IRANZI (KUSHOTO) AKIPAMBANA NA HAJI MWINYI WA YANGA. |
Kama ilivyokuwa mwanzoni mwa msimu huu ambapo Yanga ilitumia mitego yake kuwanasa nyota wawili wa kimataifa raia wa Zimbabwe, Donald Ngoma na Thabani Kamusoko, pia mbinu hizo inatarajia kuzitumia kwa kiungo mshambuliaji na nahodha wa APR ya Rwanda, Jean Claude Iranzi.
Inadaiwa kuwa Iranzi amelipagawisha vilivyo benchi la ufundi la Yanga linaloongozwa na Mholanzi, Hans van Der Pluijm kutokana na aina ya uchezaji wake baada ya kuwasumbua vilivyo wachezaji wa Yanga katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Jumamosi iliyopita nchini Rwanda.
APR |
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga zimedai kuwa, hivi sasa uongozi wa timu hiyo upo katika harakati kabambe za kuhakikisha nyota huyo anatua klabuni hapo na kuungana na Wanyarwanda wenzake wawili ambao ni Mbuyu Twite na Haruna Niyonzima.
“Mwaka jana tulipoenda Zimbabwe kucheza na FC Platinum, tuliwaona Ngoma na Kamusoko na tukawasajili, pia safari hii tulipokwenda Rwanda kupambana na APR tumemuona Iranzi.
“Tutahakikisha tunamsajili kwa gharama yoyote ile kwa sababu ametupagawisha vilivyo, jamaa anajua sana, tukimpata tutatisha, lakini pia kama kuna watu watakuwa na wasiwasi wa uwezo wake, basi nawaomba Jumamosi wajitokeze uwanjani ili wamshuhudie,” kilisema chanzo hicho cha habari.
Alipoulizwa kuhusina na suala hilo, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano cha Yanga, Jerry Muro, alisema: “Tuliuona uwezo wa Iranzi, ni mchezaji mzuri na alitusumbua tulipokutana na APR lakini suala la kumsajili bado halijafika mezani kwangu, hivyo siwezi kulizungumzia ila litakaponifikia, basi nitaliweka wazi.”
Katika mechi ya kwanza iliyofanyika Rwanda, Yanga ilishinda kwa mabao 2-1, hivyo katika mechi ijayo inahitaji ushindi au sare yoyote ile ili iweze kusonga mbele kwenye hatua nyingine ya michuano hiyo.
PICHA: RT
0 COMMENTS:
Post a Comment