February 5, 2017




Na Saleh Ally
MWAKA 2002, wakati Juma Kaseja anaanza kuichezea Simba akitokea Moro United, Kipa Essam Kamal El Hadary tayari alikuwa kipa namba moja wa timu bora kuliko zote Afrika ya Al Ahly.

El Hadary alijiunga na Al Ahly mwaka 1996 baada ya kutamba na Damietta aliyoichezea tangu 1993 hadi 1996, mwaka ambao kwa mara ya kwanza mwandishi Saleh Ally alianza kuwa mwandishi ambaye hajaajiriwa au correspondent au aliyekuwa mafunzoni.

Wakati kipa Juma Kaseja wa Simba anaanza kuonekana “mzee” mwaka 2009, El Hadary alikuwa anamalizana na FC Sion ya Uswisi ambayo alijiunga nayo 2008 na kuamua kurejea tena Misri kujiunga na Ismaily ambayo aliichezea msimu mmoja halafu akajiunga na mahasimu wake hapo, kabla ya Zamalek aliyocheza msimu mmoja hadi 2011 na kuondoka kwenda Al Merreikh ya Sudan.

Kipindi El Hadary anakwenda El Merreikh na kuwa mchezaji anayelipwa mshahara mkubwa kuliko wote, ndiyo kipindi Wana-Simba “wataalamu umri” walipohakikisha Kaseja anaondoka Simba kwa kuwa alikuwa amezeeka.

Kaseja alikuwa hazina kwa Simba na taifa, alionekana hana uwezo tena, ni mzee. Watu wakakubali kwa faida ya wachache ambao waliona umaarufu au ukubwa wa Kaseja ni kama tatizo kwao. El Hadary akaendelea kucheza na kufanya vema, juzi ameiongoza Misri kuingia kwenye fainali nyingine ya Kombe la Mataifa Afrika (Afcon) na kama watawashinda Cameroon, basi litakuwa ni kombe lake la tano, ameishatwaa katika miaka ya 1998, 2006, 2008 na 2010.



Usisahau ametokea katika kizazi cha dhahabu cha Misri kilichoongozwa na akina Mohamed Aboutrika. Leo anaendelea kucheza, pia ni kiongozi wa vijana katika timu ya Misri.

Wakati El Hadary anaichezea Misri kwa mara ya kwanza 1996, Ramadani Sobhi ambaye anakipiga Stoke City ya England ndiyo alikuwa na umri wa mwaka mmoja tu. Binti yake wa kwanza, ana umri sawa na huo wa Sobhi.

Sasa El Hadary ameichezea timu ya Taifa ya Misri kwa zaidi ya miaka 20, sasa anacheza na wajukuu zake na anaendelea kuwa tegemeo na gumzo.

Mechi 153 za kimataifa akiwa na Misri, pekee ni Gianluigi Buffon wa Italia, Iker Casillas wa Hispania na Mohamed Al-Deayea wa Saudi Arabia ndiyo makipa wanaoweza kufananishwa naye wakiwa wanamzidi kumfikia au kufanana naye.

Watanzania wakiwemo mashabiki na viongozi wa Simba, wanaweza kujifunza kupitia El Hadary kwamba chuki ni tatizo, chuki inawaua wale ambao wangeweza kuwa msaada.


Hakuna ubishi, Kaseja bado alikuwa katika kiwango cha kuisaidia Simba zaidi. Ndiyo maana unaona, tangu ameondoka hakuna kipa mzawa aliyefikia nusu ya ubora wake na akawa msaada katika kikosi chao. Badala yake wamekuwa wakihangaika na makipa wa kigeni ambao pia wanalazimika kuwabadili.


Maisha ya Kaseja ndani ya Simba yalikuwa na thamani kubwa kwa kuwa alifanya mengi kwa moyo wa dhati. Anachokifanya leo El Hadary ni funzo kuu kwa vijana wa Misri na wengine wangependa kuvunja rekodi yake.

Kaseja alivyoondoka Simba, inaonekana hakuna haja ya kujituma au kuitumikia klabu muda mrefu kwa mafanikio kwa kuwa mwisho wake hauwezi kuwa na heshima au manufaa.


Kaseja kaondoka Simba kwa kuwa hata walio na mchezo usiofikia robo ya wa kwake, waligeuka kuwa wenye nguvu na wakamng’oa. Leo anaendelea kufanya kazi yake vizuri na huenda angekuwa bora zaidi kuliko sasa.

Kaseja anaweza kuwa sehemu ya watoto wa El Hadary, lakini mazingira ya kazi yake yalikuwa magumu kuliko El Hadary na akafanya vema zaidi. Hivyo lazima Watanzania tujenge tabia ya kuheshimu michango ya wanaofanya vema badala ya kuchukizwa na kuendelea kwao kufanya vema.

Haiwezekani El Hadary akatamba kama miujiza tu. Lazima ndani yake kuna juhudi, malengo na nidhamu ya juu bila ya kuyumba. Hali kadhalika, Kaseja amekuwa hivyo. Watu wamemshusha kwa kumvika uzee. Yeye na El Hadary nani mzee?




Lazima tubadilike, la sivyo watu walio katika soka sasa watakuwa hawajui au watashindwa kuelewa faida za kufanya vema kwa muda mrefu. Au watakosa sababu ya kuona umuhimu wa kujituma kwa kuwa wana hofu na mwisho wao.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic