Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi,amewakomalia wagombea
urais Tanzania kuhakikisha wanaikumbuka michezo hasa soka pindi mmoja wao
atakaposhinda nafasi hiyo.
Kauli hiyo ya Malinzi imeenda moja kwa moja kwa
mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli na Edward Lowassa kutoka
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba
ya Wananchi (Ukawa).
Magufuli na Lowassa ndiyo wenye nguvu ya kisiasa
kwa sasa na kuna uwezekano mkubwa mmoja wao akashinda kiti cha urais.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Malinzi
alisema yeyote atakayeshinda nafasi ya rais anatakiwa kutoa kipaumbele kwa
maendeleo ya soka ili kuifanya Tanzania itambe kimataifa.
“Niwaombe tu wagombea wa urais, Magufuli na
Lowassa kama mmoja wao akifanikiwa kuingia madarakani basi asitusahau wanamichezo
kwani tunahitaji viwanja vya soka kwani vilivyopo ni vichache,” alisema
Malinzi.
“Hata kama wakishindwa kujenga vipya bali vile
vilivyopo wavisimamie kwenye ukarabati kwani kama hilo likifanikiwa naamini
michezo itapiga hatua nchini.”







0 COMMENTS:
Post a Comment