April 17, 2020



ZINEDINE Zidane anatajwa kuwa ndiye kocha bora ndani ya Klabu ya Real Madrid, lakini ubora wake siyo kwenye kufundisha tu, bali na kuvumbua vipaji vya wachezaji wengi.


Zidane amekuwa na ile pua nzuri ya kunusa vipaji ambavyo vimepata nafasi ya kuonyesha uwezo wao na hii ni baada ya kutambua uwezo wao mapema.


Kuna vipaji sita ambavyo amevivumbua na ikawa faida kwa Klabu ya Real Madrid. Kwa sasa pua yake inaonekana kunusa kwa dogo wa miaka 17 anayeichezea Rennes ya Ufaransa, Eduardo Camavinga.


Wakati wa uchezaji wake soka, Zidane alikuwa fundi kweli, akaja kwenye ukocha anafanya vizuri, lakini sasa anatajwa kuwa mmoja wa maskauti wazuri.


Timu yake ya mwisho kuichezea ilikuwa Madrid ambayo alianza kuichezea 2001, hadi 2006.


Mwaka 2014 akaanza rasmi ukocha akianzia timu ya vijana ya Real Madrid, kisha 2016 hadi 2018 akaifundisha timu ya wakubwa, akaondoka na kurudi 2019 ambapo yupo hadi sasa.


Baadhi ya nyota ambao Zidane ambaye ni mtu anayeheshimika ndani ya Real Madrid amewaibua na leo hii wanatamba, ni hawa hapa:



Kylian Mbappe
Ni miaka saba sasa Zidane amekuwa akipambana kutaka kuhakikisha Kylian Mbappe anatua ndani ya viwanja vya Santiago Bernabeu.


Zidane alianza kumsaka Mbappe akiwa mdogo katika Kituo cha Kukuza Soka cha Monaco.


Katika hilo akishirikiana na Rais wa Real Madrid, Florentino Perez, bado wanapambana kuona wanamsajili haraka iwezekanavyo.


Mbappe, 21, kwa sasa anakipiga PSG, mwaka 2012 Zidane aliomba asajiliwe ndani ya Real Madrid.


Baada ya kushindwa kusajiliwa, Mbappe alinukuliwa akisema: “Sikutaka kwenda Madrid kwa sababu nilitaka kubaki ndani ya nchini yangu.”


Mwaka 2017, Mbappe akaibuka kuwa Mchezaji Bora Ulaya mwenye umri mdogo akiwa na miaka 18.


Madrid wakaanza mazungumzo na familia yake ili kuona wanafanikiwa kumsajili dogo huyo na mpaka sasa bado yupo mikononi mwa PSG, ila Zidane bado hajakata tamaa.



Eden Hazard
Msimu uliopita, Madrid ilimnunua, Eden Hazard kwa kiasi cha euro 100m, lakini ilikuwa atue kikosini hapo tangu 2009 na Zidane alikuwa anashauriana na rais wa klabu hiyo, Florentino Perez.


Mwaka 2009, Zidane aliwahi kusema: “Natamani kumleta Hazard hapa Madrid nikiwa nimefumba macho.”


Lakini hakukata tamaa, aliendelea kumuwinda mpaka alipofanikiwa kumpata msimu huu.


Hazard sasa yupo ndani ya Madrid, lakini ameanza vibaya kutokana na majeraha ya mara kwa mara.



Raphael Varane
Akiwa na miaka 18, Raphael Varane akiicheza Lens ya Ufaransa, huko ndiko Zidane aliona uwezo wake, akamsajili kwa kitita cha euro 10m.


Baada ya kumsajili, Zidane alinukuliwa akisema: “Ni wa kipekee na haikuwa rahisi kumpata.”


Miaka nane ndani ya Madrid, Varane amekuwa msaada mkubwa katika safu ya ulinzi na amekuwa beki bora akicheza sambamba na mkongwe Sergio Ramos.



Fede Valverde
Kiungo huyu alijiunga na Real Madrid na kuanzia timu ya vijana.


Baadaye akatengenezwa vizuri na hivi sasa ni msaada mkubwa ndani ya timu hiyo.


Kumbuka msimu uliopita, Zidane alitaka kumsajili Paul Pogba, lakini ikashindikana.


Akaamua kumtumia Fede ambaye hajamuangusha kwani amekuwa na msaada kwenye kikosi cha Madrid.


Zidane amekuwa akimpenda sana kiungo huyu, anampa nafasi kubwa mbele ya Toni Kroos, Casemiro na Luka Modric.


Fede ameibadilisha Madrid msimu huu hasa katika safu ya kiungo hii ni kutokana na uwezo wake ambao Zidane aliwahi kukiri kuwa pale anapokosekana, timu inayumba.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic