September 4, 2015


NILIAMUA kusikiliza kwa umakini alichokuwa akikizungumza aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbroad Slaa wakati akiwa ameibuka kwa mara ya kwanza baada ya ukimya wa muda mrefu.


DK Slaa alikaa kimya kwa muda mrefu kabla ya siku hizo chache zilizopita alipoibuka na kuzungumza mengi ambayo naweza kusema hapa si mahali pake.

Wakati akizungumza mengi, yako niliyoshika kwa maana ya kufurahishwa na namna alivyokuwa akijieleza na hasa ile kuonyesha yuko tayari kushikilia anachokiamini.

Dk Slaa amezungumza mengi sana, lakini kuna alilolieleza kwamba “Acha nife, wajukuu zangu watakapochimbua kaburi waone jina langu, watatoa hukumu sahihi.”

Hii ilinifanya nikumbuke mengi sana kuhusiana na michezo ya Tanzania na hasa soka. Najua kuna matatizo mengi hata kwenye netiboli, riadha, ngumi na inaonekana michezo ndiyo kichaka cha wajanjawajanja wengi ambao wanaona huko ndiyo sehemu sahihi ya kujificha.
Ukiona maendeleo ya michezo katika nchi nyingi duniani, utagundua hakuna viongozi sahihi wa soka na hasa wenye mapenzi hasa na michezo husika na wengi ni wale wanaotaka kujiendeleza wao binafsi, au kuzifurahisha nafsi zao na si mapenzi ya dhati ya wanachokitumikia.
Ili kuwa na mafanikio katika kitu fulani, basi mapenzi ya dhati lazima yawepo kwani watu wanatakiwa kufanya chochote kwa dhati na bila mapenzi, basi haitawezekana.
Nitaweka mengi kwa jumla nikianza na soka, angalia namna Yanga na Simba zinavyoishi maisha ya kubahatisha licha ya ukubwa wao kwa kwa maana ya mtaji mkubwa wa jina na wingi wa watu.
Yanga na Simba, hazina hata uwanja wa kufanyia mazoezi, kitu ambacho unaona ni sehemu ya maajabu ya soka kwamba hivi ni kweli viongozi wa Yanga na Simba hawaoni kama timu zao zinahitaji uwanja wa mazoezi?
Kweli unaweza ukaniambia Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji na Rais wa Simba, Evans Aveva hawajui timu zao zinahitaji viwanja na hawajui umuhimu wake? Jibu litakuwa wanajua, lakini vipi hawalifanyii kazi kwa muda wote waliokuwepo hapo.
Si uwanja wa mechi, nazungumzia uwanja wa mazoezi tu. Unafikiri viongozi hao na wengine wa kamati za utendaji hawajui? Ndiyo maana ninarudia ile kauli ya Dk Slaa ya hukumu ya wajukuu zake.

Kweli Aveva na Manji wamewahi kuwaza hivyo kwamba siku moja wataingia kwenye hukumu ya moja ya viongozi wakubwa wa soka walioongoza klabu kubwa na kongwe za Yanga na Simba, lakini zikawa hazina hata viwanja vya mazoezi?

TFF nayo imekuwa ikiingia kwenye migogoro mingi kila kukicha. Migogoro mingine kama ule wa kufungiwa kwa Dk Damas Ndumbaro. Wazi unaonyesha ni ubinafsi, ubabe wa kipuuzi lakini umefanyika. Je, Malinzi na wenzake hawahofii kuhukumiwa baadaye?

Anachokisema Dk Slaa, sina uhakika na ukweli wake lakini nazungumzia kauli hiyo ambayo kwangu inaonyesha angalau ni kiongozi anayeweza kuhofia jambo fulani la uadilifu hadi kufikiria vizazi vijavyo vitamfikiria au kumhukumu vipi hapo baadaye.

Nilitamani viongozi wote wa soka, kuanzia TFF, vyama vyote, klabu kubwa kama Simba na Yanga, ndogo na nyingine changa wawe waoga angalau wafikirie hukumu yao kesho itakuwaje.

Wawe waoga wa kuonekana hawakufanya lolote, wasifikirie leo pekee na wabadilike kwa kuamini Yanga kuifunga Simba au Simba kuifunga Yanga ndiyo mafanikio makubwa.


Lazima tukubali, viongozi wengi wa michezo ndiyo ugonjwa wa maendeleo duni ya michezo na kama hawatabadilika na kufikiria huko mbele watahukumiwa hata na wajukuu zao, basi milele michezo itabaki tulipo na porojo ndiyo zitashika hatamu kama ilivyo sasa huku tukisubiri mafanikio ambayo yatabaki kuwa ndoto isiyofikiwa.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic