March 21, 2020


HIVI sasa kila kona stori kubwa ni uwepo wa ugonjwa wa Covid-19 unaotokana na Virusi vya Corona.

Jamii nzima imekumbwa na taharuki juu ya uwepo wa virusi hivyo ambavyo vinaenea kwa kasi mno. Wana michezo nao ni miongoni mwa waathirika wa Virusi vya Corona.

Tumeshuhudia nchi za wenzetu kwa maana ya barani Ulaya wakianza kuahirisha ligi zao kutokana na ishu hiyo, awali zilianza kwa kuchezwa bila ya uwepo wa mashabiki.

Ikaonekana kwamba si suluhisho la kuzuia kusambaa kwa virusi hivyo, ligi zikasimamishwa moja kwa moja kwa takribani siku 30.
Tanzania pia ligi zake zimesimamishwa, hiyo ilikuja baada ya mapema wiki hii Serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kutangaza kufunga shughuli mbalimbali hapa nchini zikiwemo za soka kwa siku 30.

Kuanzia Jumanne ya wiki hii lilipotoka agizo hilo, ligi zote zikasimamishwa ambapo tunatarajia ligi hizo kuendelea mwezi ujao.

Wakati ligi zikisimamishwa, kuna baadhi ya timu zilikuwa tayari zimesafiri kwenda kucheza mechi sehemu fulani, hivyo zile gharama zimeenda na maji.

Ingawa ni kweli timu hizo zimepata hasara, lakini ni jambo zuri pia kwao kutocheza mechi hizo kwani pengine ingeweza kuleta madhara kwao.

Serikali imekuwa ya kwanza kutoa elimu juu ya kujikinga na virusi hivyo ambavyo hapa nchini hadi sasa kuna wagonjwa kadhaa wameripotiwa kukumbana navyo.

Pia tumeshuhudia klabu nazo zikiwa mbele kusapoti kile inachofanya Serikali. Hivi sasa kila siku tunaona kwenye akaunti za mitandao ya kijamii ya klabu mbalimbali hapa nchini zikiposti juu ya namna ya kujikinga na Corona.

Hili ni jambo zuri na la kizalendo ambalo linaonyesha nje ya kuwa klabu za soka lakini kwenye suala la kijamii zimejitokeza mbele na kutoa elimu kwa watu wake ambao wanazifuatilia.

Suala hilo liwe funzo kwa timu nyingine na zichukue elimu ya kwamba zina jukumu la kufanya hivyo kwa sababu elimu ambayo wataitoa inafika kwa watu wao ambao wamekuwa wakiwashabikia.

Kuwapa elimu litakuwa jambo la maana sana kwa sababu mtawakinga na ugonjwa huo ili kwa hapo baadaye watakapokuwa wazima waje kuwashangilia kwa mara nyingine.

Hakuna ambaye kwa sasa haufahamu ugonjwa huu ulivyo hatari sana. Umeua maelfu ya watu duniani mpaka sasa. Kwa Tanzania bado hakuna taarifa za kifo, lakini ni vema tukaendelea kupambana nao na kuushinda.

Nichukue nafasi hii kulipongeza Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa juhudi zao za makusudi za kutii agizo la Serikali kwa kusimamisha ligi zake. Hivyo shikilieni hapohapo kwani usalama wa afya kwa kila mmoja ni jambo muhimu sana.

Pia TFF imeenda mbali zaidi kwa kusema baada ya kupita hizo siku 30, kuna uwezekano mkubwa wa ligi kuchezwa bila ya mashabiki. Hili pia limekaa poa.

Kubwa zaidi katika kuchukua tahadhari, baada ya kupita siku hizo 30, wachezaji wote watapimwa kabla ya kucheza mechi. Ni uamuzi sahihi kabisa.

Niwaombe Watanzania wasiuchukulie kawaida huu ugonjwa, wafahamu upo na ni hatari sana.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic