Na Saleh Ally
GUMZO
kubwa katika soka la England sasa ni kuhusiana na Wayne Rooney kufunga bao la
50 akiwa na kikosi chake cha timu ya taifa.
Rooney
amefunga bao la 50 wakati England ilipoivaa Switzerland maarufu kama Uswisi
katika mechi ya kuwania kucheza michuano ya Euro itakayofanyika mwakani.
Kinachozungumzwa
sana ni kwamba Rooney ameweza kuvunja rekodi ya gwiji wa England, Sir Bobby
Charlton. Inaonekana alichokifanya ni kikubwa na hilo ndiyo gumzo.
Suala
la rekodi limekuwa ni tatizo kubwa sana, angalau kidogo baadhi ya vyombo vya
habari likiwemo gazeti hili la Championi vimekuwa vikijitahidi kuhifadhi rekodi
kama hizo.
| MSUVA KAZINI...Kwa mpira wa kisayansi, rekodi ni sehemu ya chachu katika kuleta mafanikio au mwamko wa kimashindano kati ya wachezaji na wachezaji na timu na timu. |
Rekodi
ni chachu kwa kuwa ni kipimo sahihi ambacho hakina longolongo na inakuwa si
rahisi kubishana nazo, labda tu kama zitakuwa na walakini.
Rekodi
iliyokamilika kamwe hauwezi kushindana nayo, badala yake ni kupambana kuipita
au kutengeneza yako na lazima iwe ni kwa vitendo.
Wachezaji
wengi wa Ulaya na kwingineko ambako soka limepiga hatua wamekuwa wakipata
msukumo mkubwa wa utendaji kwenda kwenye maendeleo kutokana ama kutaka kuzipita
au kuzivunja rekodi fulani ambazo wanaziona ndiyo zenye sifa au kipimo cha
mafanikio.
Hakuna
ubishi, Rooney alipambana kimyakimya na rekodi ya Sir Charlton kuhakikisha
anaifikia na baada ya hapo kuipita au kuivunja, jambo ambalo tayari limetimia.
Kinachotakiwa
kwa sasa ni Rooney kupambana na kuweka rekodi yake. Maana ndiyo ana miaka 29,
anatakiwa kufunga zaidi na ‘kuishindilia’ rekodi ili wakati wengine
wanaikimbiza kuifikia na kuivunja, wajue kweli ni rekodi ya ‘mtu wa kazi’.
Hapa
nyumbani vipi? Najua hili si swali la kwanza kuuliza kuhusiana na hili kwamba,
je, wachezaji, klabu au shirikisho, mnahifadhi rekodi zenu?
Rekodi
za mambo lundo, mfano kwa wachezaji makinda kama Simon Msuva wa Yanga na Said
Ndemla wa Simba ambao haraka kwa kuwaangalia ni mashujaa wajao wa taifa letu,
kweli wana rekodi ya mechi 15 za klabu zilizopita.
Hao
wana rekodi ya timu ya taifa, mfano ukikutana na Ndemla au Msuva na kumuuliza
amecheza dakika ngapi katika kikosi cha Taifa Stars hadi sasa? Kweli atajibu!
Huenda
kwa uelewa na hata soka ya hapa nyumbani miaka sita au saba iliyopita
ilionekana ni kama sehemu ya kujiburudisha na hakuna haja ya kufuatilia mambo
mengi.
Huu
ndiyo wakati muafaka wa wachezaji kama akina Msuva, Ndemla na wengine wa umri
wao kuanza kujua kwamba wanatakiwa kwenda na wakati na hakuna ujanja zaidi ya
kubadilika. Rekodi ni muhimu sana zaidi ya makaratasi tu kwa ajili ya kuweka.
Rekodi
zinakuza, rekodi zinaamsha na rekodi zinasaidia kuongeza ushindani. Hivyo kama
mchezaji ataona hakuna kumbukumbu za kutosha kutoka kwenye vyombo vya habari,
mashirikisho na klabuni kwake, mwenyewe anaweza kuhifadhi.
Mfano
Msuva ajue kaichezea Yanga mechi ngapi msimu uliopita, za ligi, mashindano na
Ligi ya Mabingwa, michuano yoyote ya Caf. Pia anapaswa kujua mechi za kirafiki
za nyumbani na zile za kimataifa.
Kafunga
mabao mangapi kwenye ligi, mangapi kwenye mechi za kirafiki na kadhalika.
Hapa
ninawatumia Msuva na Ndemla kama mfano, lakini hili ni jukumu la wachezaji wote
wa kizazi hiki waondoke na kujikomboa kwenye hali ngumu na kuishi maisha ya
mwaka 47 wakiwa katika kipindi kingine kabisa.
Miaka
sita au saba iliyopita, Juma Kaseja alikuwa akihifadhi rekodi zake mwenyewe.
Amecheza mechi ngapi, timu zipi na hata matokeo yalikuwaje. Vipi leo umri wa
akina Msuva na Ndemla washindwe!








0 COMMENTS:
Post a Comment