May 22, 2013



 
Na Saleh Ally
WAKATI Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Osmund Mbilinyi alipokuwa akichangia makadirio ya bajeti ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo bungeni, kuna mambo kadhaa aligusia kuhusiana na wasanii.
Mbiliyingi maarufu kama Sugu kwa watu wa sanaa, alikuwa mkali katika mambo kadhaa na ilionyesha wazi alilenga kuwasaidia wasanii ambao wamekuwa wakitesema kutokana na jasho lao kwenda mikononi mwa wajanja wachache.

Pamoja na kuonyesha nia ya dhati, Sugu alizungumza maneno mawili ambayo yalibaki yakizunguka kichwani mwangu na kunikumbusha mambo mengi niliyopitia katika harakati ambazo Sugu ameziendeleza bila ya kuchoka.

Katika changia hiyo, Sugu alisema wasanii wengi ni waoga, waache unafiki na kutetea maslahi yao, kitu cha pili akasisitiza suala la umoja kwamba hakuna umoja kati yao.

Wakati anasisitiza umoja, alisisitiza kwa kusema: “Anachokililia Lady Jaydee leo ndicho Vinega walikuwa wanakipigania miaka yote. Wakati fulani ilifikia watu wakasema tunahongwa ili kufanya hivyo, lakini kikubwa kwetu ilikuwa ni kudai haki zetu.”

Kuna watu wengi sana duniani, kama ilivyo kwa wasanii lakini mara kadhaa ili kukamilika kuwa msanii, kuweza kupiga gitaa na kuimba pekee hakutoshi hata kidogo.

Suala la kutetea haki zako ni muhimu, lakini kwa kuwa msanii anaingia katika kundi la wasanii, lazima kuwe na umoja ili kulifanya kundi hilo liwe na nguvu na kuweza kupambana kama timu na kama ni vita, basi washinde pamoja.


Vita ya wasanii imekuwa ni sawa na mapambano ya walishika mitutu ya bunduki, wengine wakiwa wamejaza matenga ya nyanya ambazo wanazitumia kama risasi kuwaponda wengine ili kutaka kupata haki zao.
Wasanii wengi ni wanafiki, wabinafsi kupita kiasi na siku zote wamekuwa wakiifanya vita ya wasanii dhidi ya wanaolalamikiwa iwe laini sana kwa kuwa wengi wao hawafanani kati ya sura na mioyo yao.

Jiulize, wasanii wangapi wanaweza kusimama na kumtetea mwingine hata tatizo linalozungumziwa halimhusu yeye, angalau amesikia mwenzake ana tatizo. Asilimia kubwa wamekuwa wakifurahia matatizo ya wasanii wenzao.
Kufeli kwa msanii mmoja ni faraja kwa msanii mwingine, hiyo inakuwa inatoka moyoni, lakini kama wakitulia, usoni wanaonekana tofauti na kusisitiza kwamba wanataka haki za wasanii.

Nimesema mara kadhaa, wasanii wengi hawatetei haki za wasanii hadi wanapoguswa na kusikia uchungu. Wengi wao ‘wananunulika’ kwa ulahisi sana. Naweza kusema hivi, wenye uchungu na fani yao ni wachache kuliko wasaliti.

Ndiyo maana nayachukua maneno haya mawili ya Sugu, unafiki na wasio na umoja. Ninasema hivi kwa kuwa nina ushahidi, nakumbuka mwaka 2003, nilishiriki katika kampeni za kusaidia kuunda umoja wa wasanii zilizokuwa zinaongozwa na Innocent Nganyagwa na Mr II au  2 Proud.

Wakati huo nilijifunza mambo mengi sana ya wasanii, pamoja na kuandaliwa mikutano kadhaa, lakini karibu kila mkutano ulikuwa haufikishi zaidi ya wasanii nane wakati waliokuwa wanaahidi kuja kwa midomo yao walikuwa zaidi ya 40.

Mwisho Nganyagwa na 2 Proud mnayemuita Sugu sasa, wakakata tamaa na kuamua kuendelea na hamsini zao. Lakini siku chache kati ya wasanii ambao walikuwa hawaonekani katika vikao hivyo, akalaumu kwenye vyombo vya habari kwamba wasanii hawana ushirikiano.

