YONDANI ALETA BEKI MPYA YANGA
Beki mkongwe na nahodha wa Yanga, Kelvin Yondani amesema amesikia taarifa za kutua beki wa Lipuli FC, Ally Mtoni ‘Sonso’ na kutamka: “Mbona yupo freshi tu, nileteeni”.
Kauli hiyo ameitoa ikiwa ni siku chache tangu ziwepo tetesi za beki huyo kuwaniwa na Yanga katika usajili huu wa dirisha dogo uliofunguliwa Novemba 15, mwaka huu.
Kocha Mkuu wa Yanga Mkongoman, Mwinyi Zahera hivi karibuni alitoa mapendekezo ya usajili kwa uongozi wa timu hiyo akiomba beki wa kati, kiungo, winga na mshambuliaji ambayo tayari yameanza kufanyiwa kazi.
Kwa mujibu wa Championi Ijumaa, Yondani alisema anaufahamu vizuri uwezo wa Sonso ni beki mwenye sifa zote za kuichezea Yanga ambao ameuona akiwa naye kwenye timu ya taifa, Taifa Stars.
Yondani alisema kama uongozi wa Yanga ukifanikiwa kumleta Sonso, basi utaimarisha vema safu yao ulinzi ya kati kutokana uwezo mkubwa alionao uwanjani.
Aliongeza kuwa amecheza na Sonso mara kadhaa wakiwa na kikosi cha Taifa Stars na mchezo wa mwisho walipocheza na Lesotho katika kufuzu wa Afcon, hivyo hana hofu naye.
“Mimi nilishawahi kuzungumza na Sonso mara kadhaa tukiwa kwenye kambi ya Stars kuhusiana na mipango yake na kikubwa nilimwambia mkataba wake ukimalizika aje Yanga.
“Na uzuri yeye mwenyewe alikubali kuja kuichezea Yanga na nilifanya hivyo baada ya kumuona ni beki anayejiamini na mwenye maamuzi sahihi kwa wakati sahihi.
“Ni matarajio yangu kumuona Sonso akija kuichezea Yanga katika usajili huu wa dirisha dogo, kikubwa viongozi wafuate kanuni za usajili kwa kuifuata Lipuli kabla ya kumfuata Sonso mwenyewe kama unavyofahamu ni mchezaji mwenye mkataba,” alisema Yondani.
0 COMMENTS:
Post a Comment