July 15, 2013



Na Saleh Ally
Niliwaona mashabiki kadhaa wa timu ya taifa kutoka upande wa jukwaa la Yanga wakizomea kwa juhudi kubwa wakati wachezaji wa Taifa Stars wakitoka uwanjani kwenda vyumbani.

Wachezaji hao walikuwa wanaingia vyumbani vichwa chini mara baada ya kupata kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa wageni wao Uganda ‘The Cranes’ katika mechi hiyo muhimu sana.

Mechi hiyo ya kuwania kucheza fainali za Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (Chan) nchini Afrika Kusini ilichezwa juzi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na matarajio ya wengi, nikiwemo mimi ilikuwa ni kuiona Stars ikiibuka na ushindi.

Nilitamani sana kuiona Stars ikishinda mechi hiyo, lakini bado niliamini hata baada ya ushindi majibu sahihi yangepatikana katika mechi ya marudiano mjini Kampala wakati Uganda itakapokuwa nyumbani.


Kufungwa kwa Stars kumeonyesha kuwakatisha tamaa watu wengi waliokwenda uwanjani hasa kwa kuwa walikuwa na matumaini makubwa na kikosi cha Stars chini ya Kim Poulsen ambacho kimekuwa kikionyesha soka la uhakika.

Ndiyo maana wengine wakaona uamuzi sahihi ni kuwazomea wachezaji hao, kwangu naona hapana na hata kama walituudhi Watanzania, sidhani kama ni sahihi kuwashambulia wanajeshi wako wakati wakiwa vitani.

Ikumbukwe kwamba Stars ilitakiwa icheze mechi mbili, moja ni hiyo ambayo imechezwa Dar es Salaam, halafu ipo ya pili mjini Kampala ambayo Uganda watakuwa wenyeji.

Stars wamepoteza wakiwa wenyeji, mimi ninaamini hata Uganda wanaweza kupoteza, lakini kama wachezaji wa Stars, benchi la ufundi na wanaowaandaa wataamini hivyo.

Majibu ya kama Stars imefuzu au la hayajapatikana, kuwashambulia sasa si sahihi na si ushabiki unaolenga kujenga na kusaidia. Hadi wachezaji hao wanajenga imani kubwa kwa mashabiki maana yake walifanya kazi vizuri.

Kuwazomea wakati wana jukumu mbele, la kulitetea taifa letu ni sawa na kujishambulia sisi wenyewe kwa kuwa tunazidi kuwavunja nguvu hata kabla mapambano hayajafikia tamati. Sikubaliani na waliojishambulia kama Watanzania, naona wana haraka.

Bado niko katika kundi la kuamini soka ndiyo mchezo wenye matokeo yasiyotabirika kirahisi na Stars bado ina nafasi ya kusonga mbele, hasa kama itaamua kwa dhati.

Kwa sasa mjadala ni Stars itafanya nini kushinda mechi ijayo na ikiwezekana kusonga mbele, lakini pia kujiuliza iliteleza wapi katika mechi ya juzi hadi kushindwa kuonyesha kiwango chao kilichozoeleka, kiasi cha kufungwa bao 1-0 dhidi ya Uganda.

Baada ya hapo, kocha Poulsen na cwachezaji wake wakae na kuyafanyia kazi matatizo ambayo yalikuwa chanzo cha wao kushindwa katika mechi hiyo na kuyapatia majibu. Wafanye mazoezi vizuri halafu wakapambane ugenini na inawezekana kabisa wakashinda na kusonga mbele.

Hadi sasa Stars wako nusu ya safari na bado njia ya wao kwenda Chan haijafungwa kwa kuwa wana dakika 90 muhimu mbele yao na zinawezekana kutumika kuipeleka Tanzania Afrika Kusini na hilo ni jukumu lao kama wawakilishi wa nchi.

Waliowazomea ni Watanzania wenye uchungu na nchi yao, inawezekana walishindwa kuzuia hasira zao. Wao hawapaswi kuweka hayo akilini mwao kama hoja ya msingi, badala yake nini kifanyike katika mechi ya pili ili Stars isonge hadi Afrika Kusini ndiyo jambo la msingi zaidi na hoja nzito.

Binafsi bado ninaamini Stars bado ina nafasi ya kufuzu, kikubwa ni kurekebisha makosa na kufanya maandalizi ya kutosha na hasa kujifunza kupitia mechi ya kwanza. Lakini kisaikolojia, ni kuamini kuwa kuishinda Uganda kwao inawezekana na Stars inaweza kwenda Afrika Kusini.

Fin.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic