November 14, 2016




Na Saleh Ally
KUNA wakati unafikia unagundua kwamba mashabiki wengi wa soka nchini, ni watu wanaopenda kukurupuka na wanaofuata mkumbo wa kila wanacholetewa au kuelezwa bila ya kupima!

Mashabiki wengi wa soka, hata kama wanaona, hupenda kusikiliza zaidi. Si vibaya ukisema wanapitia uamuzi wa mambo fulani, basi wangependa kuhadithiwa hata kile ambacho wamekiona.

Ninamaanisha hivi, mtu kaliona jambo fulani, tena zaidi ya mara moja, lakini bado anaweza akatokea mtu akamhadithia basi yeye atakubali kile anachoambiwa licha ya kwamba ameona tofauti!

Msimu uliopita, hali ilibadilika na kiungo wa Yanga, Haruna Niyonzima aligeuka ghafla na kuwa kama adui wa mashabiki wengi wa Yanga huku akiingia kwenye mgogoro na uongozi wa Yanga na wengi wakaunga mkono, wakamshambulia na kusema mengi.

Wengi walikuwa wakimshambulia kwenye mitandao, kwamba Yanga ni kubwa, ataiacha na hawababaiki na maringo yake, wengine wakisema ujio wa Thabani Kamusoko kulikuwa hakuna sababu ya kuwepo kwake.

Niyonzima hata kama ni mtukutu, alionyesha ukimya na uvumilivu wa hali ya juu. Baadaye ikagundulika kwamba ndani ya uongozi, kuna kiongozi walikuwa hawaelewani na alikuwa akimfanyia visa, yakamkuta akapoteza kazi.

Wale waliokuwa wakimsakama, wakawa kimya, hawakusema lolote na mwisho amerejea na kuendelea kuitumikia Yanga tena akiwa na msaada mkubwa sana.

Wakati huu mjadala mkubwa imekuwa hata chenga ya Niyonzima, Wanayanga wengi wakijisifia na kuelezea ubora wake kila eneo huku wakitaka kumgeuza kuwa ni sawa na mtu aliyetua nchini leo au mechi mbili tatu alizocheza ndiyo za kwanza kuitumikia Yanga.

Wale ambao walikuwa wakilalama, wakijigeuza kuwa wachambuzi wa soka, kwamba Niyonzima anang’ang’ania mpira sana, anaupaka rangi sana, ndiyo vinara wa kuzungumza na kusifia kuhusiana na chenga zake.

Jiulize hizo chenga alipiga vipi akiwa hana mpira mguuni? Kama alifanya hivyo, maana yake si ndiyo ameng’ang’ania mpira? Sasa vipi leo hawalaumu?

Unajiuliza tena, kama Niyonzima atacheza kama Kamusoko, sasa kuna sababu gani ya kuwa na Kamusoko tena?

Huyu Niyonzima aliyecheza Yanga misimu zaidi ya miwili akiendelea kuisaidia kubeba ubingwa chini ya Ernie Brandts, baadaye chini ya Hans van Der Pluijm, huku nako akaisaidia kubeba ubingwa, akiwa anacheza kwa mfumo huohuo, vipi abadilike sasa?

Abadilike au anaonekana ni mbaya kwa kuwa Yanga imempata Kamusoko! Nani anajua kwamba mchezaji aliyesisitiza Kamusoko kusajiliwa Yanga ni Niyonzima baada ya Yanga kukutana na FC Platinum ya Zimbabwe katika michuano ya kimataifa?

Lazima tukubali, tumekuwa na tabia ya kukurupuka na baadaye kujisahau kuhusiana na masuala ya wachezaji. Mashabiki mmegeuka fimbo ya kuwatandika wachezaji wenu kwa kosa moja au mawili na mkasahau mazuri mia au mia mbili ambayo wamefanya na kusaidia timu nzuri.

Kama unataka kuniuliza mazuri ya Niyonzima, nitakushauri hata kufuatilia picha zake mitandaoni, utagundua chenga aliyompiga kiungo wa JKT Ruvu na kukaa haikuwa mara ya kwanza.

Inaweza kuwa gumzo kwenye vyombo vya habari kwa kuwa vyenyewe vinahitaji mambo kama hayo kwa wakati husika na kuyaripoti na likija jingine kwa wakati husika litaripotiwa pia.

Ndiyo maana ukiingia mtandaoni utaona Niyonzima amepiga chenga kama hizo nyingi tu, picha zinaonyesha. Lakini kuna picha nyingine nyingi za wachezaji wengine kama Emmanuel Okwi akimgaragaza Shadrack Nsajigwa na kadhalika, vyombo vya habari viko kazini.

Kwako shabiki, vizuri ukaonyesha uungwana na kuthamini kazi za wachezaji hasa unaowaunga mkono. Pia uamini nao ni binadamu, inapotokea wamekosea kidogo, ungana nao na hata kama unakosoa, basi punguza maneno ya jazba na kashfa.







4 COMMENTS:

  1. Umenena vyema kaka.huo ni ustaarabu ambao bado watanzania hatujafanikiwa kuwa nao.....sisi ni dakika mbili mbele wala hatuna mapenzi ya kweli na wachezaji tunatakaga muda wote tu tufurahishwe...tuna kazi za kujali hisia zetu bila kujali kuwa wachezaji na pia wana hisia

    ReplyDelete
    Replies
    1. Duniani kote mchezaji ni muhimu pale tu anapofanya vizuri. Muda si mrefu mashabiki wa RM walikuwa wanazomea kila Bale aliposhika mpira kwa sababu tu hawapi wanachokitaka, leo anawafungia magori muhimu hakuna anayekumbuka tena. Iliwahi kutokea mashabiki wa Arsenal wakawa wanaizomea timu yao, the same kwa Man U. So ukizingua pia mashabiki wanazingu pia. Duniani kote iko hivyo

      Delete
  2. Uko sahihi ila mimi navilaumu zaidi vyombo vya habari ambavyo mara nyingi vimekuwa vikiandika au kuzungumza mambo kwa mihemko huku vikijisahau kuwa wananchi wanaviamini hivyo kila wanachokifanya raia watakichukua.Ni vyombo vya habari hasa vimewafanya watanzania waendelee kuwa wale wale,wasio tafakari ila tu kuhamisha mambo toka kwenye vyanzo kwenda mitaani kama yalivyo na zaidi kuharibu.Mfano kuna hii ishu ya waamuzi wabovu pia muda mwingi inasumbua wanahabari matukio yote wanayo lakini hayalrti msaada wowote wakati huenda rekodi hizo zingesimamiwa kidete zingekuwa msaada.Yapo mengi naamin Salehe unayajua,ishu si tu kuchukua matukio,ishu pia kwanini unayachukua??,yanini? Na ishu sio tu kuripoti au kuandika,ishu kwanin unaripoti? Je taarifa zote zinzoripotiwa zinafanikisha malengo yale yanayowasukuma watu waripoti?? Au tukisharipoti tukipata pesa ndiyo yamekwisha tena hata kama malengo hayakufikiwa? Sawa lakin tukumbuke tunapoyaacha mambo haya hayamrudishi nyuma mtu mmoja au kikundi tu fulani ila ni nchi nzima tuna athirika.Pamoja na kwamba vyombo vya habari vinafanya kazi kwa maslahi lakini ni muhimu pia kuyapa kipaumbele maslahi ya taifa pia.

    Ni hayo tu,mi ni mwanadam kama kunasehemu nimekosea niwie radhi.

    ReplyDelete
  3. Hapo nilichokiona ulitaka kumzungumzia Okwi!! Ukweli ni kwamba watu hawakumchukia Niyonzima kwa kiwango chake bali kwa sababu walijengewa ushahidi wa kuwa ameleta jeuri!! Kusema kwamba Yanga ni kubwa kuliko Niyonzima bado ndo ukweli. Yanga wamepita wamgapi na timu bado ipo!?. Umewasahau akina Lunyamila, Chambua, Kizota nk!? Kuwa bora hakumfanyi mtu akawa juu ya timu. Waliachwa akina CR7, Kaka, Figo, Ronaldo, Beckham nk waondoke pamoja na yote waliyoyafanya. Niyonzima kuna watu walimtengenezea figisu, na washabiki walipogundua hilo mapenzi kwa mchezaji yakarudi zaidi ya mwanzo. Suala la kushangilia chenga hapa si issue maana ndo wakati uliopo!! Mtoto hawezi kuwa wa kwanza darasani, eti usimpe zawadi kwa sababu kila siku anakuwa wa kwanza!! Kinachoshagiliwa ni mwendelezo wa mazuri anayoyafanya. Na kama nia yako ilikuwa kuelezea chenga ya Okwi dhidi ya Nsajigwa hukuwa na sababu ya kumtumia Niyonzima kama chambo. Wewe ndo ulikuwa unapinga akina Boban kukosa nidhamu, leo unaweza vipi kufurahia mchezaji kukosa nidhamu kwa sababu ya ubora wake!? Be consistent

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic