July 15, 2013




Na Saleh Ally
Mwaka 2010 wakati wa Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini, mtaalamu wa masuala ya penalti, Ignacio Palacios-Huerta, alipewa kazi na timu ya taifa ya Uholanzi kuchambua upigaji penalti wa Wahispania.

Palacios-Huerta ni profesa katika chuo cha masuala ya uchumi jijini London, England. Alipewa kazi hiyo kwa kuwa tangu mwaka 1995 alikuwa amejisomea na kuchambua penalti 9,000.

Baada ya Hispania na Uholanzi kuingia fainali, alianza kuifanya kazi hiyo kwa saa 48. Na alitoa majibu kadhaa kama vile “Fernando Torres kawaida hupiga chini na sababu zake, Xavi na Andrés Iniesta hupiga kulia kwa kipa na sababu zake na mambo mengi zaidi.” Lakini bahati mbaya timu hizo hazikufika kwenye penalti baada ya Iniesta kufunga bao pekee la mchezo huo.

Ukiachana na kazi hiyo aliyopewa Profesa Palacios-Huerta, hadi leo timu ya taifa inayoongoza kufanya kazi na vyuo vikuu katika mechi zake ni Ujerumani.

Chuo Kikuu cha Sporthochschule Cologne ambacho kinaaminika ndiyo chuo kikuu bora cha michezo duniani, kimekuwa kinashirikiana kazi zake na benchi la ufundi la timu ya taifa ya Ujerumani.


Maprofesa na wanafunzi wa chuo hicho wamekuwa wakiandaa ripoti ya kila mechi ambayo inahusu uchezaji wa wachezaji wa timu hiyo, namna wanavyoshambulia na kulinda.

Mfano, katika fainali ya Euro 2012, Ujerumani waliteleza kufuata maelekezo ya namna wanavyolinda katika mechi dhidi ya Hispania na wakapoteza mchezo kwa mabao 2-1. 

Walielezwa namna mabeki wao walivyowapa nafasi ya hadi mita 8 Hispania kupita katikati na katika mchezo mwingine wakarudia kosa, wakaadhibiwa.

Kocha mwenye mafanikio zaidi England, Alex Ferguson, amekuwa akifanya mkutano na wasomi wa Chuo Kikuu cha Manchester mara mbili karibu kila mwaka ili kujua vitu zaidi.

Amekuwa akikutana na wale wanaosoma biashara na michezo na hii imemsaidia kuwa kocha bora.

Hii ni mifano michache ya kuonyesha mchezo wa soka unapiga hatua kubwa tofauti na hapa nyumbani.

Hivi karibuni Simba walianza kuonyesha mfano baada ya kuwalipa maprofesa wa Chuo Kikuu Huria (OUT), wanaoongozwa na Profesa Tolly Mbwette kuandaa mpango mkakati wa kuendesha klabu hiyo kwa zaidi ya miaka 10 ijayo.

Simba wamelipa Sh milioni 15 kwa maprofesa hao, huenda kwa muda huu wakaonekana kuwa hawafanyi lolote ila mafanikio yakawa makubwa hapo baadaye.

Pamoja na juhudi hizo za Simba, suala la kufanya kazi na wataalamu zaidi bado halipewi nafasi, lakini ipo haja ya soka nchini kuangalia mbali zaidi.
Wachezaji wengi hawana takwimu zao za mechi walizocheza lakini ajabu zaidi hata klabu hazijui lolote kuhusiana na takwimu za wachezaji ambazo zingeweza kuwa msaada kwa benchi la ufundi, pia historia ya klabu.

Soka la kitaalamu linazidi kutuacha mbali sana kama hata takwimu tu za wachezaji kwa kila mechi klabu hazina. Ipo haja ya kuajiri wataalamu watakaokuwa wakifanya kazi hizo.
TFF wana wataalamu wao, lakini inaonekana wamekuwa na majukumu mengi zaidi kuliko hata yaliyowapeleka hapo.

Kutumia takwimu kama mchezaji alicheza vipi mechi iliyopita, wiki moja na mwezi mmoja uliopita, ni jambo la msingi sana katika kupiga hatua.
Kwenda kwa kupapasa ni tatizo, lakini kupiga hatua mbele bila ya kuwa na uhakika wa ulichokifanya nyuma pia ni tatizo jingine, tena kubwa.

Iko haja leo wataalamu zaidi waaminiwe katika soka, tena wasiwe wale wataalamu waganga wa kienyeji ambao wamekuwa wakichukua bajeti kubwa katika klabu.

Ukubwa wa klabu hautoshi kwa jina pekee, soka linapiga hatua. Kuwa na makocha bora pekee bado haitoshi, lazima tusome alama za nyakati, hii ni kwa wachezaji na viongozi pia.

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic