwa umbali wa kuanzia mita 25 lile la Mtibwa Sugar na zaidi ya mita 30 lile dhidi ya Yanga, umefanya yawe mabao gumzo zaidi katika kipindi hiki.
 
REUS...
Pamoja na kwamba hakufanikiwa kufunga bao katika mechi dhidi ya Mgambo Shooting wakati Simba ikilala kwa mabao 2-0 Mkwawani, Tanga, jana. Bado haizuii mabao aliyofunga dhidi ya Yanga na Mtibwa kuendelea kuwa bora.

Katika mahojiano maalum, Okwi amekiri kuwa amejifunza aina ya upigaji mipira kupitia kiungo mchezeshaji hatari kutoka klabu ya Borussia Dortmund ya Ujerumani, Marco Reus.

Huyu ndiye shujaa na mchezaji kipenzi zaidi kwa Okwi. Raia huyo wa Ujerumani ni kati ya wachezaji ambao wamekuwa wakiwaniwa na timu mbalimbali kama Real Madrid, Arsenal na nyingine kubwa kadhaa.

Reus anajulikana kwa uwezo mkubwa wa kuchezesha timu pia ufungaji wa mabao muhimu, jambo ambalo Okwi amekuwa akitaka kulifanya kwa  Simba.


Okwi tayari ana mabao saba katika Ligi Kuu Bara. Lakini anataka kufunga zaidi kama nafasi itapatikana.

SALEHJEMBE: Kipi hasa kinakuvutia kwa Reus?
Okwi: Ni mchezaji anayejiamini, hana hofu na anaijua kazi yake. Kwangu ndiye mchezaji bora zaidi kuliko wote wanaocheza soka duniani.

SALEHJEMBE: Kipi umechukua kutoka kwake?
Okwi: Kwanza siwezi kuchukua kila kitu, kama mchezaji pia nina mambo yangu. Lakini namna ya kumiliki mpira, pasi nzuri, kujiamini pia upigaji wa mashuti kama ambavyo uliona tulivyocheza na Yanga na baadaye Mtibwa.

SALEHJEMBE: Unajifunza kwa kuona tu, au kuna ziada?
Okwi: Kwanza naangalia kazi zake, Dortmund ikiwa inacheza. Lakini kwenye You tube, halafu nikiwa uwanjani nafanya kazi ya kupiga mipira. Nilikuwa nikikosea mingi, sasa naanza kupatia zaidi.

SALEHJEMBE: Unafikiri ulikosea mara nyingi hata katika mechi au mazoezini tu?
Okwi: Hata katika mechi, naamini hata nilionekana kama sijui ninafanya nini. lakini nilipania kufanikiwa na ilikuwa ni lazima nijaribu.

SALEHJEMBE: Unafikiri utaendelea kufunga zaidi mabao ya aina hiyo?
Okwi: Inawezekana au isiwe hivyo. Kikubwa ni kumuomba Mungu maana yeye ndiye kila kitu. Lengo kubwa kwangu ni kufunga, nikishindwa basi nisaidie timu hata kutoa pasi kwa wenzangu wafunge. Akifunga yoyote ni muhimu kwa timu.

SALEHJEMBE:  Unafikiri Simba ina nafasi ya kutwaa ubingwa wa Ligi kuu Bara?
Okwi: Nafasi ipo, kama tutaendelea kushinda, itakuwepo. Kikosi chetu ni kizuri na matatizo madogo yanaanza kurekebishika. Imani yangu tutafanya vizuri, lakini bado tunamuachia Mungu.

SALEHJEMBE:  Vipi kuhusu ufungaji bora?

Okwi: Ninaweza kuwa mfungaji bora au hapana. Lakini zaidi naangalia Simba itapata nini baada ya ligi. Ndiyo maana nilikuambia kufunga mimi sawa, nikitoa pasi sawa. Lengo hasa ni kuisaidia timu na ikishinda mechi nyingi zaidi bila ya kujali nani kafunga, ndiyo faida kubwa zaidi.

SALEHJEMBE: Karibu sana Championi Okwi.

Okwi: Nashukuru sana.



1 COMMENTS:

  1. Na kujipoza baada ya machungu kunaruhusiwa .

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic