May 1, 2019


LIGI Kuu Tanzania Bara inazidi kupasua anga, ambapo kwa sasa ni mzunguko wa pili na timu zote zipo kwenye Lala Salama.

Kwa sasa kuna timu tano ambazo mwendo wake ni wa kusuasua kutokana na pointi ambazo wanazo kibindoni pamoja na idadi ya michezo ambayo wamebakiwa nayo hivyo kama hawatapambana kuna hatihati wakafungua mlango wa kurejea Ligi Daraja la kwanza.

Hizi hapa kwa sasa zipo nafasi tano za chini kwenye msimamo wenye timu 20:-

1. African Lyon.

Timu hii imepanda Daraja msimu huu, haijawa na matokeo chanya kwenye Ligi Kuu Bara kwani katika michezo 33 iliyocheza imeshinda michezo minne pekee na kufungwa jumla ya michezo 19 na kuambulia sare michezo10.

Mpaka sasa wamejikusanyia jumla ya pointi 22 na wamefunga jumla ya mabao 43 huku safu yao ya ushambuliaji ikifunga jumla ya mabao 19 wanashika nafasi ya 20 kwenye msimamo.

Ruvu Shooting

Mwenendo wake msimu huu umekuwa wa kusuasua licha ya kutokuwa na tatizo kwa wachezaji wala benchi la ufundi kutokana na kulipwa mshahara kwa wakati, kwenye michezo 33 waliyocheza wameshinda michezo 8 pekee na kupoteza michezo 13.

Wapo nafasi ya 19 wakiwa wamejikusanyia pointi 36, wamefungwa jumla ya mabao 39 huku safu yao ya ushambuliaji iliyo chini ya Hassan Dilunga ikiwa imetupia mabao 28.

Mbao FC

Msimu walianza kwa kasi na walikaa kileleni kwa muda wa miezi kadhaa, aliposepa Kocha Mkuu, Amri Said mambo yakaanza kubadilika, ghafla kwa sasa wapo nafasi ya 18 baada ya kucheza mechi 33.

Kibindoni wanapointi 37, wameshinda michezo tisa na sare 10 huku wakipoteza michezo 14 mpaka sasa kwenye ligi, wapo nafasi ya 18.

Alliance FC

Kasi yao ni ya kupanda na kushuka, ni miongoni mwa timu ambazo zimepanda Daraja msimu huu ikiwa imecheza michezo 33 imejikusanyia pointi 37 kibindoni ipo nafasi ya 17 kwenye msimamo.

Imebakiwa na michezo mitano kukamilisha mzunguko wa Ligi Kuu Msimu huu.

Biashara United

Kama ilivyo kwa Alliance nao pia wamepanda Daraja Msimu huu, ni timu inayotokea Mara kwa wafanyabiashara, inajiendesha kwa nguvu za wananchi huku hali ya ukata ikiwasumbua na kuwafanya wawe na mwenendo wa kusasua.

Kocha Mkuu Amri Said amesema ana imani na kikosi chake kubaki msimu ujao kwa kushinda michezo yake mitano iliyobaki, ipo nafasi ya 16 ina pointi 37 ikiwa imecheza michezo 33.

1 COMMENTS:

  1. Sio Hassan Dilunga, ni Said Dilunga ndo yupo Ruvu Shooting!!!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic