February 20, 2017



Kikosi cha vinara wa Ligi Kuu Bara kinaendelea kujifua vilivyo kisiwani Unguja kwa ajili ya mchezo wake wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Yanga utakaofanyika Jumamosi ijayo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mchezo huo unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na vita iliyopo kati ya timu hizo ya kuwania ubingwa wa ligi kuu msimu huu ambapo mpaka sasa Simba ndiyo ipo kileleni ikiwa na pointi 51 wakati Yanga ipo nafasi ya pili ikiwa na pointi 49.

Hata hivyo, ili kuhakikisha Simba inaibuka na ushindi katika mchezo huo, kocha mkuu wa timu hiyo, Mcameroon, Joseph Omog amemtengea dakika 30 za mazoezi ya kufunga kila siku, mshambuliaji wake raia wa Burundi, Laudit Mavugo ili aiangamize Yanga.

Katika mazoezi ya timu hiyo huko Unguja, Omog amekuwa akimfua Mavugo pamoja na washambuliaji wengine wa timu hiyo kwa dakika 30 kila siku akiwapatia mbinu mbalimbali za kuzifumania nyavu kabla ya kuanza mazoezi ya pamoja na kikosi kizima.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Omog alisema kuwa amekuwa akifurahishwa na jinsi Mavugo anavyofanya vizuri katika mazoezi hayo lakini pia wachezaji wengine, hivyo anaamini atafanya vizuri dhidi ya Yanga.

“Tunaendelea vizuri na mazoezi yetu, wachezaji wote tuliokuja nao huku wapo vizuri hata wale waliokuwa majeruhi maendeleo yao siyo mabaya.

“Kuhusiana na Mavugo yupo vizuri anaendelea kujifua vilivyo na kila siku anazidi kufanya vizuri mazoezini kwa muda wote ambao nimekuwa nikiwafundisha, hivyo ni matumaini yangu ataendeleza rekodi yake ya kuzifumania kama alivyofanya katika mechi tatu zilizopita,” alisema Omog.

Simba ipo visiwani Zanzibar tangu Ijumaa iliyopita, hivyo leo wanafikisha siku ya nne visiwani humo.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic