December 27, 2019



MAMBO yanazidi kupamba moto ambapo kwa sasa kombe la Shirikisho linazidi kuchanja mbunga kwa kila timu kuvuna kile ilichokipanda ndani ya dakika 90 jambo ambalo linaongeza utamu wa soka ndani ya uwanja.

Tunaona kwamba kuna timu ambazo zimeingia kushiriki zikiwa hazijui zinataka nini jambo ambalo linafanya ziambulie kichapo kikubwa kutokana na kushindwa kujiandaa vema huku zile zilizojiandaa zikipata ushindi.

Ukweli kwenye mpira huwa haubadiliki timu iliyojiandaa vema ndiyo inapata matokeo ila ile ambayo inajiingiza kwenye propaganda na maneno kibao ni maumivu hupokea mwisho wa siku.

Tumeona kwamba kuna timu ambazo hazijui utamu wa Ligi Kuu zinawapa taabu wakubwa ambao wanashiriki ligi hii sio miujiza bali ni maandalizi ya timu husika mwisho wa siku inapata matokeo chanya.

Tukuyu Stars imeonyesha umwamba na ufahari wa kujiandaa bila kujali inacheza na timu iliyo kwenye hatua gani bali ilijikubali na ikajipanga mwanzo mwisho.

Baada ya dakika 90 iliibuka na ushindi wa mabao 4-3 mbele ya Singida United ambayo inashiriki Ligi Kuu Tanzania Bara jambo ambalo linaonyesha kwamba vijana walijipanga na walikuwa na nia ya kile wanachokifanya.

Kujipanga kwao nje na ndani ya uwanja kumewapa matokeo chanya na wanasonga mbele huku wakiwaacha Singida United wakitafuta pale ambapo walikwama wanastahili pongezi katika hilo.

Sio Tukuyu tu hata Coastal Union nao walionja joto ya jiwe kwa kutolewa na timu ambayo haishiriki ligi kuu jambo linalomaanisha kwamba kila mmoja anaweza, African Sports nao wanastahili pongezi licha ya kushinda kwa changamoto ya penalti.

Kwa timu ambazo zimepewa zigo la mabao sio jambo la kufurahisha kwani mchezo wa mpira sio sawa na rede timu ifungwe mabao mengi inamaanisha udhaifu kwa timu ni mkubwa na hazijachukulia umakini mashindano haya.

Ukianza na Iringa United pamoja na Arusha FC hizi kwa sasa inaonyesha zimefungwa mabao mengi zaidi kuliko timu nyingine ambazo zinashiriki michuano ya kombe la Shirikisho.

Licha ya kufungwa na timu ambazo zinaitwa kubwa na kongwe bado zinastahili kuonyesha ushindani na ukomavu kwa kile ambacho wanacho kwenye mashindano haya kwani fainali kila timu ina nafasi ya kushinda.

Yanga ambayo ilipata ushindi wa mabao 4-0 mbele ya Iringa United kabla ya watani zao Simba kushinda mabao 6-0 mbele ya Arusha FC wanastahili pongezi ila hawa waliofungwa nao wanastahili kujitathimini wapi walikwama.

Ikumbukwe kuwa Simba iliyoshinda mabao 6-0 ni ile iliyofungwa mabao 3-2 na Mashujaa ambao nao walikuwa ligi Daraja la Kwanza msimu uliopita jambo ambalo linamaanisha kwamba hata timu zinazoitwa kubwa zinafungika.

Kuna umuhimu mkubwa kwenye michuano ya Shirikisho kwa timu kucheza kwa kujituma na kutumia tahadhari kubwa hasa zinapocheza na wale ambao wanaona wamewazidi uwezo kwa kutumia akili nyingi na mbinu.

Timu nyingi zimekuwa zikishiriki michuano katika hali ya ukawaida bila ya kuwa makini jambo ambalo linawafanya wapoteze ushindi mapema kabla ya mechi kuisha.

Tumeona Simba wenyewe wamekiri kwamba msimu uliopita walishindwa kuyapa uzito mashindano haya jambo lililowapa chati Mashujaa ambao nao msimu huu wamepoteza mapema kwenye hatua ya 62.

Wakati uliopo kwa sasa kwa timu ambazo zinashiriki michuano ya kombe la Shirikisho kuona namna gani zinapata matokeo chanya kwani siri ya ushindi kwenye mpira ni kujiandaa.

Timu zilizopata nafasi ya kusonga mbele zinatakiwa kujipanga upya zisipate vichapo vya aibu kwa kuwa ukubwa wa mashindano hauchangiwi na idadi ya mabao bali umakini wa wachezaji.

Kila timu ambayo itajipanga vema ina nafasi ya kushinda bila kujali aina ya timu ambayo inacheza nayo endapo itaamua kuongeza nguvu mwanzo mwisho ina nafasi ya kupata matokeo chanya.

Kila mchezaji anatakiwa atumie nguvu zake zote na akili kutafuta matokeo na sio kujidanganya kwamba hayana faida mashindano haya ambayo yanaendelea kushika kasi.

Tunahitaji kuona bingwa anakuwa ni yule aliyestahili kwa kupambana mchana hata usiku kupata matokeo chanya kwa kuwa mshindi ana nafasi ya kupeperusha bendera ya taifa kwenye michuano ya kimataifa.

Hatua nzuri ambayo ipo kwa timu shiriki zile za ligi daraja la kwanza na la pili ni muda wao kujipanga vema kupambana kwa ajili ya mechi za ushindani ambazo zinaendelea.

Kila siku wachezaji wanastahili kujiuliza ni kazi gani ambayo wanaifanyia timu yao bila kujali aina ya michuano ambayo wanashiriki kwa sasa.

Imani yangu ni kwamba waamuzi watafuata sheria 17 za mpira kuendeleza ule ubora na utamu wa mechi ambazo unaendelea kwa sasa.

Mashabiki ni wakati wenu kuendelea kujitokeza kwa wingi kuzipa sapoti timu zenu zinapobambana ili zipate matokeo chanya ambayo mnayahitaji.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic