Kamati
ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imetoa adhabu kwa
watu tisa wakiwemo viongozi, wachezaji na kocha mmoja kwa kupatikana na hatia
ya makosa ya kinidhamu.
Katika
kikao chake kilichofanyika juzi (Februari 3 mwaka huu) jijini Dar es Salaam,
Kamati hiyo imewafungia mwaka mmoja viongozi wawili wa Chama cha Mpira wa Miguu
wa Wanawake Tanzania (TWFA) Mkoa wa Mwanza kwa kuwashawishi wachezaji wa Mwanza
Queens kugomea uamuzi halali.
Sophia
Tigalyoma (Mwenyekiti) na Katibu wake Hawa Bajanguo walitiwa hatiani kwa
kuwashawishi wachezaji kugomea uamuzi wa Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake
ya TFF kutupa rufani yao dhidi ya Kigoma.
Kocha
wa Polisi Tabora, Eliakim Christopher amefungiwa mechi kumi na kupigwa faini ya
sh. 300,000 kwa mujibu wa Kanuni ya 39(2) ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) baada
ya kutiwa hatiani kwa kumtukana refa wakati wa mechi kati ya timu yake na
Panone FC iliyochezwa mjini Moshi.
Wachezaji
wa JKT Oljoro FC, Dihe Makonga, Swaleh Idd Hussein, Ramadhan Mnyambegu na
nahodha Shaibu Nayopa wamefungiwa mechi tatu na faini ya sh. 300,000 kila mmoja
kwa kuzingatia kanuni ya 36(10) ya FDL kutokana na kufanya vurugu kwenye mechi
kati yao na Burkina Faso iliyochezwa mjini Morogoro.
Mtunza
Vifaa (Kit Man) wa JKT Oljoro FC, Eliud Mjarifu amefungiwa miezi sita na
kupigwa faini ya sh. 200,000 kwa kumpiga Kocha wa Burkina Faso, CR Mwakambaya
kwenye mechi kati ya timu hizo iliyofanyika Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
Pia
Mjarifu amepewa onyo kali na kutakiwa kutorudia tena kutenda kosa, kwani hata
mwenendo wake wakati wa shauri hilo ulionyesha utovu wa nidhamu mbele ya
Kamati.
Naye
Mtunza Vifaa wa Rhino Rangers FC, Albert Mbuji amefungiwa miezi sita na faini
ya sh. 200,000 kwa kupatikana na hatia ya kuwatukana na kugomea uamuzi wa
marefa kwenye mechi dhidi ya Polisi Dodoma. Adhabu hizo zimetolewa kwa mujibu
wa kanuni ya 40(2) ya FDL.
Kamati
ilikubaliana na utetezi wa Gunda kuwa, jukumu la timu hiyo lilikuwa mikononi
mwa viongozi wa TWFA Singida, na tayari SIREFA kupitia Kamati yake ya Nidhamu
ilishatoa adhabu kwa viongozi wa timu hiyo kutokana na kitendo hicho.
Nayo
malalamiko ya Polisi Tabora FC kutaka mechi yao dhidi ya Toto Africans FC
irudiwe kwenye uwanja huru (neutral ground) kwa madai ya kuchezeshwa zaidi ya
muda unaotakiwa, na kutokuwepo ulinzi wa kutosha kwenye Uwanja wa CCM Kirumba
jijini Mwanza yamekataliwa.
Pia
Kamati ya Nidhamu imeelekeza malalamiko ya timu za Mwadui FC na Polisi Mara FC
dhidi ya Toto Africans kwa kumchezesha mchezaji Ladislaus Mbogo bila kuonyesha
leseni yake yasikilizwe haraka na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) kwa vile si
ya kinidhamu.
Wakati
huo huo, Kamati ya Nidhamu inaendelea na kikao chake leo (Februari 5 mwaka huu)
kusikiliza malalamiko mengine ya kinidhamu yaliyofikishwa mbele yake.
0 COMMENTS:
Post a Comment