March 7, 2015


Na Saleh Ally
MECHI ya watani wa jadi, Yanga dhidi ya Simba ambao ni ‘dugu’ moja, kila inapopigwa inakuwa na jambo lake ambalo linabaki kuwa gumzo miaka nenda rudi.


Kwa kifupi, wanapokutana watani Simba na Yanga, basi lazima kuwe na ‘surprise’ ya siku kwa aina yoyote ile.

Mechi ya kesho Jumapili inasubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka huku kukiwa na rekodi kibao nyuma kabla ya watani hao kukutana leo.

Tuanzie msimu wa wa 2011/12 hadi mechi hiyo ya kesho inakuwa ni mechi ya nane kwa kuwa Yanga na Simba zimeshakutana mara saba katika Ligi Kuu Bara.

Kila msimu, Yanga na Simba zinakutana mara mbili katika mechi za Ligi Kuu Bara. Misimu mitatu maana yake mechi sita na msimu huu zimekutana mara moja na kutoka sare ya bila kufungana.


Katika mechi saba ambazo zimecheza katika misimu minne, inaonekana wachezaji wa kigeni ndiyo wenye bahati zaidi ya kutikisa nyavu katika mechi za watani wa jadi hata kuliko wenyeji.

Katika mechi hizo saba, wageni ndiyo wenye mabao mengi zaidi kuliko wenyeji na waliotikisa nyavu hizo wanatokea katika nchi za Zambia, Uganda, Burundi na DR Congo.

Ukianzia msimu wa 2011-12, jumla ya mabao 18 yamefungwa na wageni wamefunga 11 huku wenyeji au wazawa wakiwa na 6, hii ni sehemu ya kuonyesha kweli wana bahati zaidi na mechi ya watani.


Msimu wa 2011-12, mechi mbili zilikuwa hivi. Ile ya kwanza Yanga ilishinda bao 1-0, mfungaji akiwa Davies Mwape, raia wa Zambia. Mechi ya pili, Yanga ikakutana na kipigo cha kihistoria cha mabao 5-0.

Mabao matano ya Simba siku hiyo, manne yalifungwa na wageni ambao ni Emmanuel Okwi (mawili), Patrick Mafisango (DR Congo, lakini alichukua uraia wa Rwanda), Felix Sunzu (Zambia) na mwenyeji pekee aliyefunga siku hiyo ni kipa Juma Kaseja.

Msimu wa 2012-13, mechi ya kwanza ilikuwa sare ya bao 1-1, wenyeji wakitamba kwa Amri Kiemba kuanza kuifungia Simba na Simon Msuva akasawazisha. Mechi ya pili, Simba ikalala 2-0, Mrundi Didier Kavumbagu na Mganda Hamisi Kiiza wakifanya yao.

Ukafuatia msimu wa 2013-14, mechi ya kwanza, Yanga ikatangulia hadi mapumziko ikiwa na mabao matatu ya Kiiza (mawili) na Mrisho Ngassa. Simba ikasawazisha yote kupitia Gilbert Kaze (Burundi), Joseph Owino (Uganda) na Mtanzania Betram Mwombeki. 


Ziliporudiana sare nyingine, safari hii ikiwa ni bao 1-1 akianza kufunga Haruna Chanongo na Simon Msuva akasawazisha ‘jioni’.
 
Kwa misimu hiyo mitatu, zikawa zimekamilika mechi sita na msimu wa nne ni huu wa 2014-15 na mechi ya kwanza haikuwa na mabao yaani sare ya 0-0.

Mechi ya pili ni ngumu, kila upande unachoangalia ni kupata pointi tatu. Suala la wageni kufunga au wenyeji halitiliwi mkazo kwa timu hizo, muhimu ni ushindi.

Lakini halibadilishi kuwa kweli wageni wana bahati zaidi kwa kuwa katika mechi saba tu wamefunga mabao 11 huku wenyeji wakifunga 7 tu.

Katika mechi hiyo pia sare zimekuwa nyingi zaidi, kwani katika mara saba walizokutana, Yanga imeshinda mara mbili, imepoteza moja na sare nne.

Wakati Simba imepoteza mara mbili, sare nne na imeshinda mara moja, mara ya mwisho kuifunga Yanga katika Ligi Kuu Bara ikiwa ni ile mechi ya 5-0, mechi ilipopigwa  Mei 6, 2012.

Kesho kwa upande wa Simba wana Waganda tu ambao ni Okwi, Simon na Danny Sserunkuma, Juuko Murshid na Joseph Owino wakati Yanga wamechanganya uraia wakiwa na Mbuyu Twite na Haruna Niyonzima (Rwanda), Kpah Sherman (Liberia), Amissi Tambwe (Burundi) wakati Andrey Coutinho raia wa Brazil atakuwa jukwaani kutokana na majeraha.


Washambuliaji kama Elius Maguri, Ibrahim Ajib ‘Kadabra’, Ramadhani Singano ‘Messi’ watakuwa na kazi ya kuonyesha hata wenyeji wanaweza kufunga mabao mengi zaidi.

Kwa upande wa Yanga pia, Simon Msuva, Mrisho Ngassa, Hussein Javu na wengine, pia wana nafasi hiyo ya kubadilisha wageni kutawala zaidi.



MECHI:

2011/2012
Oktoba 29, 2011

Yanga       1- 0     Simba
Mwape 72

Mei 6, 2012
Simba       5-0       Yanga    
Okwi    1&62, 
Sunzu   53, 
Kaseja   66
Mafisango 71


2012/13
Oktoba 3, 2012
Yanga          1-1          Simba               Taifa
Bahanuzi 65             Kiemba   4
  
Mei 18, 2013
Simba          0-2                  Yanga                   Taifa

                                           Kavumbagu, Kiiza

2013-14

Oktoba 20, 2013

Simba                        3-3              Yanga                        Taifa
Mwombeki 53                           Ngassa 15, Kiiza 35&45
Owino 60, Kaze84                                  

                      

Aprili 19, 2014

Yanga                         1-1              Simba                        Taifa
Simon Msuva 86                        Haruna Chanongo 75          


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic