July 15, 2013



Saleh Ally
Inawezekana wengi wanaweza wakawa wanajiuliza namna ambavyo mshambuliaji Luis Suarez Alberto anavyogombewa.

Suarez anagombewa katika kipindi akiwa na matukio lukuki yanayoonekana kumpeleka katika dimbwi la wachezaji watukutu ambao hakika unaweza kusema hawana nidhamu.


Inakuwaje kama UIaya na kwingineko kulikoendelea kisoka wanasisitiza sana suala la nidhamu halafu kipindi hiki wanamgombea Suarez ambaye nidhamu yake inaonekana hakuna lolote?

Ana matukio mengi ya utovu wa nidhamu kama kuwauma wenzake, akianzia wakati akiwa Uholanzi akiichezea Ajax, lakini akarudia baada ya kumuuma beki Branislav Ivanovic wa Chelsea katika moja ya mechi za Premiership.

Lakini kabla ya hapo, Suarez alihusishwa na matukio kibao likiwemo lile la kuushika mpira kwa makusudi wakati wa mechi ya Kombe la Dunia wakati Uruguay ilipokuwa inaivaa Ghana.

Mwamuzi akaamuru mkwaju wa penalti na Asamoah Gyan akakosa, mwisho Uruguay ikasonga hadi nusu fainali na Suarez akapokelewa kwao kama shujaa.
Kwa mfano wa Suarez inaonyesha kiasi gani Wazungu wanavyoangalia utendaji kwanza, halafu suala la nidhamu linafuatia baada ya hapo.
Wanachoangalia kwa Suarez ni uwezo zaidi, ndiyo maana Arsenal na Real Madrid zimekuwa zikichuana vikali kumpata mshambuliaji huyo Mruguay huku Liverpool ikionyesha kufanya juhudi za kutaka kumbakiza.

Siku chache baada ya Suarez kumuuma Ivanovic, Liverpool ilimpa adhabu lakini ikasisitiza kuendelea kubaki naye na kuweka katika mtandao wake ujumbe uliokuwa unasema hivi: “Suarez si mtu mwenye matatizo na kama analo tatizo ni kwa kuwa hapendi kushindwa, hupenda kufanya lolote ili ashinde.”

HAKUNA KUREMBA:
Timu zote tatu zina kila sababu ya kuchanganyikiwa na utendaji wa Suarez, kwanza ni kati ya wachezaji wachache wanaoonyesha uwezo wa kujituma kwa nguvu sana.

Suarez anacheza tofauti na wachezaji wengi maarufu, wachambuzi wa soka wanamlinganisha na Lionel Messi ambaye hucheza kwa juhudi muda wote na kutaka kushinda.


Angalia anavyocheza Suarez, hakika hakuna ‘kuremba’ na hucheza kwa kujituma mwanzo mwisho.

MGUSA NYAVU:
Alijiunga na Liverpool, Januari 2011 akiwa ametoka kutikisa katika Kombe la Dunia lililofanyika nchini Afrika Kusini.

Suarez alikuwa ameonyesha kuwa yeye ni mchezaji tofauti katika Kombe la Dunia, lakini kabla ya hapo rekodi yake ya ufungaji akiwa na Ajax katika Ligi ya Uholanzi ilikuwa juu.

Katika msimu huo wa 2009-10, aliweka rekodi ya kufunga mabao 49 katika mechi 48. Ilikuwa kubwa na ambayo inaweza kumuweka mchezaji katika kiwango cha kuitwa “World Class Player”.

PASI ZA MABAO:
Ukiachana na suala la kipaji chake cha kufunga mabao na uwezo mkubwa wa kujituma, Suarez ana kitu cha ziada ambacho timu nyingi sana zinahitaji, pasi zinazozaa mabao.

Mchezaji ambaye anafunga na kutoa pasi zinazozaa mabao kwa wingi ni lulu katika nchi zilizoendelea kisoka. 

Suarez alimaliza muda wake katika Ligi ya Uholanzi akiwa amecheza mechi 159 na kufunga mabao 111. Pia alitoa pasi 37 zilizozaa mabao kwa timu yake na Liverpool hawakuwa na ujanja zaidi ya kumchukua.

MASHUTI:
Suarez anazidi kuwa lulu kwa kuwa katika msimu ulioisha wa Ligi Kuu England, alikuwa kati ya wachezaji wanaowania nafasi ya kuwa mchezaji bora lakini akaharibu mwisho kwa kumuuma Ivanovic.

Pamoja na kuwa na uwezo wa mambo mengi, wastani wa 4.2 wa kupiga mashuti yaliyolenga langoni ulimfanya ashike nafasi ya tatu baada ya Robin van Persie wa Man United aliyekuwa na 4.4 na kinara Wayne Rooney aliyemaliza na 4.7.

Hii ni sehemu ya kuonyesha kwamba Suarez anatosha kuwa mchezaji wa kuwaniwa na timu nyingi kubwa za Ulaya na kila moja inatamani kumpata kwa kuwa ni msaada.

Hadi ligi hiyo ya England maarufu kama Premiership inamalizika, Suarez pia alishika nafasi ya tatu kwa kufunga akiwa na mabao 16, Rooney 17 na kinara van Persie 25.

MAISHA:
Inawezekana Wazungu ni wepesi kuchunguza, wameona Suarez aliyezaliwa miaka 26 iliyopita katika Mji wa Salto nchini Uruguay, alikulia katika mazingira magumu hasa baada ya wazazi wake kutengana akiwa na miaka tisa, ikiwa ni miaka miwili tu baada ya kuhamia katika Jiji la Montevideo.

Wanajua wafanye nini kupata alichonacho kama msaada au faida na vigumu kukipata kwa wengine. Suarez amemuoa mpenzi wake wa siku nyingi aitwaye Sofia Balbi na wamezaa mtoto aitwaye Delfina na inaelezwa maisha katika familia yake yamejaa amani na hakuna utukutu kama anaofanya uwanjani.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic