Katika hali isiyokuwa ya kawaida, juzi mashabiki wa soka walitaka
kufanya fujo kwenye ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) zilizo chini ya rais
mpya, Jamal Malinzi, kisa kikiwa ni kiingilio kikubwa kwenye Uwanja wa Karume
uliopo Ilala, Dar es Salaam.
Mashabiki hao walitaka kufanya fujo hizo wakati wa mechi ya kujipima
nguvu kati ya Future Taifa Stars dhidi ya Taifa Stars iliyofanyika kwenye
uwanja huo ambapo ndipo ofisi za TFF zilipo.
Kiingilio katika mechi hiyo kilikuwa ni Sh 5,000, hali ambayo
ililalamikiwa na mashabiki hao waliokuwa wanataka kuingia uwanjani kuishuhudia
mechi hiyo, ambapo Malinzi pia alikuwa ni mmoja wa waliohudhuria.
Wengi wa wale waliokuwa wakilalamika, walidai kuwa wamezoea kuingia
uwanjani hapo kwa kiingilio cha Sh 500 au 1,000.
“Haya ndiyo ya uongozi mpya ulioshika hatamu sasa, hapa Karume
kiingilio kinakuwa elfu tano, usishangae kwenye ligi ikapandishwa na kuwa elfu
hamsini,” alihoji shabiki mmoja. Hata hivyo, baada ya vuta-nikuvute ya muda,
mashabiki hao walipoa na kuendelea kubaki nje.
0 COMMENTS:
Post a Comment