Mshambuliaji Elias Maguri amebakiza miezi sita tu
katika mkataba wake na Stand United, sasa timu yake inapambana kuhakikisha
inamuuza ndani ya muda huo ili asiondoke kama mchezaji huru.
Awali, Stand United baada ya kusikia habari za
Maguri kutakiwa na TP Mazembe, ikakubali kumuuza kwa dola 50,000 ambazo ni
zaidi ya Sh milioni 100, lakini bado kuna kitu kinawachanganya.
Ofisa Habari wa Stand United, Deo Kaji Makomba,
amesema wameona wakizubaa Maguri mwenye mabao
tisa katika Ligi Kuu Bara, anaweza kuondoka bure, hivyo wanatafuta namna ya
kuzipata fedha za usajili wake.
“Tulimsajili Maguri kwa mkataba wa mwaka mmoja,
hivyo baada ya msimu huu atakuwa amemaliza majukumu yake ya kuitumikia timu
yetu na atakuwa huru.
“Tunaangalia jinsi gani ya kufanya ili tuweze
kufaidika naye, kwani hata sisi bado tunahitaji huduma yake, kama itashindikana
basi tumuombee kwa Mungu mipango yake ya kwenda Mazembe ikae sawa katika
kipindi hiki ambacho bado ana mkataba ili na sisi tuweze kufaidika naye,”
alisema Makomba.
TP Mazembe ambayo imetuma maofisa wake Ethiopia
kumtazama Maguri akiichezea Kilimanjaro Stars katika Kombe la Chalenji, inataka
kumsajili straika huyo ili kuziba pengo la Mbwana Samatta anayeondoka klabuni
hapo.
0 COMMENTS:
Post a Comment