December 30, 2019






Na Saleh Ally
LIVERPOOL ilishika nafasi ya pili katika Ligi Kuu England, nafasi ya pili katika Ligi ya mabingwa Ulaya wakati kocha mkuu akiwa ni Jurgen Klopp.


Klopp huyo raia wa Ujerumani, bado ni kocha mkuu wa Liverpool. Kwa sasa ndiye ameiwezesha kubeba mataji matatu makubwa ndani ya mwaka mmoja.


Liverpool hawataisahau 2019 kwa muda mrefu sana, wamekuwa mabingwa wa Ulaya, wamebeba ubingwa wa Super Cup ya Ulaya na sasa ni mabingwa wa dunia kwa klabu, wakifanikiwa kuishinda Flamengo ya Brazil.


Wakati wakiishinda Tottenham katika fainali ya Ligi ya mabingwa Ulaya, hakuna ubishi, Liverpool walionekana kweli walikwenda kucheza fainali wakiwa watu ambao walijifunza kupitia makosa yao ya fainali ya mara ya mwisho dhidi ya wababe Real Madrid ambao wakati wanakutana na Liverpool ilikuwa ni fainali yao ya tatu mfululizo na wakafanikiwa kubeba ubingwa kwa mara ya tatu mfululizo na kuandika rekodi mpya na ngumu kuivunja katika Ligi ya Mabingwa Ulaya.


Wakati wanakutana na mabingwa wa Europa League, Chelsea, hakuna aliyekuwa na uhakika, lakini uchezaji wao haukuwa ule wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. 


Walicheza tofauti kwa aina iliyoonekana wazi walitambua wanacheza na mabingwa wa upande mwingine wa Ulaya. Wakaibuka wababe na kuchukua Super Cup.


Kwa Kombe la Dunia, timu za England haziwezi kuwa na kelele nyingi sana, si michuano zinayofanikiwa kufika mara nyingi au kubeba kombe hilo mara kwa mara. Ni Manchester United pekee walikuwa wamelitwaa mwaka 2008 chini ya Alex Ferguson.


Mara ya mwisho, Liverpool walicheza fainali ya michuano hiyo mwaka 2005, wakakutana na Sao Paulo ya Brazil na kukubali kipigo cha bao 1-0, kombe likapelekwa Brazil.


Mwaka 2012, Chelsea nao wakaingia fainali, wakakutana na kipigo cha bao 1-0 kutoka Corinthias ya Brazil, kombe likaenda Brazil tena.


Kuanzia 2012, hakuna timu ya England iliyokuwa imegusa fainali ya michuano hiyo. Ikawa hivi; mabingwa wa Ulaya ni Bayern Munich, fainali dhidi ya Raja Casablanca (2013), mabingwa Real Madrid, fainali dhidi ya San Lorenzo (2014), bingwa FC Barcelona, fainali dhidi ya River Plate (2015), bingwa Real Madrid dhidi ya Kashima (2016), Madrid tena dhidi ya Gremio (2016), Madrid tena dhidi ya Al Ain (2018).


Mwaka 2019 umekuwa ni wa England na waliopeleka kombe ni Liverpool ambao wamefuta uteja wa timu za England dhidi ya zile za Brazil katika fainali ya Kombe la Dunia. Hakuna ubishi tena kuwa Kocha Klopp ni ufunguo mpya ambao umerudisha faraja na kutengeneza mwamko mpya ambao haukutegemewa.


Utaona jambo moja, wakati mwaka 2015 Klopp akitua Liverpool akitokea Borussia Dortmund, deni kubwa kwake lilikuwa ni kubeba ubingwa wa Ligi Kuu England ambao Liverpool kwao umekuwa ni kama “ugonjwa usio na tiba”.


Zaidi ya miaka 29 wamekuwa wakiusikia, lakini wamekuwa na mashabiki wenye roho ngumu zaidi ile ya paka, kwani wamebaki na kumbukumbu ya historia ambayo wengine hata hawakuwa wamezaliwa au kujitambua vizuri. Lakini wakaendelea kujivunia bila ya woga.


Walichotaka ni kubeba ni ubingwa wa England lakini Klopp anaonekana kutokana na namna walivyotaka Liverpool, yeye ameanza tofauti kabisa. Badala ya kuanzia chini kwenda juu, anatokea juu kurejea chini.


Ana ubingwa dunia, Super Cup ya Ulaya, ubingwa wa Ulaya na sasa anashuka kwenda kwenye ubingwa wa England ambao kiuhalisia hadi sasa inaonekana vigumu sana kuwazuia.


Kwa wanavyokwenda kama hakutakuwa na mabadiliko, suala la ubingwa kwao ni la kusubiri kwa kuwa wazi wanaonekana hawako tayari tena kufanya makosa ya msimu mmoja au miwili iliyopita na hilo wamalithibitisha kwa kubeba makombe matatu ndani ya mwaka mmoja.


Kikosi cha Liverpool, msimu uliopita kiliteleza mwanzoni na mwisho kikashindwa kuendana na kasi ya Manchester City. Safari hii, Klopp ameonyesha Liverpool hii si ile ya msimu uliopita, wanajua wanataka nini kwa wakati gani na mambo yanafanyika kwa wakati mwafaka.


Liverpool wanacheza kulingana na wanachotaka, wanashinda kutokana na wanayekutana naye. Bado hawajapoteza hata mchezo mmoja katika EPL ndani ya mechi 18 na wanaongoza kwa tofauti ya pointi 10 na anayeishika nafasi ya pili Leicester City, tena wakiwa na mechi mbili mkononi dhidi ya yake.


Uchezaji wao unaonyesha wazi, Liverpool hawakuchanganywa na kuukosa ubingwa wa Ulaya, kuukosa ubingwa wa EPL mwishoni lakini wakatumia muda wao kujifunza wapi walipokosea na Klopp amekuwa ufunguo wa Liverpool ya zamani yenye mambo ya kisasa na hakuna kinachoshindikana mbele yao kwa sasa kwa kuwa Klopp ni ufunguo mpya unaotumika kufungua mlango imara wa zamani.




1 COMMENTS:

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic