Na Saleh Ally
MSHAMBULIAJI mpya wa Yanga, Donald Ngoma
amefanikiwa kufunga mabao matatu katika mechi zake tatu za kwanza za Ligi Kuu
Tanzania Bara.
Ngoma raia wa Zimbabwe alianza kuifungia
Yanga bao katika mechi ya ufunguzi wa ligi wakati iliposhinda kwa mabao 2-0
dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Bao hilo lilionekana ni kama kuondoa ‘nuksi’
kwa kuwa katika mechi za kirafiki, mambo yalionekana kutokuwa mazuri kwa Mzimbabwe
huyo, hadi baadhi ya wadau wakaamini Yanga ilikuwa imeingizwa mkenge.
Mechi iliyofuata, Yanga ilishinda kwa mabao
3-0 dhidi ya timu ngumu ya Prisons. Ngoma alikuwa ‘ubaoni’ tena baada ya
kufunga bao moja, safari hii akafikisha mabao mawili.
Swali likawa kweli ataweza kufikisha mabao
matatu katika mechi tatu kwa kuwa ilikuwa inafuatia JKT Ruvu iliyokuwa imetoka
kujeruhiwa. Ngoma akatoa jibu kwa kufunga bao safi kabisa na kuweka hesabu ya
mabao matatu katika mechi tatu sawa na Amissi Tambwe.
Ngoma sasa ana mabao matatu sawa na
mshambuliaji aliyekuwa mfungaji bora msimu mmoja kabla ya msimu uliopita.
Lakini akashika nafasi ya pili kwa kufunga mabao 14 msimu uliopita.
Ngoma kwake ndiyo msimu wa kwanza akicheza
Ligi Kuu Bara na amefanikiwa kufunga mabao matatu katika mechi tatu. Jambo zuri
kwa Yanga au kamati yake iliyohusika na usajili inaonekana ililenga au kusajili
mchezaji sahihi kwa kuwa kazi yake ni kufunga na anaonyesha kweli anaweza.
Si sahihi kuanza kumtwisha Ngoma misifa kwa
wingi kwa sasa, kwamba hakuna kama yeye au hashikiki hadi hapo atakapofanya
mambo mawili.
Nianze na yale aliyoyafanya kabla ya kwenda
kwenye namna gani tunaweza kuthibitisha. Ngoma amefunga mabao matatu lakini mawili
ni ya aina yake na yanayoweza kufungwa na mshambuliaji mwenye uwezo mkubwa,
hilo halina ubishi.
Bao lake la kwanza, mechi dhidi ya Coastal
Union, Ngoma alifunga bao katikati ya mabeki wanne wa Wagosi wa Kaya,
akionyesha namna gani alivyotulia. Lakini alimsubiri kipa kabla ya kupiga
upande mmoja aliotokea kipa na asingeweza kugeuka.
Bao lake linaloweza pia kuingia kwenye moja
ya mabao bora ya Ligi Kuu Bara, ni lile la tatu alilofunga dhidi ya JKT. Kwani
alianzia na mpira mbali akitoa pasi na kuomba, akatoa na kuikuta tena kabla ya
kufunga kwa mchomo safi wa chini ulioonekana ana malengo na huenda ni vigumu
kuona wachezaji wengi hapa nyumbani wakifunga hivyo.
Uthibitisho kwamba kweli Ngoma ni bora na
anaweza kuwa bora zaidi ni kama atafunga au kusababisha bao katika mechi dhidi
ya Simba wiki ijayo. Mechi yenye presha kubwa, mechi ambayo mchezaji bora
anaweza kuonekana hana lolote.
Kuhimili presha ni sehemu ya kipimo cha
kuonyesha ubora wa mchezaji fulani ana uwezo, mzoefu ana msaada na pia ana
uwezo. Pili, tusubiri atakapokwenda kucheza mikoani ambako viwanja vingine
mchezaji analazimika kuutuliza mpira mara sita, saba.
Kama Ngoma ataifunga Simba, akaondoka na
Yanga kwenda mikoani akaifungia pia, basi kuna kila sababu kuwa kweli ni
mchezaji ambaye Watanzania wangependa kuona anasajiliwa na timu za hapa nyumbani.
Lengo la usajili ni kuona kunakuwa na
wachezaji wanaoashiria ushindani, upinzani ambao utajenga na kufanya mchezo wa
soka nchini kusonga mbele. Acha tuendelee kuona ngoma ya Ngoma inavyokuwa.








0 COMMENTS:
Post a Comment