September 29, 2019



MOTO utawake leo uwanja wa Karume kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara ambao utawakutanisha mabingwa watetezi Simba ambao watakaribishwa na Biashara United kuzisaka pointi tatu muhimu ndani ya Ligi Kuu Bara.

 Simba imecheza jumla ya mechi tatu na kushinda mechi zake bila kupoteza hata moja huku wenyeji Biashara United wakiwa wamepoteza michezo mitatu na kujikusanyia pointi moja pekee kwani walipoteza michezo mitatu na kutoa sare moja.

Biashara United ilifungua kete yake ya kwanza kwa kupoteza mbele ya Kagera Sugar wakiwa nyumbani kwa kufungwa mabao 2-0 dhidi ya Kagera Sugar na wakapoteza mchezo wa pili mbele ya Mbao FC kwa kufungwa bao 1-0 ugenini uwanja wa CCM Kirumba wakaambulia sare mbele ya Alliance kwa kufungana bao 1-1 na kupoteza mchezo wake wa nne mbele ya JKT Tanzania kwa kufungwa bao 1-0 uwanja wa Karume.

Simba wao kwa sasa wameanza kuwasha moto ndani ya TPL kwani michezo yao yote mitatu wamekomba pointi tatu walianza kukusanya pointi mbele ya JKT Tanzania kwa ushindi wa mabao 3-1 kisha wakasepa na pointi tatu mbele ya Mtibwa Sugar kwa ushindi wa mabao 2-1 na kumalizia kulipa kisasi mbele ya Kagera Sugar kwa ushindi wa mabao 3-0 uwanja wa Kaitaba.

Mambo haya yatanogesha mchezo wa leo na kuufanya uwe wa kuvutia kwa timu zote mbili ndani ya dakika 90:-

Kuvunja mwiko na kuendeleza ubabe

Hapa timu zote mbili zinahaha kutafuta rekodi mpya kwa kuvunja mwiko na nyingine ikihaha kuendeleza ubabe. Biashara hesabu zao kubwa ni kuvunja mwiko ambao msimu uliopita ulivunjwa na Simba kwa kufungwa mabao 2-0 na yote yakifungwa na nahodha John Bocco jambo lililowaumiza mashabiki na viongozi hvyo leo lao ni moja tu kulipa kisasi.

Simba wao wanaingia uwanjani wakiwa na hesabu za kuendeleza ubabe wao ambao waliuanzisha msimu uliopita kwa kusepa na pointi tatu muhimu ili kulinda rekodi yao ya kucheza mechi nyingi bila kufungwa.

Heshima

Biashara United leo inahitaji heshima kwani inatambua kwamba Simba ana hasira za kutolewa Ligi ya Mabingwa hivyo lazima apambane kurejea kwenye ubora wake msimu ujao jambo ambalo litaongeza ushindani wa mchezo wa leo.

Pia Simba haitakuwa na presha kubwa kwenye mchezo wa leo kutokana na matokeo ambayo imeipata mpaka sasa kwenye michezo yake mitatu kwa kujikusanyia pointi tisa wakiwa ni vinara kwenye ligi.

Tatizo la Biashara limefanyiwa kazi

Tayari kwenye michezo minne ambayo wamecheza mpaka sasa, safu ya ushambuliaji wa Biashara United imeonesha kuwa ni nyanya huku washambuliaji wake wengi wakiwa ni butu jambo ambalo limefanya Kocha Msaidizi, Omari Madenge kulifanyia kazi kwa ukaribu hivyo leo atatesti mitambo yake upya mbele ya Simba.

Mpaka sasa safu ya Biashara United imefunga bao moja pekee ndani ya dakika 360 huku Innoncent Edwin ndiye aliyefunga bao mbele Alliance wakati timu ikilazimisha sare ya kufungana bao 1-1.

Kagere leo kazi anayo

Mshambuliaji wa Simba, Meddie Kagere ndiye mchezaji atakayekuwa analindwa leo na Biashara United kutokana na kasi yake ya kucheka na nyavu kwani ndani ya dakika 270 ambazo ni sawa na mechi tatu ametupia jumla ya mabao matano na akitoa assiti mbili za mabao.

Karume yaigomea Biashara

Kwenye michezo miwili ambayo Biashara United wamecheza uwanja wa Karume hawajaambulia hata bao moja zaidi ya kuruhusu mabao matatu na kupoteza jumla ya pointi sita kwani walianza kufungwa mbele ya Kagera Sugar mabao 2-0 kabla ya kupoteza mbele ya JKT Tanzania kwa kufungwa bao 1-0.

Hasira za kupoteza michezo miwili ya nyumbani ziliufanya uongozi wa Biashara United kuketi kikao kizito wakiongozwa na Mwenyekiti Seleman Mataso kutafuta dawa mpya ambayo itaanza kufanya kazi leo mbele ya Simba.


Makocha hawa hapa

Omary Madenge , Kocha msaidizi wa Biashara United amesema kuwa wanatambua mchezo utakuwa mgumu ila watapambana.

“Msimu uliopita tuliambulia pointi moja kwa Simba, msimu huu tupo vizuri na lengo letu ni kuona tunapata pointi tatu muhimu.

Patrick Aussems, Kocha wa Simba amesema kuwa mchezo utakuwa mgumu kutokana na ugumu wa uwanja pamoja na ushindani ila hesabu zake ni pointi tatu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic