July 16, 2014



Na Saleh Ally
KUNA mzozo mkubwa ikiwa ni siku chache tu baada ya kwisha kwa michuano ya Kombe la Dunia iliyofanyika nchini Brazil na Wajerumani kuibuka na ubingwa kwa kuifunga Argentina kwa bao 1-0 katika muda wa nyongeza.


Ujerumani walistahili, hakuna hata mmoja anayeweza kulalama. Tofauti na tuzo ya mchezaji bora ambaye ameitwaa Lionel Messi, wengi wanapinga hasa kutoka barani Ulaya.

Waingereza ambao timu yao iling’olewa hatua ya makundi, ndiyo wamelivalia njuga, kizuri zaidi hawasemi alistahili kuibeba Wayne Rooney lakini wanasisitiza kwamba angalau Toni Kroos, kiungo maestro wa Ujerumani au kinda James Rodriguez angeweza kuchukua tuzo hiyo.


Wanaweza kuwa na hoja, lakini lilionekana ni jambo la kupita, badala yake wamelifanya hoja hadi kufikia baadhi ya wachezaji wa Amerika Kusini wakiwemo nyota wa Argentina, nao wamekuwa wakipewa maswali yatakayotimiza wanachotaka Wazungu hao.

Wako wanaosema Arjen Robben wa Uholanzi au Thomas Muller wa Ujerumani ndiyo waliostahili. Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) limejaribu kutoa ufafanuzi lakini ukweli Messi alistahili.

Angalia hii:
Kuanzia mwanzo wa michuano, Messi alionyesha ni nahodha wa ushindi, kiwango cha Argentina hakikuwa kati ya vilivyopewa nafasi ya kuchukua kombe, lakini Messi ndiye alionekana ni uhai.

Akitokea katika hali ya kusuasua kutokana na majeraha yaliyomfanya kutofanya vizuri katika kikosi cha Barcelona msimu uliopita, Messi ndiye alikuwa chagizo la kuipeleka Argentina kwenye fainali Maracana.

Alifunga na kutoa pasi wakati wa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Bosnia and Herzegovina. Mechi dhidi ya Iran wakabana vilivyo, lakini uwezo binafsi akafunga bao pekee na wakapata pointi tatu muhimu, wakavuka hadi 16 bora.

Hatua ya 16 ilikuwa dhidi ya Nigeria, kama unakumbuka, walikuwa 2-2 na mechi ilikuwa ngumu lakini haikuishia hapo, angalia uwezo binafsi wa Messi kukimbia na mpira kwa kasi ya juu na kutoa pasi ya bao kwa Angel Di Maria katika dakika ya 118 iliyozaa ushindi dhidi ya Uswisi na Argentina ikatinga nusu fainali kwa ushindi wa bao 1-0.

Nusu fainali haikuwa lelemama dhidi ya Uholanzi waliokuwa wamekamilika vilivyo, dakika za nyongeza pia hazikusaidia, hivyo wakasonga kwenye mikwaju ya penalti. Usisahau pamoja na kuwapa wakati mgumu mabeki wa Waholanzi hao, Messi alifunga moja ya penalti muhimu zilizoipeleka Argentina fainali wakati wengi waliamini siku hiyo ingelala hata kwa mabao sita.

Fainali pia mambo hayakuwa na tofauti, Ujerumani ilikuwa imeibutua Brazil kwa mabao 7-1. Fainali ilikwenda muda wa nyongeza hadi Mario Gotze alipofunga bao katika dakika ya 113.

Utaona kila mechi Messi alishiriki kikamilifu, hata kama ana mabao manne ya kufunga na anazidiwa mawili na Rodriguez, haikuwa rahisi kumuangusha kutwaa tuzo hiyo.

Muller alikuwa kwenye kikosi cha Ujerumani ambacho hata asingekuwepo nani, kilikuwa bora bado, Messi alikuwa mmoja anayebeba kikosi kizima.

Kwa hali halisi, alistahili hiyo tuzo lakini Wazungu watakuwa wanachukizwa na hilo kwa kuwa alitaka achukue mchezaji kutoka Ulaya na hata ile hali ya kumtetea Rodriguez ni sehemu tu ya kutaka kupatikana kwa msisitizo kwamba Messi hakustahili!

Baada ya Messi aliyeshika nafasi ya pili ni Muller na Robben akachukua ya tatu na utaona, Muller anapewa kwa kuwa timu yake imefika fainali sawa na Messi unapomlinganisha na Rodriguez. Wazungu bana!

KIATU CHA DHAHABU:
James Rodriguez (Colombia)
Bao 6, pasi 2 za mabao

KIATU CHA SILVA:
Thomas Muller (Ujerumani)
Bao 5, pasi 3 za mabao

KIATU CHA SHABA
Neymar
Bao 4, pasi 1 ya bao

GLOVU ZA DHAHABU
Manuel Neuer (Ujerumani)

MCHEZAJI BORA KINDA:
Paul Pogba (Ufaransa)

TUZO YA FIFA YA FAIR PLAY:
Colombia

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic