HABARI njema
kwa wapenda soka Ujerumani na duniani kote ni kwamba, Ligi Kuu ya Uejrumani
maarufu Bundesliga inarejea na mechi zake zinatarajiwa kuchezwa katikati ya
mwezi huu.
Hatua hiyo
imekuja baada ya Serikali ya Ujerumani kutangaza sasa ligi zinaweza kurudi kuchezwa
nchini humo.
Bundesliga
ilisimama katikati ya Machi, mwaka huu baada ya kusambaa kwa kasi virusi vya
corona ambavyo kwa Ujerumani vimeathiri zaidi ya watu 150,000, huku takribani
watu 6,300 wakifariki nchini humo.
Tangu kuwepo
kwa corona, Bundesliga inakuwa ligi ya kwanza Ulaya kurudi kuchezwa, huku
Uholanzi na Ufaransa wenyewe wakimaliza ligi zao za msimu huu.
Kesho Alhamisi,
kikao cha Bundesliga kitafanyika kwenye Mji wa Frankfurt kuangalia hali ya afya
itakuwaje, huku pia kukipangwa tarehe rasmi ya kuendelea kwa msimu huo.
Wakati Bundesliga
inasimama, klabu nyingi zilikuwa zimebakiwa na mechi takribani tisa kumaliza
msimu huu, huku Eintracht Frankfurt na Werder Bremen zikibakiwa na mechi kumi
kila moja.
Vinara Bayern
Munich wamewaacha Borussia Dortmund kwa pointi nne.
Lakini ligi
hiyo itarudi ikiwa chini ya uangalizi maalum kutokana na hivi karibuni Klabu ya
FC Cologne kuripoti kuwa na wagonjwa watatu wa corona.
0 COMMENTS:
Post a Comment