September 11, 2015


Na Saleh Ally
GUMZO kubwa katika soka la England sasa ni kuhusiana na Wayne Rooney kufunga bao la 50 akiwa na kikosi chake cha timu ya taifa.


Rooney amefunga bao la 50 wakati England ilipoivaa Switzerland maarufu kama Uswisi katika mechi ya kuwania kucheza michuano ya Euro itakayofanyika mwakani.

Kinachozungumzwa sana ni kwamba Rooney ameweza kuvunja rekodi ya gwiji wa England, Sir Bobby Charlton. Inaonekana alichokifanya ni kikubwa na hilo ndiyo gumzo.

Suala la rekodi limekuwa ni tatizo kubwa sana, angalau kidogo baadhi ya vyombo vya habari likiwemo gazeti hili la Championi vimekuwa vikijitahidi kuhifadhi rekodi kama hizo.
 
MSUVA KAZINI...Kwa mpira wa kisayansi, rekodi ni sehemu ya chachu katika kuleta mafanikio au mwamko wa kimashindano kati ya wachezaji na wachezaji na timu na timu.

Rekodi ni chachu kwa kuwa ni kipimo sahihi ambacho hakina longolongo na inakuwa si rahisi kubishana nazo, labda tu kama zitakuwa na walakini.

Rekodi iliyokamilika kamwe hauwezi kushindana nayo, badala yake ni kupambana kuipita au kutengeneza yako na lazima iwe ni kwa vitendo.
 
NDEMLA

Wachezaji wengi wa Ulaya na kwingineko ambako soka limepiga hatua wamekuwa wakipata msukumo mkubwa wa utendaji kwenda kwenye maendeleo kutokana ama kutaka kuzipita au kuzivunja rekodi fulani ambazo wanaziona ndiyo zenye sifa au kipimo cha mafanikio.

Hakuna ubishi, Rooney alipambana kimyakimya na rekodi ya Sir Charlton kuhakikisha anaifikia na baada ya hapo kuipita au kuivunja, jambo ambalo tayari limetimia.

Kinachotakiwa kwa sasa ni Rooney kupambana na kuweka rekodi yake. Maana ndiyo ana miaka 29, anatakiwa kufunga zaidi na ‘kuishindilia’ rekodi ili wakati wengine wanaikimbiza kuifikia na kuivunja, wajue kweli ni rekodi ya ‘mtu wa kazi’.

Hapa nyumbani vipi? Najua hili si swali la kwanza kuuliza kuhusiana na hili kwamba, je, wachezaji, klabu au shirikisho, mnahifadhi rekodi zenu?

Rekodi za mambo lundo, mfano kwa wachezaji makinda kama Simon Msuva wa Yanga na Said Ndemla wa Simba ambao haraka kwa kuwaangalia ni mashujaa wajao wa taifa letu, kweli wana rekodi ya mechi 15 za klabu zilizopita.

Hao wana rekodi ya timu ya taifa, mfano ukikutana na Ndemla au Msuva na kumuuliza amecheza dakika ngapi katika kikosi cha Taifa Stars hadi sasa? Kweli atajibu!

Huenda kwa uelewa na hata soka ya hapa nyumbani miaka sita au saba iliyopita ilionekana ni kama sehemu ya kujiburudisha na hakuna haja ya kufuatilia mambo mengi.

Huu ndiyo wakati muafaka wa wachezaji kama akina Msuva, Ndemla na wengine wa umri wao kuanza kujua kwamba wanatakiwa kwenda na wakati na hakuna ujanja zaidi ya kubadilika. Rekodi ni muhimu sana zaidi ya makaratasi tu kwa ajili ya kuweka.

Rekodi zinakuza, rekodi zinaamsha na rekodi zinasaidia kuongeza ushindani. Hivyo kama mchezaji ataona hakuna kumbukumbu za kutosha kutoka kwenye vyombo vya habari, mashirikisho na klabuni kwake, mwenyewe anaweza kuhifadhi.

Mfano Msuva ajue kaichezea Yanga mechi ngapi msimu uliopita, za ligi, mashindano na Ligi ya Mabingwa, michuano yoyote ya Caf. Pia anapaswa kujua mechi za kirafiki za nyumbani na zile za kimataifa.

Kafunga mabao mangapi kwenye ligi, mangapi kwenye mechi za kirafiki na kadhalika.

Hapa ninawatumia Msuva na Ndemla kama mfano, lakini hili ni jukumu la wachezaji wote wa kizazi hiki waondoke na kujikomboa kwenye hali ngumu na kuishi maisha ya mwaka 47 wakiwa katika kipindi kingine kabisa.

Miaka sita au saba iliyopita, Juma Kaseja alikuwa akihifadhi rekodi zake mwenyewe. Amecheza mechi ngapi, timu zipi na hata matokeo yalikuwaje. Vipi leo umri wa akina Msuva na Ndemla washindwe!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic