April 17, 2017




Na Saleh Ally
YANGA wamefungwa mabao 4-0 katika mechi ya pili ya Kombe la Shirikisho (Caf) na sasa Tanzania haina mwakilishi tena katika michuano ya Caf katika ngazi ya klabu.

Kipigo hicho kinaifanya Yanga iwe imetoka kwa jumla ya mabao 4-1 baada ya ushindi wa bao 1-0 jijini Dar es Salaam.

Katika mechi ya jana, kwa yule aliyebahatika kuiangalia atakubaliana na mimi kwamba Yanga walisafiri wakienda kufungwa Algeria, walijua na walikuwa na uhakika.

Kwanza waliondoka wakiwa tayari wameanza kutanguliza madai yao ya mishahara ya mwezi mmoja mmoja. Wapo wachezaji waliobadili uamuzi wa mgomo baada ya Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji kwenda kuzungumza na wachezaji katika mazoezi ya mwisho na kuwaeleza kilichomtokea akisisitiza uvumilivu lakini akawaahidi hakuna haki yao itakayopotea.

Lakini bado uchezaji wa kikosi cha Yanga ulionyesha upungufu mwingi na hakukuwa na morali. Timu ilicheza ikionyesha haina kiongozi na hakika haikuwa imejiandaa kushinda.
Huenda walitaka kujaribu kuangalia kama itawezekana kushinda. Lakini walijua watafungwa, hawakuwa na furaha na hawakuwa tayari kuipigania Yanga kwa asilimia mia.

Mchezaji kama Obrey Chirwa yeye aliamua kung’ang’ania pasi yake ya kusafiria, akikataa viongozi wa Yanga kuichukua kwa ajili ya maandalizi ya safari hadi atakapolipwa mshahara wake anaodai.

Yanga ilimhitaji kwa kuwa alikuwa ndiye mshambulizi mwenye kiwango cha juu baada ya Amissi Tambwe na Donald Ngoma kuumia. Mechi ya juzi wamecheza wakionekana wazi hawakuwa na msaada hata kidogo.


Ngoma na Tambwe si wale waliozoeleka, wanahitaji mechi moja mbili, tatu kuanza kurudi vizuri. Chirwa angeisaidia Yanga, lakini akasahau hata alipotua nchini hakuwa na msaada licha ya kusajiliwa kwa zaidi ya Sh milioni 150.

Anajua alikaa benchi, alishindwa kufunga mechi kadhaa. Yanga wakaendelea kumvumilia lakini baada ya kuonekana tegemeo kashindwa kuonyesha uvumilivu, jambo ambalo linashangaza na Yanga wanashindwa kuonyesha wao ni klabu. Jiulize, alipwe wa nini sasa? Kwenye mshahara wa Aprili, hakuwa kazini bila ruhusa ya mwajiri. Sasa kwa nini alipwe?

Bao la kwanza:
Wakati Mohamed Derrardja anapiga krosi na mpira kuguswa na Said Juma ‘Makapu’, unaona mmaliziaji Said Aouedj anatokea nyuma ya Mwinyi Haji, anamalizia wavuni.

Mwangalie Mwinyi, anageuka kama kitu kisichomuhusu akijua wazi hakuwa amemkaba mtu ambaye amekimbia na kufunga mbele yake.

Bao la pili:
Safari hii Mohamed Derrardja ambaye ni mtaalamu wa kupiga mipira iliyokufa wa MC Alger, anafunga kwa mkwaju wa adhabu. Unaweza kushangazwa na Yanga waliokubali kumuweka Hassan Kessy kwenye ukuta. Lakini kuonyesha hakuna tahadhari au mafunzo ya kutosha, Kessy aliruka na kuondoka kwenye ukuta. Mpigaji akatumia nafasi hiyo kufunga kirahisi kabisa na kipa Deogratius Munishi ‘Dida’ hakuwa na nafasi ingawa ukiangalia bila kupima unaweza kuamini ni uzembe wake.

Kessy ni mfupi, angeweza kutolewa na kwenda mbele kama namba tisa wakati Ngoma na wengine wote wakirudi nyuma. Baada ya Yanga kupata mpira anashuka katika nafasi yake wanakwenda kushambulia. Ilikuwa lazima kujilinda na mapigo ya faulo ya Waarabu hao kwa kuwa wanajulikana.

Bao la tatu:
Zacharia Mansour ndiye alifunga bao la tatu akipokea krosi ya Hadj Bougueche, Dar walimtunga jina la “Mwarabu Mweusi”.

Bougueche alitokea nyuma ya Kessy wakati krosi inapigwa ambaye hakugeuka wala kutaka kujua nini kinatokea nyuma yake. Lakini wakati Mansour anafunga Yanga ilikuwa na wachezaji watatu ndani ya boksi, lakini hakuna aliyekuwa na msaada na kipa.

Bao la nne:
Huenda hili ndiyo bao lililodhihirisha Yanga walikuwa tayari kufungwa Algeria. Wakati Aouedj anafunga, utaona hivi, kulikuwa na wachezaji nane wa Yanga pamoja na kipa wakiwa wamewazunguka wachezaji watatu wa MC Alger.

Wanne akiwemo Thabani Kamusoko, Haruna Niyonzima, Kessy na Makapu walikuwa wanatembea kama vile mechi ilishakwisha! Andrew Vincent ‘Dante’, Kelvin Yondani na Mwinyi walijaribu kupambana kuzuia, wakazidiwa ujanja.
Yanga walishafungwa tatu, kweli walikuwa wametolewa lakini walikuwa na jukumu la kuzuia mabao kuendelea kuingia.

Lwandamina:
Kocha George Lwandamina anapiga makofi tu baada ya Yanga kufungwa bao la pili, haumuoni kuchangamka na kuwaita wachezaji na kuanza kuwapa maelekezo ya haraka na kipi walikosea.

Wakati mwamuzi anasumbuka kuwarudisha wachezaji wa MC Alger uwanjani, wakati huo ulikuwa ni wa Lwandamina kuanza kuzungumza na wachezaji kuhakikisha hawarudii makosa yanayofanana si kuendelea kupiga makofi akiamini ndiyo hamasa.

Kiongozi:
Kila bao lililofungwa, wachezaji wa Yanga walionekana “wamekufa” kabisa. Hakuna wa “kuwafufua”, kocha alikuwa anapiga makofi tu!

Lakini nahodha je? Kuwaita wenzake angalau kuzungumza nao au kuwapigia kelele kuendelea kujitahidi ikiwezekana kuwakumbusha kuhakikisha wanapambana zaidi wasikumbane na aibu ya kufungwa mabao mengi? Yote hii haikuwa sawa na imechangia wao kufungwa mabao mengi zaidi na utaona makosa yanafanana kwa kuwa hakukuwa na kukumbushana kwa kutosha.

Inawezekana kuna matatizo ya uongozi, ya wachezaji nayo yameonekana. Lakini tayari Yanga imepoteza uvumilivu miongoni mwao, itakuwa aghalabu kuwa na umoja na inaonekana wazi hakuna upendo.

Uongozi wa klabu hiyo ukishindwa kufungua macho mapema, basi adhabu, maumivu na mateso ya kila mara yataendelea sana tu!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic