Na Saleh Ally
BAO alilofungwa kipa Ally Mustapha ‘Barthez’
wa Yanga katika mechi dhidi ya Simba, lilionekana ni kosa la karne kwake,
hakuna aliyejali mfungaji alikuwa mahiri kiasi gani.
Acha wengine waamini Barthez ni mzembe sana!
Lakini bao kama hilo au linalofanana kwa kiasi cha asilimia 80, amefungwa pia kipa
Said Mohammed ‘Nduda’ wa Mtibwa Sugar.
Nakukumbusha aliyemfunga Barthez, ndiye
aliyemfunga kipa huyo wa Mtibwa. Hawa ndiyo makipa wazembe zaidi kwa mwezi huu?
Au mfungaji anapaswa kupongezwa kwa umahiri wa hali ya juu aliouonyesha?
Kila mmoja anaweza kuchagua anavyoona yeye
kulingana na msukumo, uwe wa kishabiki au kitalaamu, ila ukweli Mganda Emmanuel
Okwi ni hatari.
Hawezi kuwa hatari wa maneno, lakini uwezo
mkubwa wa kufunga ambao amekuwa akiuonyesha sasa hauna ubishi.
Si mara moja ameifunga Yanga au timu nyingine
ya Ligi Kuu Bara unayoijua, lakini amefunga mabao mawili yenye kiwango cha juu
kabisa katika kipindi cha siku kumi tu.
Ameonyesha uwezo mkubwa unaotoa majibu kuwa
kiutendaji Okwi ni tofauti na wachezaji wengi wengine wakiwemo wazawa na wale
wa nje.
Okwi ni mbunifu, Okwi ni aina ya wachezaji
wenye kipawa cha juu cha soka. Lakini bado unaweza kumlaumu kwa utukutu.
Ana mambo mengi amekuwa akijadiliwa au
kutotekeleza kile alichoomba au kuahidi kukifanya. Kama kuwahi kurejea lakini
mwisho asifanye hivyo.
Mwisho wa ukweli uko hivi, Okwi ana uwezo
mkubwa ambao unatakiwa kuwa changamoto kwa wachezaji wa nyumbani.
Kweli timu kama Simba, Yanga, Azam FC, Mtibwa
Sugar na nyingine zinawaleta wachezaji bora katika vikosi vyao kwa lengo la
kufanya vyema.
Lakini taifa litafaidika katika maendeleo ya
soka kwa kuwa na wachezaji kutoka nje wenye uwezo wa juu kama Okwi. Wanaotaka
kujifunza, hakika watafaidika.
Bao dhidi ya Yanga, huenda ilikuwa ni rahisi
sana au alibahatisha. Lakini alipofunga dhidi ya Mtibwa Sugar, waliokataa au
walioamini alibahatisha, si rahisi kufungua tena midomo yao kusema jambo hilo.
Binadamu kawaida hatukubali mapema,
inawezekana wako wanaoendelea kukataa licha ya Okwi kufunga dhidi ya Yanga na
akafanya hivyo dhidi ya Mtibwa Sugar.
Pointi sita muhimu kupitia mabao mawili bomba
kabisa. Okwi anahitaji kujivunia ingawa yeye anasisitiza kuwa ameamua kuongeza
mazoezi.
“Lengo langu ni kufunga, nikishindwa basi
nitoe pasi izae bao au niwe na mchango mkubwa kwenye timu kwa kusaidiana na
wenzangu.
“Mambo yote ni Mungu na ndiye ninayemshukuru
sana. Lakini nimepania kusaidiana na wenzangu kuleta mabadiliko Simba,”
alisisitiza.
Mabao:
Okwi ndiye mshambuliaji aliyefunga mabao
mazuri zaidi kwa msimu huu kama utalinganisha yote yaliyofungwa.
Kabla ya mchezo wa jana wa Mbeya City dhidi ya
Mgambo JKT, mabao 223 yalikuwa yamefungwa katika Ligi Kuu Bara ikiwa inaenda
ukingoni. Hadi sasa asilimia 50 ya mabao yake yanaonyesha kipaji na uwezo wa
juu zaidi.
