April 3, 2015


MIEZI michache ijayo, mimi na wewe msomaji tutakuwa tumesimama kwenye foleni kwa ajili ya kupiga kura ili tuchague viongozi wetu watakaotuongoza kwa miaka mingine mitano ijayo.


Najua, tunapishana au kufanana kuhusiana na hisia au kuamini kwamba ni kiongozi yupi sahihi na anapaswa kutuongoza. Acha tusubiri hiyo foleni kwa kuwa kila kitu ni majaaliwa.
Lakini wakati huu wa uchaguzi mkuu, kuna kila aina ya mbinu zinazotumiwa na wanasiasa kwa ajili ya kuhakikisha wanatimiza malengo yao.

Wanachoangalia ni kipi ambacho kinaweza kuwapatia nafuu ya kuwapata watu ambao watawapigia kura za ushindi washinde ubunge au vyeo vingine vitakavyokuwa vinagombewa.

Wanaopiga kura ni watu, ili kuwapata lazima uwavute na wanachokipenda hata kama watakuwa hawakupendi wewe. Michezo ni kati ya nguvu kubwa katika mioyo ya Watanzania.

Wanasiasa wanalijua hilo na wapo wengi sana wamekuwa wakiitumia michezo kama sehemu ya kurahisisha mambo yao hasa inapofikia wanataka kushinda.

Wapo ambao wamekuwa wakionyesha mapenzi au kutaka kuisaidia michezo tokea awali. Yaani hata kabla ya uchaguzi na baada ya uchaguzi. Hapa kuna makundi mawili ya wanasiasa.

Wale ambao huisaidia michezo kwa lengo la kupata kura washinde, halafu hata baada ya hapo wanaendelea kutoa msaada. Kundi la pili ni lile ambalo linasaidia kutaka kupata ushindi, likifanikiwa, linaachana kabisa na michezo kwa kuwa limepata linachotaka.

Kundi la pili ndiyo kubwa zaidi, hata sasa inawezekana litakuwa linajipanga ili liwatumie wanamichezo na michezo kwa ajili ya kupata kura na kuendelea mbele huku likiwa halina habari na michezo kabisa.

Michezo ina nguvu, michezo ni ajira, michezo ni afya na msaada mkubwa kwa taifa letu. Wanasiasa walaghai wamekuwa wakiitumia na kuiacha kama mwanaume anapoamua kutupa soksi zake zilizochakaa kwa kuwa na matundu kibao.

Jiulize anayetaka kukamua maziwa ya ng’ombe bila ya kufikiria kumpa chakula kizuri ili kuhakikisha anaweza kuhimili vishindo vya kukamuliwa, anataka nini?
Wanasiasa wengi ni watu wanaojali wanachotaka, wanaojali nafsi zao, wanaoangalia faida ya maisha yao na si vitu vingine vinavyowasaidia au vilivyowawezesha kupata ushindi. Wanasiasa wengi ni wabinafsi.

Kuna mifano mingi ambayo tumekuwa tukiiona, mfano timu au bondia fulani akiwa anajiandaa katika michuano ya kimataifa au mechi kali dhidi ya bondia kutoka Marekani au China, kamwe hauwezi kuona akiwa mazoezini na mwanasiasa yeyote.

Wakati huo hauwezi kuwa bora kwa wanasiasa kuona watafaidika. Wanajua wakiingia watagharimika, au wakiingia bondia akapoteza itaonekana wao si watu imara wanaoweza kusababisha ushindi.

Kama atashinda au timu itashinda, basi unakuwa ni wakati bora kabisa kwa wanasiasa kujisogeza, kulazimisha kuonekana kwenye picha wakiwa naye na ikiwezekana hata kutoa zawadi kadhaa kwa madai wanapongeza.
Wanasiasa siku zote wanapenda kushiriki katika vilivyoiva, kamwe si katika kulima au upishi. Ndiyo wamekuwa wakiifanya hivyo michezo ambayo ‘inaishi’ ikiwa na viwanja duni, vifaa vya hovyo, vijana wasio na viwanja vya kuchezea! Lakini wanataka wawatumie wakati wanapoona wanahitaji kushinda.

Wanasiasa wanaamini wao wana akili nyingi kuliko viumbe wote duniani. Wanaamini hivyo kwa kuwa tu wamekuwa wakitumia uongo uleule miaka nenda rudi na bado unawasaidia kutimiza ndoto ya wanachokitaka.
Rasmi natangaza, kamwe sitakubali kuona wanasiasa waongo, wasio na mawazo ya kuiendeleza michezo halafu waitumie kwa ajili ya faida za matumbo yao wakati hawakufanya lolote kuisaidia kabla.

Najua nitawaudhi wanasiasa wengi, lakini nitasema ukweli. Ninawaamsha wanamichezo kwamba hawana sababu ya kutumika kwa misaada isiyo na tija ili wawasaidie hata wanasiasa wasio na uwezo kupita ndani yao na kupata nafasi ya kuingoza nchi yetu.

Hakuna ubishi unajua, wanasiasa wangapi walishiriki kusaidia michezo na wakati gani. Wale ambao hawakuijali, hakuna haja ya kushirikiana nao, acheni waende njia zao ambazo waliamini ni sahihi. Watatumaliza, amkeni, msikubali.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic