Klabu ya
Mbeya City imemwaga kitita cha Sh milioni 6 kwa mkataba wa miezi sita iliosaini
na kipa Juma Kaseja.
Kaseja ametua Mbeya City akiwa mchezaji huru
baada ya kuhitilafiana na Yanga ambayo alijiunga nayo akitokea Simba.
Katika mkataba huo, Mbeya City wamemlipa Kaseja
Sh milioni 6 kama ada ya usajili na tayari mkataba umesainiwa juzi usiku jijini
Dar es Salaam ambapo mshahara wake utakuwa ni Sh milioni moja kwa mwezi, hivyo
kama ukigawa fedha zake za usajili, ukajumlisha na mshahara, thamani yake
itakuwa ni Sh milioni mbili kila mwezi.
“Mshahara utakuwa ni shilingi milioni moja,
unajua Juma ni mchezaji mkongwe, hivyo tumeamua kumpa heshima yake ili
ashirikiane na wenzake vizuri,” kilieleza chanzo kutoka Mbeya City.
“Lengo ni kujiimarisha zaidi, hivyo uongozi
umefikia uamuzi huo na tunaamini atakuwa na mchango mkubwa kutokana na ukongwe
wake.”
Mbeya City imekuwa ni timu ya nne kwa Kaseja
kuichezea katika Ligi Kuu Tanzania Bara, kwani alianza na Moro United, Simba,
Yanga kabla ya kutua City.
0 COMMENTS:
Post a Comment