![]() |
| MOSHA AKIWA OFISINI KWAKE SINZA JIJINI DAR ES SALAAM |
Na Saleh Ally
WATANI wa jadi Yanga na Simba wanakutana
katika mechi yao ya Ligi Kuu Bara, kesho na huenda ukawa ndiyo mwisho wa
majigambo kwa kuwa jibu la nani mbabe litapatikana.
Mechi ya kwanza kwenye Uwanja wa Taifa,
Dar es Salaam, Simba ililala kwa mabao 2-0. Hapohapo zinakutana na aliyewahi
kuwa mmoja wa viongozi katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Davis Mosha
ni kati ya wanaofuatilia.
Mosha ambaye ni kati ya vijana matajiri
wa Kitanzania, ana imani kubwa kwamba mechi hiyo itakuwa ngumu na mshindi
atapatikana baada ya dakika 90.
Pamoja na hivyo, Mosha anaamini kuna
mambo mengi yanayotakiwa kufanywa ili Yanga iweze kushinda mechi ya kesho.
Katika mahojiano maalum na gazeti hili,
Mosha anaelezea mambo kadhaa huku akisisitiza ndiyo msingi sahihi.
SALEHJEMBE:
Kipi cha kwanza kinatakiwa kufanyika?
Mosha:
Umoja na ukaribu wa makundi yote. Mfano wachezaji, mashabiki na uongozi kuwa
pamoja kwa ajili ya timu na kusiwe na hisia za kutafutwa mchawi.
SALEHJEMBE:Mchawi
kivipi Mosha?
Mosha:
Unajua, kabla ya mechi hiyo ya watani kuna mambo mengi, suala la kutafuta
mchawi kabla au baada ya mechi halina faida.
SALEHJEMBE:Unafikiri
viongozi wawe karibu vipi, watoe ahadi au motisha ya kutosha?
Mosha:
Kutoa fedha ni sehemu tu, lakini kuwapa wachezaji fedha pekee haitoshi.
Viongozi wawe karibu nao, waonyeshe ni sehemu yao. Ikiwezekana waende kambini
na kula nao hata kulala nao. Unakumbuka nikiwa mfadhili wa Ushirika Moshi,
Simba ilikuwa inateseka sana, nilikuwa pamoja na wachezaji hadi kambini. Pia
Moro United, waulize Simba watakuambia na nilipokaa Yanga kwa mwaka mmoja na
nusu hivi, hawakuwahi kuifunga Yanga.
SALEHJEMBE:Unafikiri
kweli viongozi wa sasa wanaweza kulala kambini kama enzi za akina Viran au Azim
Dewji?
Mosha:
Ninaamini inawezekana, kiongozi asijikwaze na kuona yeye si saizi ya wachezaji.
Kwa kuwa ndiye kiongozi wao, basi awe nao pamoja.
SALEHJEMBE:Hauonekani
tena uwanjani, uliondoka kabisa Yanga, kipi ulifeli?
Mosha:
Sikufeli, ila niliona sisikilizwi. Nilitaka Yanga isiwe tegemezi kama sasa.
Nilitaka Yanga isiyotegemea mtu mmoja, ikaonekana ni kama nakosea, nikaamua
kuondoka.
Wanachama na mashabiki bado wanaamini
kuifunga Simba na kuongoza ligi ndiyo kila kitu. Hilo si sahihi, baadaye
yatakuwa ni mateso ya Yanga.
Ni timu kubwa lakini haina kitu, haina
maendeleo. Leo Yanga na hata Simba wanatakiwa kujifunza kwa Azam FC? Kweli watu
hawaoni, hawaumii na wanaona ushindi dhidi ya Simba pekee ndiyo unatosha!
SALEHJEMBE: Sasa
tatizo ni lipi hadi inashindikana?
Mosha:
Mfumo ni mbovu, Wanayanga pia hawaoni. Yanga inapaswa kuwa na vitega uchumi,
kuna Mafia na Jangwani. Vikiendelezwa itajitegemea. Leo hakuna hata anayeuliza
kwa kuwa kila mmoja anaona ubingwa na kuifunga Simba, inatosha kabisa! Si sahihi
hata kidogo hasa ukizingatia Yanga imeanzishwa mwaka 1935, leo inajifunza kwa
timu iliyoanzishwa miaka saba, nane iliyopita.
SALEHJEMBE:Lakini
ulipaswa ubaki badala ya kuondoka!
Mosha:
Niliona sieleweki, peke yangu nisingeweza. Nitabaki kuwa Yanga damu, lakini
muda, fedha zangu ninaona nielekeze kwingine kwa kuwa nina biashara zangu.
SALEHJEMBE: Vipi
utakwenda uwanjani Jumamosi?
Mosha: Hapana, nitaangalia tu mechi.
Nilishakata tamaa, naona kila siku tuko palepale.
SALEHJEMBE: Uliwahi
kusema kuhusiana na serikali kusaidia michezo, unaonaje kwa kipindi hiki?
Mosha:
Bado kabisa, naendelea kushauri na kusisitiza, serikali ijitokeze na kusaidia
kuweka mfumo bora katika michezo. Kila sehemu mambo ni ya kubahatisha, watu
wako kwenye michezo kwa ajili ya siasa au maslahi yao pekee. Serikali inaona na
haifanyi lolote.
Michezo ni furaha, afya na ajira. Hili
linaihusu serikali, ikae kati na kusaidia ukuaji wa michezo kwa mfumo bora na
sahihi.
| KIKOSI CHA YANGA |
SALEHJEMBE: Watu
wanakuwa katika michezo kwa maslahi yao, fafanua kidogo…
Mosha:
Mtu hajui michezo, kwa kuwa anajulikana, mwanasiasa au ana fedha. Basi anaingia
kuongoza, mwisho wake ni matatizo tu. Nawashauri watu kuipa nguvu michezo.
Wasaidie zaidi kuliko kujisaidia wao.
SALEHJEMBE: Nikimalizia,
Yanga hata Simba, hufanya maandalizi makubwa katika mechi ya watani tu, wewe
ulikuwa mmoja wao, huoni mnakosea sana?
Mosha:
Hilo nakubali kuwa si sahihi, maandalizi bora yanatakiwa katika mechi zote. Mpira
unaenda na historia, mechi hiyo inakuwa tofauti kutokana na historia ya timu zenyewe
na klabu pia. Hivyo inafanya iwe hivyo, ingawa nashauri kuwa, maandalizi bora
kwa kila mechi ni jambo bora zaidi.










0 COMMENTS:
Post a Comment