Na Saleh Ally
SIKU ikifikia
Kocha Charles Boniface Mkwasa akashindwa kuipa matokeo timu ya taifa, Taifa
Stars, basi bila ya kuchelewa wala woga, nitasema, aachie nafasi.
Lakini sasa ni
wakati mwafaka wa kusema maslahi yake yaangaliwe ili kwa wakati mwingine
tuangalie kama kocha mzalendo na wenzake wazalendo wanaweza kuisaidia timu yetu
ya taifa.
Makocha wageni
waliopita, walikuwa wakilipwa mshahara zaidi ya Sh milioni 10 kwa mwezi.
Aliyeondoka alifikisha hadi Sh milioni 20, lakini hakuwa na lolote.
Hakuna anayeweza
kukataa kwamba Kocha Mart Nooij hakuwa na msaada katika kikosi cha Stars,
alikuwa tatizo na alichangia kuirudisha nyuma kwa kiasi kikubwa.
Nimekuwa
nikisisitiza hili, kwamba TFF ilifanya makosa kumuondoa Kim Poulsen na
kumchukua Nooij ambaye huenda alibebwa na urafiki wake na baadhi ya watu wa TFF
au ni siasa za soka kwa kuwa uongozi mpya ulitaka usafishe kila kitu
kilichokuwa chini ya uongozi uliopita.
Uamuzi wa TFF kwa
kipindi hiki kujaribu kumtumia mzawa na hasa Mkwasa, hakika umekuwa ni katika
wakati mwafaka na kinachotakiwa ni kuuongezea nguvu kwa kuwaongezea maslahi
wahusika.
TFF ilimpa Mkwasa
mkataba mfupi wa miezi mitatu kutaka kuiona kazi yake. Hakika kila mtu sasa
hana wasiwasi, kwa kile ambacho Mkwasa amekionyesha katika mechi zake mbili.
Wakati Stars
ilitwangwa nyumbani mabao matatu na Uganda chini ya Nooij, ikiwa chini ya
Mkwasa ilisafiri kwenda Kampala na kutoka sare ya bao 1-1. Ingawa tulitolewa
kuwania Chan, tofauti ilionekana.
Mechi iliyofuata
ya kuwania kucheza Afcon dhidi ya Nigeria, hakukuwa na matumaini hata kidogo
baada ya kipigo cha mabao 3-0 kutoka kwa Misri, Stars ikiwa ugenini.
Nani alikuwa na
matumaini hata ya sare dhidi ya Nigeria? Nani alikuwa anahisi kuwa Stars
itapata hata pointi moja tu katika mechi zake za Kundi G kuwania kucheza Afcon?
Matumaini yalishazama.
Sasa Stars
inaanza kuinuka angalau kwa sare dhidi ya Nigeria. Lakini kilichowafurahisha
Watanzania wengi ni soka safi, soka la kasi, kazi na kushambulia muda wote.
Kumbe Mkwasa anaweza?
| KIKOSI CHA TAIFA STARS |
Yeye kwa
kushirikiana na benchi lake la ufundi, wamefanya kazi kubwa. Mimi sizungumzii
kishabiki, ndiyo maana nimeanza kwa kusema, siku Mkwasa akikwama, basi nitakuwa
wa kwanza kumuomba aachie nafasi hiyo ya Stars.
Kwa sasa, Mkwasa
na benchi lake la ufundi, yaani wasaidizi wake, pia mshauri wa ufundi, Abdallah
Kibadeni, wanastahili maslahi mazuri.
Nimeishi nao
Uturuki wakati Taifa Stars ikiwa kambini. Walionyesha kiasi gani walivyokuwa na
juhudi kubwa kutaka kuisaidia timu na kufanikisha kazi yao. Walionyesha kiasi
gani walivyokuwa na hofu ya kufeli, walijua wataambiwa wamefeli kwa kuwa ni
wazalendo, hivyo juhudi ya kutaka mafanikio ilikuwa kubwa sana.
Sasa ndiyo wakati
mwafaka, iwahiwe kabla haijafa na kuwapatia maslahi bora ili waiendeleze ili
kuinua morali na heshima ya soka nchini ambayo sasa ni matope kabisa.
Mshahara aliokuwa
analipwa Nooij kutoka kwa Rais Kikwete uko wapi? Vipi Mkwasa aliyeonyesha
matumaini na sasa anafanya vizuri asipewe, wakati Nooij aliyeboronga alikuwa akipewa?
Sitaki kuamini
kwamba kwa kuwa ni Mzungu, kwa kuwa ni mgeni basi inawezekana akalipwa vizuri
zaidi hata kama anavurunda, halafu mzalendo halipwi vizuri hata kama anafanya
vizuri.
Miezi mitatu
aliyopewa na TFF imepita, kaiongoza timu katika mechi mbili na mambo yameenda
poa kabisa. Sasa ni wakati wa kumlipa mshahara ili ikiwezekana aachie kazi yake
Yanga na kuwekeza nguvu zake zote katika kikosi cha taifa.
Ninaamini Rais
Kikwete atasoma makala haya na kulifanyia kazi hili kwamba asiondoke mwezi ujao
kabla mshahara haujamfikia Mkwasa, chonde.
Hakuna sababu ya
sisi watu wa soka kuanza kuandika mabango “Rais Kikwete, Mkwasa unamuachaje?”
Namuomba aupitishe mshahara ufike kwa Mkwasa ambaye sasa anastahili kuupata.
Rais Kikwete hana
tatizo, watu wa wizarani kama wanataka kuleta figisu, basi huu si wakati wake
na wanapaswa kujali uzalendo na thamani ya kazi.
Kama ukivunja
morali aliyonayo Mkwasa kwa kipindi hiki ni rahisi sana kuvunja morali ya wengi
katika timu hiyo. Chonde Rais Kikwete, mpe Mkwasa mshahara wake ili kazi
iendelee vizuri.







0 COMMENTS:
Post a Comment