December 11, 2013





Wasanii watakaoshiriki tamasha la Krismasi litakalofanyika Desemba 25, mwaka huu jijini Dar es Salaam, watamuenzi rais wa kwanza wa Afrika Kusini, marehemu mzee Nelson Mandela kwa kusimama kwa dakika moja kabla ya kuanza kutumbuiza.
 
Mwenyekiti wa kamati ya kuratibu tamasha hilo, Alex Msama, alisema jana kuwa wasanii hao watafanya tukio hilo kutokana na ukweli kwamba Mandela alitoa mchango mkubwa katika kuleta amani ya dunia na hivi leo ulimwengu unashuhudia Afrika Kusini isiyo na machafuko.

“Mandela ni alama ya amani, waimbaji wa Injili wanahusika sana katika kuhubiri amani ya dunia miongoni mwa mataifa. Kwa kutambua ukweli huu, wasanii hao watasimama kimya kwa dakika moja kumuenzi shujaa huyu pamoja na watu wote watakaohudhuria tamasha hilo,” alisema Msama.

Tamasha hilo litakalofanyika katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam litawakutanisha wasanii kama Rose Muhando, Upendo Nkone, Upendo Kilahiro, John Lisu na New Life Band kutoka Tanzania wakati wasanii wa nje ni pamoja na Solly Mahlangu, Liliane Kabaganza, Solomon Mukubwa na Ephraim Sekeleti.  
 
Mzee Mandela alifariki dunia Alhamisi iliyopita akiwa na umri wa miaka 95 nyumbani kwake jijini Johannesburg baada ya kusumbuliwa na maradhi ya mapafu kwa muda mrefu. Anatarajiwa kuzikwa Jumapili hii kijijini kwake Qunu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic