Saleh Ally
MOJA ya
mambo yanayouangusha mchezo wa mpira nchini ni unafiki wa wadau wake
wanaouzunguka.
Watu
hawafanyi mambo kwa maslahi ya mpira wenyewe, wanafanya kila jambo kwa ajili
yao, hali inayowafanya kuwa wanafiki kwa mambo mengi sana.
Wanasingiziana
mambo, wanajengeana uadui, wanatumia visingizio vya ushabiki kuwaumiza au
kuwasemea wengine mambo mabaya na haya mengi yanaendelea chinichini ndani ya
mpira wa Tanzania.
Kitu kibaya
zaidi ni wachache sana wanaoweza kusema ukweli na kuyazungumzia matatizo ya
wanadamu hawa ambao ni wadau wa soka kwamba yanaukabili mchezo huu na inapaswa
kubadilika.
Rais wa
Awamu ya Tano, John Joseph Pombe Magufuli, ndiye pekee ambaye alikuwa chachu na
akaweza kusema maneno mengi ya wazi na ukweli kama kiongozi.
Pamoja na
kwamba ilikuwa ni mara ya kwanza anahudhuria katika mechi ya mchezo wa soka
kama kiongozi mkuu wa nchi, Magufuli aliendelea kuonyesha kwamba yeye si mtu wa
kubabaisha mambo na kama ni kusema ukweli, basi ni ukweli moja kwa moja bila ya
kuhofia wala kuingiza siasa.
Ninaamini
leo, Simba wanaishi na wanafanikiwa kupitia maneno ya Magufuli ambayo
aliwaambia kuhusiana na ubora na namna ambavyo timu zimekuwa zikitolewa katika
michuano mikubwa hasa ya Afrika.
Magufuli
aliwaeleza Simba wakifungwa na Kagera Sugar bao 1-0 wakati tayari wakiwa
mabingwa wa Ligi Kuu Bara. Aliwaeleza wazi akisisitiza “Kwa kiwango hiki
hamtafika popote.”
Aliwaambia
anataka kombe la Afrika, akawaambia Simba kwamba amewaheshimu kwenda Uwanja wa
Taifa wakati huo kuwakabidhi kombe la ubingwa wa Ligi Kuu Bara. Lakini
anatamani ubingwa wa Afrika na kuwataka Simba wawe wa kwanza kuuleta Tanzania.
Haya maneno ni dawa ndani ya mioyo ya wachezaji, viongozi na hata mashabiki wa
Simba.
Wanajua nini
kinatakiwa sasa, wanajua inawezekana hata kama ilionekana haitawezekana au ni
ngumu. Wanaelewa kwamba wao si wa kushindwa na hii inakuwa na mchango mkubwa
hata katika mwendo wa Simba kwa sasa.
Tunaona
mwendo wa Simba katika Ligi ya Mabingwa Afrika leo. Baada ya mechi nne za hatua
ya makundi, hawajafungwa hata bao moja. Wakati misimu miwili iliyopita,
walifungwa mabao 13 katika mechi tatu za ugenini.
Simba
wamejifunza mengi kwa njia zao lakini somo la Magufuli limeendelea kuwa sehemu
ya mabadiliko yao na huenda litawasaidia na wengine watapata nafasi ya
kujifunza kwa kuwa sauti yake itaendelea kuishi.
Rais
Magufuli hakuwa na uoga wa zile tabia za kinafiki za kutaka kuwafurahisha Simba
na ukumbuke siku hiyo Simba walikuwa wengi uwanjani lakini akawaeleza ukweli
bin haki kuhusiana na uhalisia.
Alieleza kwa
nini hana timu Simba au Yanga, alisema ni kutokana na timu za Tanzania
kutofanya vizuri au kufungwafungwa tu. Hivyo ikamkatisha tamaa kwa kuwa yeye si
mtu anayependa kushindwa. Maana yake aliyakimbia maumivu ya kushindwa kwa kukaa
mbali na ushabiki wa soka.
Nakumbuka
alisimulia namna alivyokuwa akicheza soka shuleni, alikuwa fowadi, baadaye
akaamua kuwa kipa lakini akaacha baada ya kulazimika kuvaa miwani akiona
kutakuwa na ugumu kwake katika suala la uvaaji miwani wakati akidaka. Maana
yake kweli alikuwa mwanamichezo ambaye baadaye maumivu ya kufeli, yalimkimbiza.
Magufuli
ameondoka mapema, angekuwa dawa ya kudumu katika michezo nchini kwa ukweli
wake, kutokuwa muoga wala unafiki wa wanamichezo kulikuwa msaada mkubwa kwa
michezo nchini.
Angalia
vyama vingi au mashirikisho ya soka, kuna mambo yamebadilika katika masuala ya
uongozi au utendaji yamebadilika kabisa. Maana watu wamekuwa waoga na mwenendo
wa maisha ya Magufuli yalivyokuwa kuhusiana na uongozi.
Hakuna
anayeweza kupinga kwamba tumejifunza mengi sana na uwepo wake. Wakati mwingine
Magufuli kuwepo kwake tu kulikuwa kunabadilisha mambo.
Wale ambao
hawakuwa na uoga wa mali za umma au hofu ya kufuja mali za Watanzania, hii
imekuwa ni kama kitu cha kawaida lakini wakati wake mambo yalibadiliika na watu
wakawa waoga na faida ya mali za umma kwa umma wenyewe zikaanza kuonekana.
Tumejifunza
mengi kutokana na muda wa Magufuli takribani miaka sita na michezo imefaidika
lazima tukubali na tuseme ahsante sana Mungu na baada ya hapo tuendelee
kumuombea kama sehemu ya shukurani kwake Mungu.








0 COMMENTS:
Post a Comment