Kiboko ya mabeki:
Simba inapomkosa Okwi, hakuna ubishi nguvu kubwa
inapungua kwa kuwa ndiye tishio la kila ngome inayokutana na Simba.
Huenda anaingia kwenye akili za kila kocha
anayekutana na Simba. Hivyo kufanya kumwekea umakini na wakati mwingine
kuharibu mipango mingine ya kawaida.
Hakuna ngome ambayo imeweza kudhibiti makali
yake kwa asilimia mia. Kwani hata ile inayoongozwa na Nadir Haroub ‘Cannavaro’
na Kelvin Yondani ambao ndiyo viongozi wa ngome ya Taifa Stars, wamemshindwa!
Pasi nzuri:
Mmoja wa wachezaji wanaotoa pasi nzuri za
mwisho zinazozaa mabao ni Okwi, iwe ni pasi ya kawaida au krosi.
Okwi anajua afanye nini katika wakati mwafaka
na mfano mzuri pasi alizompa Danny Sserunkuma katika mabao yake mawili
aliyofunga.
Lakini anajua mpira uende kwa nani katika
wakati upi, hasa timu inapokuwa inashambulia kwa kasi.
Kuipandisha timu:
Anaposhika mpira, hasa kama Simba ilikuwa
inashambuliwa halafu akauchukua yeye, ndiyo kipindi ambacho timu hupanda kwa
kasi zaidi.
Anajua kuipandisha timu kwa kasi, huku akiwa
na uwezo mkubwa wa kumiliki mpira akiwa anawachanganya mabeki kwa kuwa hawajui
atafanya kipi kwa wakati mmoja.
Maana ana uwezo wa kupiga na kufunga, kutoa
pasi ya bao au kuendelea kuumiliki mpira. Hii ni sehemu ya sifa kubwa mno
aliyonayo na huenda asilimia 85 ya wachezaji wanaocheza Ligi Kuu Bara katika
timu 14 wasiwe nayo.
Msumbufu:
Kumekuwa na lawama mara kadhaa kutoka kwa wachezaji
wenzake ambazo zinaonyesha kweli Okwi naye kama binadamu ana matatizo yake.
Moja ni kutoshiriki mazoezi vya kutosha, hali
inayowaudhi wenzake. Kuchelewa mazoezini au kutoonyesha yuko na wenzake pamoja.
Kuaga akachelewa kurudi, ingawa hili
kalirekebisha sana. Kikubwa hapa ni ule msemo wa kuangalia mazuri ya mtu zaidi
kuliko mabaya yake.
Kesi:
Okwi ana kesi ameishtaki Etoile du Sahel kwa
kutompa mshahara wake kwa wakati mwafaka, timu hiyo ya Tunisia nayo imeshtaki
pia.
Hali kadhalika, Yanga imemshtaki, naye pia
kaishtaki. Hii inaonyesha kiasi gani Okwi anavyoongoza kwa kesi.
Hii inaweza kuwa tafsiri mara mbili tofauti.
Mchezaji mtukutu kwa kuwa na kesi lukuki alizoshtaki na kushtakiwa, pia
mchezaji anayezijua haki zake.
Uchungu:
Hata ajiunge na timu gani, Okwi ameonyesha
Simba ni nyumbani. Kwani ndiyo timu anayoichezea kwa kiwango cha juu zaidi
anapokuwa nayo. Unaweza kupima alipokuwa Etoile du Sahel, Yanga na sasa Simba.
Mfano mzuri aliamua kumuacha mkewe na
kuahirisha fungate ili arejee na kuichezea Simba dhidi ya Kagera.
Bado utamuona anavyohangaika uwanjani kuhakikisha
inapata ushindi kila anapokuwa anacheza. Unaweza kujifunza kupitia mazuri au
mabaya yake.







Kaka unamahaba na msimbazi kumshinda hata Kaduguda!
ReplyDelete