March 10, 2018




MUNICH, Ujerumani
BAYERN Munich inaongoza kwa tofauti ya pointi 20 katika Ligi Kuu ya Ujerumani ‘Bundesliga’ na inaelekea kutwaa taji la sita mfululizo la ligi hiyo endapo itashinda mechi tatu mfululizo.

Ipo hivi, katika ligi ya Bundesliga inayoonyeshwa live nchini na StarTimes, Bayern ina pointi 63 kileleni ikifuatiwa na Schalke 04 yenye pointi 43 na timu zote zimecheza mechi 25.

Bundesliga ina mechi 34 ambazo kila timu inatakia kucheza, hivyo kwa sasa timu zote zimebakiza mechi tisa na kama Bayern ikishinda mechi zote itafikisha pointi 90. 

Lakini Schalke 04 hata kama ikishinda mechi
zote zilizobaki itafikisha pointi 70.
Hiyo ina maana kwamba, Bayern yenye pointi 63, ikishinda mechi tatu tu itafikisha pointi 72 ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote ile, hivyo itakuwa imeshajitangazia ubingwa mapema.

Ijumaa wiki iliyopita ikiwa chini ya Kocha Jupp Heynckes, Bayern iliisambaratisha Freiburg mabao 4-0 na kufikisha pointi 63 zinazowafanya wasubiri pointi nane tu ili watangaze ubingwa.

Bayern pia inahitaji pointi mbili tu ili iweze kufuzu kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.

"Sasa ni wakati wa kuonyesha uzoefu wetu, Jupp Heynckes hatodharau chochote sasa licha ya kuwa katika nafasi nzuri," anasema Mwenyekiti wa Bayern, Karl-Heinz Rummenigge.

Bayern ilikuwa imeachwa kwa pointi tano katika ligi wakati ikimtimua kocha wake Carlo Ancelotti, Oktoba mwaka jana, lakini tangu Heynckes, 72, akabidhiwe mikoba ameweza kurejesha nidhamu na timu inafanya
vizuri.

Ni wachezaji wawili winga Kingsley Coman na kipa Manuel Neuer ndiyo hawapo katika kikosi cha Bayern kutokana na kuwa na majeraha lakini Javi Martinez, Arjen Robben na Robert Lewandowski ndiyo wanaofanya kazi ya maana kwa sasa.

WANAIVAA HAMBURGER

Leo Jumamosi saa 11:30 jioni, Bayern itakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa
Allianz-Arena kucheza na Hamburger SV ambayo ipo nafasi ya 17 ikiwa na
pointi 18 tu.
Wakati Bayern ikiwa imeshinda mechi 20 kati ya 25 ilizocheza ikitoka sare tatu na kupoteza mara mbili, Hamburger wao wameshinda mara nne tuna wamefungwa mara 15 na kutoka sare sita.

Takwimu zinaonyesha Bayern inacheza mechi dhaifu leo hivyo kuna uwezekano mkubwa ikashinda.

MECHI NYINGINE ZA BUNDESLIGA LEO

Hoffenheim        v       Wolfsburg

Hannover 96       v       Augsburg

Hertha BSC        v       Freiburg

Leverkusen         v       B. M'gladbach



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic