Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal
Malinzi ameuandikia barua uongozi wa Lipuli ya Iringa kwa mafanikio ya kupanda
daraja msimu huu kutoka Ligi Daraja la Kwanza hadi Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania
Bara (VPL) msimu wa 2017/18.
Lipuli ya Iringa imepanda daraja baada ya kupita miaka 17
na Rais Malinzi amesema katika barua yake hiyo kwenda kwa Katibu Mkuu wa
Lipuli, akisema: “Nitumie fursa hii kukupongeza wewe, uongozi wa klabu yako,
benchi la ufundi na wadau wote wa timu ya Lipuli kufuatia kupanda daraja kwenda
Ligi Kuu.
“Bila shaka ni kazi kubwa imefanyika ikihusisha kujitolea
kwa ari na mali kuhakikisha mnafika hapa mlipo,” ilisema barua hiyo na
kuongeza: “Rai yangu kwenu ni kuongeza juhudi na kuendesha klabu kwa weledi
mkubwa zaidi ili muweze kuwa washindani wa kweli katika ligi.”
Lipuli iliyokuwa kundi “A” imepanda daraja na kuzipiku timu
za Kiluvya United ya Pwani, Pamba ya Mwanza, African Sports ya Tanga, Polisi
Dar, Ashanti United, Friends Rangers, Mshikamano za Dar es Salaam.
0 COMMENTS:
Post a Comment