Hali ya kiafya ya aliyekuwa kocha wa
makipa wa Simba, James Kisaka, bado siyo nzuri, baada ya kubadilika ghafla.
Kisaka anayesumbuliwa na matatizo ya
kutetemeka kwa miguu na kuvimba kwa jicho lake la kulia, hali yake imebadilika
ambapo sasa miguu yake imepungua nguvu na kumpa tabu zaidi katika kutembea.
Championi Jumatano lilimtembelea Kisaka
ambaye ni kipa wa zamani wa Simba na kumkuta nyumbani kwa kaka yake Msasani
jijini Dar, akiwa hoi huku akiongea kwa tabu ambapo amesema maumivu ya kichwa
yanazidi kuongezeka.
Amesema alikuwa akitumia tiba ya
kutundikiwa maji ‘drip’ ambayo tayari ameshamaliza na sasa anaendelea kutumia
vidonge mbalimbali alivyoandikiwa katika hospitali mbalimbali, ambavyo
vimeshindwa kubadilisha hali yake.
“Hali yangu siyo nzuri, imebadilika kidogo,
juzi ulivyokuja (wiki iliyopita) nilikuwa naweza kutembea kidogo ingawa kwa
kusaidiwa lakini sasa miguu yangu yote imezidi kupungua nguvu na kunipa tabu
katika kutembea, naumwa kwa kweli,” alisema Kisaka kwa uchungu.
“Nilikuwa natumia drip ambazo sasa
zimeshakwisha, naendelea kutumia vile vidonge nilivyoandikiwa, lakini sasa
maumivu ya kichwa nayo yanazidi katika siku mbili hizi, hapa nazungumza na wewe
kwa sababu nakuheshimu sana lakini ingekuwa mtu mwingine ningemuomba aniache,”
alisema Kisaka kwa shida.
SOURCE: CHAMPIONI







0 COMMENTS:
Post a Comment