July 25, 2020


KESHO Jumapili, msimu wa Ligi Kuu Bara 2019/20 unatarajiwa kufikia tamati ambapo tutashuhudia mechi kumi zikichezwa huku timu 20 zikichuana vikali.

Tayari bingwa anajulikana ni Simba na wamekabidhiwa kombe lao muda tu. Kama umesahau, nikukumbushe kwamba baada ya kucheza na Namungo kule mkoani Lindi ndiyo walikabidhiwa kombe.

Vita kubwa iliyobaki sasa ni katika kupambana na janga la kushuka daraja ambapo huko vita yake si ya kitoto kabisa.

Ikiwa tayari Singida United imeshuka daraja rasmi kabla ya ligi kumalizika, zimebaki timu takribani saba ambazo zinapambana zisishuke daraja.

Kuanzia timu ya nafasi ya 13 hadi 19, ndizo zinapambana na janga hilo kwa sasa. Kumbuka timu zinazotakiwa kushuka daraja moja kwa moja ni nne. Singida tayari, bado zingine tatu.

Lakini kuna zingine mbili zitalazimika kucheza mechi za mtoano ‘playoffs’ ili kupambania nafasi zao za kubaki ligi kuu. Zitacheza dhidi ya Ihefu SC na Geita Gold.

Ngoja nikufahamishe kitu hapa kabla sijaenda mbali zaidi. Timu zitakazoshika nafasi ya 17, 18, 19 na 20 ndizo zitashuka daraja moja kwa moja, kisha zile za nafasi ya 15 na 16 ndizo zitacheza mechi za mtoano.

Ukitazama msimamo ulivyo mpaka sasa wakati timu zote zikiwa zimecheza mechi 37, Mbeya City, Alliance, Ndanda na Singida, ndizo zinashika nafasi nne za chini, huku Mbao na Mtibwa zikiwa nafasi ya kucheza mechi za mtoano.

Kuwa nafasi hizo kwa sasa haimaanishi kwamba ndiyo tayari kazi imeisha kwao, bali wanaweza kubadili upepo kulingana na matokeo ya mwisho hapo kesho.

Ndanda ina pointi 41, Alliance sawa na Mbeya City, Mbao na Mtibwa. Pia Mwadui ina 44 kama ilivyo kwa Lipuli.

Mwenye pointi 41, akishinda mechi ya mwisho anafikisha 44, yule mwenye 44 akipoteza mechi ya mwisho, wanakuwa sawa, hapo ishu ya tofauti ya mabao itaamua.

Kwa manaa hiyo ni kwamba, vita yao ni kubwa sana. Hapa lazima jambo lifanyike kipindi hiki msimu unamalizika.

Mamlaka husika kwa maana ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), zinapaswa kuwa na jicho la tatu katika mechi hizi za mwisho.

Suala la upangaji matokeo hatutaki kuliona wala kusikia limetokea kesho wakati msimu unamalizika.

Zibeni mianya yote ya rushwa ili kila timu iweze kupata matokeo kulingana na ilivyojiandaa. Haitapendeza kusikia timu fulani imebebwa na nyingine kunyimwa haki yake.

Siku zote dhuluma si jambo zuri, timu itakayotumia njia zisizo sahihi katika kutafuta matokeo, itakuja kuhukumiwa huko mbele. Pengine isihukumiwe na mamlaka husika, lakini inaweza kuhukumiwa uwanjani kwa maana ya kupata matokeo mabovu msimu ujao.

Yote kwa yote, nizipongeze timu zote 20 zilizoshiriki Ligi Kuu Bara msimu huu kwani zimeonesha ushindani mkubwa hadi sasa tunakwenda kumaliza msimu, ni timu moja tu ndiyo imeshuka daraja.

Kuna ligi zingine huko utakuta ligi inaendelea ikiwa imebaki mechi tatu au nne, lakini tayari kuna timu zaidi ya moja tayari zimeshuka. Kwetu imekuwa tofauti msimu huu.

Nikiwa namalizia, pia nizikumbushe timu ambazo zitashiriki ligi hiyo msimu ujao kujipanga kisawasawa, kama katika ishu ya kushuka tumesubiri hadi mwisho, basi na katika kumpata bingwa iwe hivyohivyo

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic