Kikosi cha Yanga kimeijulia janja ya
wapinzani wao FC Platinum ya Zimbabwe katika mchezo wa marudiano wa Kombe la
Shirikisho utakaopigwa wiki mbili zijazo huko Zimbabwe, baada ya kuamua
kuondoka nchini siku tano kabla kwa kile walichosema kuwa hawataki kurudia
makosa ya Wakenya, Sofapaka yaliyowagharimu na kuishia kunyeshewa mvua ya
mabao, huku wakisema watarejea nchini mara tu baada ya mchezo.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Idara ya Habari na
Mawasiliano wa Yanga, Jerry Muro, Yanga itaondoka nchini Machi 29, mwaka huu
ambapo mchezo wao unatarajiwa kupigwa kati ya Aprili 3 na 5.
Muro alitaja sababu mbili za kuwafuata
Wazimbabwe mapema; mosi, umbali mrefu kutoka Mji Mkuu wa Zimbabwe, Harare
kwenda kwenye uwanja utakaotumika, pili ni kutaka kuzoea hali ya hewa.
Muro alisema umbali kutoka Harare kwenda
sehemu yenyewe ni muda wa saa 10, jambo lililowaathiri Wakenya Sofapaka na
kujikuta wakitolewa kwa jumla ya mabao 4-2.
“Sofapaka walikwenda siku moja kabla
ya mchezo, wakidhani kuwa watachezea pale Harare, kumbe haikuwa hivyo.
“Umbali kutoka mji mkuu kwenda Bulawayo ni
saa saba, kisha kuna safari tena ya saa tatu kufika huko mgodini (kwa
Platinum), hivyo walijikuta wakifika saa nane za usiku na kucheza mechi kesho
yake. Kwa hiyo tumechukua tahadhari ili na sisi yasitutokee ya Sofapaka. Pili,
tunataka wachezaji wetu wazoee hali ya hewa ya kule kabla ya mchezo,” alisema
Muro.
Yanga ilitinga hatua ya kwanza kwenye
michuano hiyo baada ya kuiondosha BDF XI ya Botswana kwa jumla ya mabao 3-2.
Wakati huohuo, Muro ametangaza kuwa, wale
wanaotaka kwenda Zimbabwe kwa ajili ya kuipa sapoti Yanga, wanatakiwa
kujiandikisha klabuni na si sehemu nyingine, ambapo ni lazima wawe na hati ya
kusafiria (paspoti) na nauli ya kwenda na kurudi ni laki tatu.
Wakati huohuo, uongozi wa klabu hiyo
umesema kuwa wataondoka nchini Zimbabwe mara tu baada ya kumalizika kwa mechi
hiyo.
“Tutaondoka na kila kitu chetu, hatutaki
kutumia bidhaa zao maana kwenye soka kuna mambo mengi na hasa fitna. Kwa hiyo
kukwepa yote, tumeamua tubebe vyakula vyetu na maji.
“Ndiyo maana tumeamua punde tu baada ya
mchezo, tutaanza safari yetu usiku huohuo baada ya mechi na kurejea nchini
kutokana na mambo kama hayo ya fitna,” alisema Muro.







0 COMMENTS:
Post a Comment