May 4, 2015


NILIKUWA uwanjani jijini Alexandria nchini Misri wakati Yanga walikuwa wakipambana vilivyo na Al Ahly katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.


Yanga waling’olewa kwa mikwaju ya penalti baada ya kufungwa bao 1-0. Mechi ikaongezewa muda na baadaye penalti ambazo ziliwatoa Yanga.

Yanga ndiyo walikuwa na nafasi ya kushinda mara mbili, wakianzia kwa Mbuyu Twite, akakosa na baadaye ikawa zamu ya Said Bahanuzi, naye akakosa, mwisho Waarabu hawakufanya makosa.

Nilikuwa nimeketi pembeni ya runinga nikishuhudia mechi kati ya Yanga dhidi ya Etoile du Sahel ya Tunisia.
Yanga ilikuwa ugenini kupambana katika Uwanja wa Olimpiki mjini Sousse, Tunisia. Ikafungwa bao 1-0 na kung’olewa katika michuano hiyo ikiwa ni baada ya sare ya bao 1-1 jijini Dar es Salaam.

Sitaki kukubaliana na hadithi, eti Yanga iliisumbua Al Ahly kwa kuwa ilikuwa imechoka. Tumeona ilikwenda Kombe la Shirikisho, ikaingia hadi fainali.

Bado hauwezi ukasema Yanga imeibahatisha Etoile na imeikosea kidogo tu kwani ilikuwa ina uwezo wa kuing’oa katika michuano yao pamoja na kujiandaa kwa kiwango cha juu ili kuhakikisha wanashinda mechi hiyo muhimu ya kurudiana dhidi ya Yanga.

Inawezekana kwa kipindi hiki, Yanga inaweza kuwa dira ya mwamko wa soka la Afrika Mashariki kutokana na mwenendo wake ulivyo.

Mara mbili, Yanga inatolewa na timu za Afrika Kaskazini ambazo zinajulikana kuwa zina uwezo mkubwa kutokana na kuwekeza kwake katika michezo katika kiwango cha juu.

Unajua Waarabu walivyowekeza katika soka, tena kitambo. Tunajua hali hiyo namna ambavyo imekuwa ikisaidia ubora wa timu zao kuwa juu.

Kupambana kwao ni kwa hali ya juu, wana mbinu za kila aina. Pamoja na kwamba tumekuwa tukilaumu kwamba wana fitina, lakini uwezo wao uko juu.

Wana timu nzuri za watoto, vijana. Wana viwanja bora vya kuchezea. Unaweza kusema mambo yao ni kama Ulaya kwa asilimia kubwa ndiyo maana timu zetu zikisafiri kwenda Afrika Kaskazini, mara nyingi ni kipigo hadi cha mabao matano au zaidi.

Lakini kama ulibahatika kuangalia mechi hizi mbili za Yanga, ile ya Misri msimu uliopita na hii ya juzi dhidi ya Etoile utagundua kuna tofauti kubwa.

Yanga ilicheza soka safi na kuwapa Waarabu wakati mgumu. Hakuna aliyehofia kama ilivyokuwa awali na huenda licha ya kuwa nyumbani, Etoile walikuwa na wakati mgumu sana.

Yanga ilishambulia mfululizo na kuwapa wakati mgumu. Wakati mwingine walilazimika kucheza kwa umakini mkubwa huku wakijilinda kuhofia wasipoteze dhidi ya Yanga.

Kweli Yanga imetolewa, lakini kiwango dhidi ya Al Ahly na Etoile ndani ya misimu miwili jambo la kulitupia macho na kulifanyia kazi. Kama kiwango hicho kitadumishwa, basi msimu ujao inaweza kufika mbali.

Kama kikosi kitafanyiwa marekebisho husika, uongozi wa Yanga utaendelea kuwa imara. Ule uisoyumba, basi lahisi mambo kwenda vizuri hapo baadaye.
Kuwaangusha Waarabu haiwezi kuwa hadithi ya siku moja. Lazima kuwe na mabadiliko taratibu. Maana yake Yanga imeingia katika anga ambazo inaweza kuhimili mikiki ya Waraabu. Imekuwa ikikosea kidogo tu ili kuwalipua kama itakutana nao.

Wao wamejipanga siku nyingi ukilinganisha na nchi za ukanda wa Afrika Mashariki. Mabadiliko kama hayo, yatasaidia timu zetu kuzidi kuimarika.

Kikubwa Yanga wahakikishe hakuna mvurugiko katika kikosi chao. Pia kazi ya kusaka vijana, kuwa na utaratibu mzuri nayo iingie kwenye programu.

Kuna kila sababu ya kuamini kuna mabadiliko yanakuja kama timu kama Yanga leo inakwenda kucheza Uarabuni haina tena hofu kufungwa bao tano au saba. Hiki ndiyo kipindi muhimu cha kuendeleza mapinduzi ya soka hapa nyumbani. Mwendo wa Yanga ni njia sahihi.


1 COMMENTS:

  1. Kweli kabisa mwandishi,tukiacha ushabiki hawa watani zetu wana soka la hali ya juu pengine tunaweza kusema ni tishio kwa club za africa mashariki,sioni kama kuna tofauti sana na TP mazembe,nina uhakika mwakani watafanya vizuri sana kama hawatatibuana.Hongera sana YANGA.

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic