*Afunguka
kila kitu kuhusu usajili, awataja adui wa Simba
Na Saleh Ally
BAADA ya maneno mengi, hatimaye aliyekuwa Kocha
Mkuu wa Simba, Milovan Cirkovic amebeba mabegi yake na kurejea kwao Serbia
akiwa rasmi ameachana na mabingwa hao wa Tanzania Bara.
Milovan ndiye aliyewapa Simba ubingwa, dalili
zinaonyesha msimu huu si wao. Ameondoka baada ya kulipwa fedha zake na Mlezi wa
Simba, Rahma Al Kharusi ‘Malkia wa Nyuki’ ambaye alijitolea kulimaliza tatizo
hilo.
Milovan, baba wa watoto watatu, Sarah, Ana na
Malta, alikuwa anaidai Simba mishahara minne, jumla ni dola 32,000 (Sh milioni
51.8), ingawa Malkia wa Nyuki alimlipa dola 35,000 ili amalize na matatizo yake
mengine kama hoteli na tiketi ya ndege.
Jumatano saa nane na nusu usiku, wakati Milovan
akiwa njiani kwenda Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA),
Championi Ijumaa lilifanya mahojiano naye ambayo yalikuwa ya mwisho akiwa
katika ardhi ya Tanzania.
Milovan anaeleza mambo kadhaa kuhusiana na hali
ilivyo huku akisisitiza kuna viongozi na wadau wa Simba ambao wamekuwa
wakifanya juhudi kumchafua, kitu anachoamini si sahihi kwa kuwa yeye hakuwa
adui wa Simba, badala yake wao ndiyo tatizo kubwa.
“Lengo langu si kumshambulia mtu, lakini nakuhakikishia
Simba haitatulia, kuna matatizo mengi na viongozi ndiyo chanzo. Leo
ninazungumza hapa, lakini baadaye nitakaa kimya na kuacha ukweli uonekane,
baada ya muda utaonekana tu.
“Hapa mwisho, nilifanya kazi katika mazingira
magumu sana Simba, uongozi uliachia matundu mengi, ikawa rahisi kila mtu
kuingia na kuzungumza anachotaka au kukufundisha bila kujali wewe ni kocha,”
anasema Milovan na kuendelea kuelezea mambo kadhaa.
Vijana:
Mimi ndiye nilikuwa wa kwanza kuchukua uamuzi wa
kuwapa wachezaji makinda nafasi, nakumbuka nilikutana na upinzani mkali,
ilionekana hawataweza. Lakini nilishikilia msimamo, ninashukuru vijana
hawakuniangusha, walicheza vizuri.
Baadaye, siku ninapoamua kuwaweka benchi kutokana
na ninavyoiona mechi ilivyo mbele yetu, utashangaa kiongozi analaumu eti siwapangi,
tena anakasirika kabisa. Lakini kiongozi huyu ndiye alikasirika sana baada ya
mimi kuanza kuwapa nafasi hadi kufikia kusema ninawaharibia timu.
Wenye
fedha:
Wenye fedha ni muhimu sana katika klabu au
uhamasishaji wa timu, lakini baadaye waligeuka na kuwa tatizo. Kuna huyu jamaa
anayependa kuvaa kofia kubwa, awali nilijua ni mtu mzuri sana.
Lakini alinishangaza sana, kila mechi alianza
kunifundisha wakati wa mapumziko. Alitaka nipange wachezaji kwa mfumo wake.
Kweli hiyo ilinishangaza sana, nimeisomea chuoni kazi hii kwa miaka kumi na
moja.
Jiulize, mtu ambaye anaona tu pale uwanjani au
kwa kuwa mara nyingi anakwenda uwanjani, anaamini anajua kuliko wewe. Bora
angeshauri na si kukufundisha au kuamrisha, niligundua tatizo moja, kwamba kwa
kuwa wana fedha, basi wanaamini wanajua kila kitu. Hilo ni tatizo kubwa sana la
Simba.
Kaseja
hatarini:
Watu haohao wenye fedha ndiyo wamekuwa wanaharibu
mambo mengi, mfano kushinikiza mchezaji acheze wakati kocha unamuona hajawa
tayari na inapotokea akashindwa kufanya vizuri, wanageuka na kukuangushia
lawama.
Ninaamini, subiri muda utaeleza kila kitu.
(Juma) Kaseja ambaye mimi ninaamini ni kipa bora
kabisa atakumbana na hali hiyo. Watafikia kushinikiza kipa mgeni (Abel Dhaira)
acheze, lakini likitokea tatizo, watamuangushia mzigo mwingine kabisa, hilo ni
tatizo jingine kubwa.
Ochieng
& Akuffor:
Nilisikia kuna kiongozi mmoja alikuwa akijitahidi
kunichafua kwenye mitandao na vyombo vya habari, mimi nimefanya kazi ya mpira
siku nyingi. Najua nifanye nini, nimesomea hii kazi, siwezi kuwa kama yeye,
ndiyo maana hata jina simtaji, ninajua ninachofanya.
Wanasema mimi niliwasajili kina Daniel Akuffor na
Paschal Ochieng, hiki ni kichekesho kwangu, eti nimeitia Simba hasara, kwa
lipi? Niliporudi nikawakuta, wakaniambia niwaangalie tukiwa Arusha, nikafanya
hivyo na kutoa majibu.
Wale wachezaji si wabaya, nasisitiza si wabaya na
wana uwezo. Lakini inaonekana walikokuwa hawakuwa wakicheza au vinginevyo,
walihitaji muda. Niliwaambia ni wachezaji wazuri ambao wanahitaji muda, wao
walitaka siku mbili wawe wazuri, kitu ambacho hakiwezekani.
Leo matatizo yao, mwisho wakaniangushia mimi
ndiye nilisema wasajiliwe. Mchezaji pekee niliyempendekeza asajiliwe wakati huo
ni (Mrisho) Ngassa, wao hili wanalijua.
Yondani:
Angalia Kelvin (Yondani), aliondoka wakati
tunamhitaji, Simba leo inahangaika sana kwa sababu yake. Ndiye beki bora wa kati
Tanzania, hakuna timu anayoweza kwenda akakosa namba. Anaijua kazi yake, yupo
makini na hana utani hata sekunde moja.
Waliniambia wamemuongezea mkataba, nilisisitiza
kuhusiana na umuhimu wake. Sikutaka kusema moja kwa moja, ila nilianza kuhofia
ataondoka baada ya kusikia haelewani na kiongozi mmoja ambaye kila siku
anakorofishana na wachezaji.
Nikaona bora nisisitize kuhusu kuongezewa
mkataba, wakaniambia kila kitu tayari, nikiwa Serbia nikasikia amejiunga Yanga,
sikuamini.
Tatizo hilo Simba watakaa nalo kwa muda mrefu,
limewatia hasara kubwa mara kumi zaidi ya fedha ambazo wangetoa kumbakiza
Kelvin. Ndiyo maana nasema wanaamini wanajua mambo, kumbe hapana.
Boban &
Nyosso:
Niliingia kwenye matatizo kuhusiana nao, waliniita
tuwajadili katika kipindi ambacho tayari wamewasimamisha, lakini siku ya mwisho
wakasema walinishirikisha, hakikuwa kitu sahihi. Niliposema likawa kosa la jinai.
Hawa ni watu wa ajabu kabisa, Milovan akikosea
walitaka apambane na makosa yake, lakini wakikosea wao, wanataka watu wote
waingie kwenye makosa hayo. Ajabu sana!
Mafisango:
Mimi sikuangalia sana mambo binafsi kama
wanavyofanya wao, nilitaka kazi yangu iende kwa mafanikio. Kama unakumbuka
marehemu Mafisango alinitukana, lakini nilisisitiza abaki, maana tulikuwa
tunamhitaji sana Sudan, hapa niliangalia maslahi ya Simba na Milovan.
Lakini Boban alisimamishwa kwa kuwa alizozana na
mtu mmoja si kiongozi, lakini huwa ni mtu wa karibu wa Simba na anayetoa
msaada. Akasimamishwa, mimi sikuona sawa kwa kuwa nilikuwa namhitaji, msaada
wake ulikuwa muhimu kwa wakati huo.
Angalia hao watu wenye fedha wanavyopenda
heshima, ukiuliza yeye ni nani hadi Boban anasimamishwa, haupati jibu. Lakini
siku ya mwisho wanasisitiza tulishiriki wote, pia nilipohoji nikaonekana ni
adui. Wangekuwa wazalendo kwa Simba, wangeangalia maslahi ya timu kama
nilivyofanya kwa Mafisango.
Hata iwe vipi, lazima viongozi na watu wa karibu wa
Simba wakubali, kama wanampa kocha kazi, basi wamuache afundishe na kufanya
kazi yake kwa ufasaha, wasiingilie anachokifanya, wasimshinikize, huo si
weledi.
Kuna mengi nimeyaona Simba, lakini wao ndiyo
wananifanya niseme leo kwa kuwa wanadanganya umma. Nilichoamua nikifika Serbia,
nitapumzika, nitaacha kuzungumzia Simba ili angalau niisahau kwa kuwa
inaniumiza ninapoikumbuka. Lakini wakizidi kunisakama, nitamtaja mmoja baada ya
mwingine na madhambi yao.
SOURCE: CHAMPIONI SPORTS NEWSPAPER..
0 COMMENTS:
Post a Comment