Mwaka 2019 ulikuwa na mengi yalitokea na hatimaye ukurasa umefungwa na taratibu tumeanza kuumega mwaka 2020 ni suala la kushukuru kwa
Mungu na kuomba atujalie uzima wakati mwingine tuonane tena mwaka ujao.
Basi yote tunayoyapanga
tusisahau kwamba hapa tunapita na kazi yetu kubwa kwa sasa ni kuishi kwa amani
na upendo hakuna namna nyingine ya kufanya zaidi ya hayo tu ndugu yangu.
Leo napenda kuzungumzia
juu ya mchezo ambao umezidi kuwa juu kwa wadau na wafuatiliaji wa soka Bongo na
nje ya Bongo ni kutokana na msisimko wake ambao upo kwenye soka.
Itakuwa ni mechi ya
kwanza ndani ya mwaka 2020 ambayo itakuwa na ushindani mkubwa kwa timu zote
mbili kubwa zinazosaka ubingwa wa ligi kuu.
Simba ni mabingwa
watetezi walitwaa msimu uliopita na sasa wanaingia kwenye vita kupambana na Yanga ambao walianza kwa kusuasua
kabla ya kurejea kwenye mstari na sasa vita imepamba moto.
Itakuwa ni Januari 4,
2020 ni siku ambayo mchezo huu unatarajiwa kuchezwa uwanja wa Taifa wenye uwezo
wa kubeba mashabiki 60,000 wakitazama uhondo ndani ya uwanja huo.
Kikubwa ni kuona kwamba
kila mmoja anatafuta ushindi utakaowafanya wawe ndani ya vita ya kufuata
ulipo ubingwa ila kikubwa tunachohitaji ni burudani safi na sio vita kwa
mashabiki na wachezaji.
Ukweli ni kwamba nchi
itasimama kwa muda kushuhudia watani wa jadi
wakipiga mechi yao ya kwanza ya msimu wa 19/20 kitu ambacho kinasubiriwa kwa
shauku kubwa.
Ni mechi ambayo imebeba hisia kubwa kwa pande
zote za Yanga/ Simba mchezo huu huwa hautabiriki kirahisi kwa wapinzani wote
wawili kutokana na kila timu kujiandaa kwa presha kubwa na hofu.
Huwa haitabiliki kwenye
matokeo yake bila kujali ni timu ipi ipo vizuri kiuchumi ama ipo vibaya
kiuchumi haina hiyo ni vita ya kweli ambayo haichagui silaha ila ikikupata
inakupoteza jumla.
Kila timu imekuwa na mbinu zake ambapo kwa
upande wa Simba imekuwa ikitegemea sana viungo katika kuandaa mashambulizi na
kumalizia jambo ambalo linaifanya iwe na unyumbulifu muda mwingi.
Mkwasa naye ana mbinu
yake ya kushambulia kwa kushtukiza na kutumia mabeki wake kuanzisha
mashambulizi huku viungo wake wakiwa nao kwenye ubora wake jambo linaloongeza
utamu.
Matumaini yangu kwamba, Charlse Mkwasa anajua vema mbinu za mpinzani wake na Sven Vanderbroeck naye anatambua
mbinu ya mpinzani wake jambo litakalonogesha vita ya watani hawa wa jadi.
Kitu cha msingi ni kwa
kila timu kujiandaa vema na kufanya maandalizi mazuri nje na ndani ya uwanja
ili waweze kupata matokeo ambayo wanahitaji kuyapata ndani ya uwanja.
Marefa watakaopewa
jukumu la kuchezesha mechi hiyo wanapaswa wafuate sheria 17 za mpira ili
kuongeza ile ladha ya soka ndani ya uwanja bila kutibua mambo.
Nina amini kwamba
endapo kila mmoja atatimiza jukumu lake kwa wakati tutampata mshindi kwa haki
bila vurugu zozote zile na mtindo wa kuvunja viti utasahaulika milele.
Mshindi ni yule ambaye
atajiandaa vema na sio yule atakaywekwenda na matokeo uwanjani huyo amejiandaa
kufeli mapema kabla ya mchezo.
0 COMMENTS:
Post a Comment