Upendo hauna sehemu fulani, mfano kwenye nyumba
za ibada au ndani ya familia nyumbani kwa fulani, yeye, mke na watoto wake.
Upendo ni nguzo ya mwendo wa maisha kokote kule.
Hata wanyama wanapendana na wanategemeana ili
kuendesha maisha yao kwa amani. Hakuna upendo, basi hakuna amani na ikiwemo
wakati hakuna amani, basi ni unafiki.
Kocha Sylvester Marsh ni mgonjwa, anasumbuliwa
na ugonjwa wa kansa ya koo, nimeelezwa hali yake si nzuri.
Juhudi ya kutaka kumuona nilizozifanya kwa
takribani wiki sasa, zimekwama na nimeelezwa madaktari wamekuwa wakizuia
kumuona kutokana na hali yake.
Nimeelezwa Marsh ni mgonjwa kwa kuwa kula yake
imekuwa ni ya shida, pia kadiri siku zinavyosonga mbele, hata kumeza mate yake
limekuwa ni tatizo, maneno haya nimeelezwa na mmoja wa watu wanaomuuguza.
Najua unamkumbuka Marsh, huyu aliwahi kuwa
kocha msaidizi wa Taifa Stars, Kilimanjaro Stars, pia amefundisha klabu
mbalimbali ikiwemo Azam FC.
Wakati fulani niliwahi kuandika kuhusiana na
msaada kwa Christopher Alex nikisisitiza kwamba wanamichezo wajitokeze
kumsaidia na si kusubiri hadi mambo yaharibike.
Kuna mtu mmoja baada ya kusoma nilichoandika
alisema kwamba Alex ambaye sasa ni marehemu alipaswa kujiandaa mapema ili
wakati akiumwa asitegemee misaada kutoka kwa mwajiri au watu wengine.
Wala sikumlaumu, nikajua hayajamkuta, hajui ya
dunia na anapaswa kujifunza kwa kuwa hajui maana ya upendo.
Si kila anayesaidiwa anakuwa hana, wakati
mwingine ni vema kuonyesha upendo. Kwani wangapi wanachangiwa wakati wao wana
uwezo wa kugharamia harusi zao? Hiyo ni sehemu ya kuonyesha upendo na ndiyo
ubinadamu hasa.
Hatuwezi kuonyeshana upendo watu wanapokuwa na
uwezo wa kusaidia au kuwaona wanafaa wakati wanapokuwa na nguvu zao na wanaweza
kufanya jambo fulani ambalo litawafurahisha.
Mwenyezi Mungu ndiye anayeamua kila kitu,
inapofikia akapitisha mwisho wa yoyote pia hakuna yeyote anayeweza kuzuia hilo,
hili kila mtu analijua.
Pamoja na hivyo, hilo halizuii binadamu
kuonyesha mlijaribu kufanya jambo kwa mpendwa wenu badala ya kusubiri mambo yamekuwa
mabaya, halafu muanze kusema fulani alikuwa mtu mzuri sana na pengo lake
halitazibika hata kidogo.
Kumekuwa na kawaida ya kuwapenda zaidi watu
wanapoondoka. Mara kadhaa, nimekuwa nikitoa mfano huo kuhusiana nami kwamba
huenda wako wengi wanaonilaumu kila siku, hawajawahi hata siku moja kusema
walivutiwa na kazi yangu. Siku nikiondoka hapa duniani, wataongoza kwa kusema
nilijitahidi sana.
Inawezekana kupongezana kwetu ni tatizo, kwa
kuwa kila mmoja huenda alipendelea kupongezwa yeye. Basi hata kusaidiana?
Marsh anaumwa, kocha huyo ana maumivu makali,
jaribu kufikiria iwapo maumivu anayoyapata yangekuwa yako? Ndiyo, inawezekana
kwa kuwa nawe ni mwanadamu kama yeye pia.
Kama mlikuwa mnaona kuna juhudi zinafanyika
katika kupambana kuokoa maisha ya Marsh, mimi naona bado na huenda wachache wanashiriki.
Kama kuna mmoja aliona imeshashindikana, basi
bado tulitakiwa kuonyesha upendo wa kwamba tunapambana kwa ajili yake kwa kuwa
ni mmoja wetu na kinachomuumiza sasa, kinaweza kumkuta yeyote kati yetu kwa
kuwa sote ni binadamu.
Tukubali, bado hatujawa imara linapofikia suala
la upendo. Kawaida rafiki sahihi, utamjua katika kipindi kigumu.
Marafiki wengi watajumuika na wewe wakati wa
furaha, Marsh hana furaha, anaumia, maumivu makali nanyi mumemtenga na kukaa
mbali naye, mnasubiri lini ili muonyeshe majonzi na kumjaza sifa!








0 COMMENTS:
Post a Comment