Nimejifunza mengi sana katika kuripoti kwangu kuhusiana na muziki, nilianza kuripoti muziki tokea mwaka 1996 nikiwa shuleni. Tokea wakati huo katika gazeti la Msanii Afrika, ninachokiona mbele yangu ni nguo yenye matobo ambayo wasanii wanajaribu kuitumia kujifunika kuepuka baridi.

Haitawezekana hata siku moja kwa kwa mmoja mmoja. Ushirikiano ndiyo ungewawezesha wasanii kuwa na nguvu ya pamoja na kuweza kupambana. Lakini kinachotokea ni wasaliti ndani ya chumba cha mapambano dhidi ya maadui.

Unafiki ndiyo sifa kubwa ya wasanii wengi wa Tanzania, wakiwemo wale wanaotaka kuficha sura zao kwenye sura ya uungwana na kuidanya jamii, eti wanaonewa na wao wanapewa sapoti kubwa sana kwa jamii.

Wanasema hivyo kwa kuwa wameumizwa wao, hawajajali vipi sanaa wanayoitumikia imeumia. Kibaya zaidi, walishindwa kuitetea sanaa ilivyoumia, wakiumia wao, wanataka iwe vita ya sanaa yote kuwatete,a kitu ambacho nakiona ni upuuzi mkubwa.

Sitaki kuwataja kwa majina, ila nawakumbusha wasanii kibao ambao mliwahi kusema Sugu ameisha ndiyo maana anapiga kelele tu. Leo mnaomuona shujaa na kutafuta urafiki tena, mbaya zaidi katika umri mdogo mlionao, albamu na nyimbo chache na hata umaarufu wa siku chache, nyie ndiyo mmeisha kabisa!

Wasanii mnapaswa kujiangalia upya, wanapaswa kutafuta rekodi na kutathimini upya kwamba bado haitoshi kujificha katika kivuli cha Sugu ambaye amekwenda katika njia yake, hata waliomchukia na kumsema vibaya leo wamerudi upande wake.

Hebu jaribuni angalau wasanii kumi tu kuwa wakweli na wapambanaji kama Sugu muone kama hakutakuwa na mabadiliko. Sisemi muwe maadui wa adui zenu, ikiwa hivyo hakutakuwa na mafanikio katika mnachokitaka.
Ninachosisitiza, mpambane kwa ajili ya maslahi ya sanaa yenu ambayo itakuwa ndiyo mafanikio yenu na mabadiliko yatapatikana. 

Lakini nisisitize, mnakosea sana kupendana machoni na mioyo yenu imejaa roho ya kutu, hamtaki maendeleo ya wenzenu mkiwa mmesahau kuwa kama kuna mtu anaendelea, maana yake anakupa changamoto na wewe kujipanga na kufikiria kupambana ndiyo njia sahihi ya kuleta maendeleo.

Mnataka wengi wawe waoga, wasio na uwezo wa kupambana na kufanikiwa. Lakini ajabu, mnataka tasnia ya muziki iwe imara na inayoheshimika. Kwa kuwa ninawajua, kwangu nawaona sawa na paka anayewinda samaki wa mapambo aliye ndani ya kioo, akiamini atamkamata na kupunguza njaa yake. 

NINAAMINI, WASANII NDIYO JAMII INAYOSIKILIZWA ZAIDI NA JAMII, HIVYO MKIUNDA UMOJA WA DHATI KILA KITU CHENU KITASIKIKA KWA ULAHISI ZAIDI, LAKINI MKIENDELEA NA UNAFIKI KAMA ILIVYO SASA. MTAENDELEA KULALAMA HADI MWISHO WA DUNIA.

1 COMMENTS:

  1. makala nzuri sanaa tenaa sanaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa uwiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii wasanii wengi nuwanafiki na waoga wanapambana leo na kujidai wapo na sugu sababu hawana tena pakukimbilia makala ninzuri uwiiiiiiiiiiiiiiiii nzurii sanaaa

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic